CCM chakipongeza Chadema kwa kukitua 'mzigo'


Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Rufiji kimepongeza hatua ya Chama cha Chadema kumchukua aliyekuwa kada wake Seleman Ndumbugani na kueleza kuhama kwake sawa na kuutua mzigo ulioshindikana.

Akizungumza na NIPASHE Jumamosi, Katibu wa Uenezi na Uhamasishaji wa Wilaya hiyo, Hemed Mnyeresa alisema CCM kamwe haisikitiki kuondoka kwa mwanachama wake huyo wa siku nyingi kutokana na kuwepo kwake kulikuwa na migogoro isiyokwisha na kusababisha chama hicho kuyumba.

Alisema kauli ya Ndubugai ambaye alikuwa Katibu wa Uenezi na Uhamasishaji wa Wilaya hiyo, kwamba ameondoka ndani ya Chama hicho kwa sababu kinaendeshwa kiukoo, hazina msingi na badala yake alimtaka aseme ukweli kilichomfanya aondoke.

Ndubugai alikihama chama hicho na kuhamia Chadema Desemba 13, mwaka huu, ambapo alinukuliwa na vyombo vya habari akisema aliondoka CCM kutokana na chama hicho Wilaya ya Rufiji kutawaliwa kiukoo.

Mnyeresa alisema chama hicho kinaendelea kuwabaini na kuwaondoa wanachama wote wanaodhani uongozi ni mali yao na kuwepo kwao humo ni moja ya maisha yao.

"Hatutaki watu wanaodhani wao hawawezi kushindwa kwenye uongozi na kuona ni mali yao milele, tunaendelea kuwasaka watu wa aina hiyo na kuwapa mkono wa kwaheri wakishindwa kufuata kanuni na maadili ya chama," aliongeza kusema katibu huyo.

Alisema Ndubugai aliingia nyongo na kuchukua hatua hiyo baada ya kushindwa nafasi hiyo katika uchaguzi uliopita, ambapo alianza kufanya mambo mbalimbali yanayokwenda kinyume na chama hicho na alipoona kuna dalili ya kumuondoa aliamua kujiondoa mwenyewe.

Hata hivyo, katibu huyo alieleza kwa sasa CCM imejikita katika kuhakikisha kinaondoa kero zinazowakabili wananchi wa chama hicho ikiwemo kuishinikiza serikali kutafuta soko la korosho pamoja na kusimamia usambazaji wa zana za kilimo katika msimu huu wa kilimo.

CHANZO: NIPASHE

Sh Milioni saba ‘zafichwa’ akaunti binafsi


Mratibu Elimu kata wilayani Nzega mkoa wa Tabora amekiri kuchukua pesa za ujenzi wa shule na kuweka kwenye akaunti yake.

Mratibu huyo, Richard Nkwabi wa Kata ya Puge wilayani Nzega alikiri kuweka fedha hizo baada ya malalamiko ya wananchi wa kata hiyo kumshutumu  yeye pamoja na diwani Alex Nyasani kujichukulia maamuzi ya kuweka pesa za maendeleo ya ujenzi wa majengo mawili ya shule ya kidato cha tano na sita ya shule ya sekondari Puge kwenye akaunti binafsi.

Shutuma nyingine zilizotolewa na wananchi hao kwa viongozi wao ni kutekeleza mradi wa madarasa hayo na kuuhamishia sehemu nyingine kwa lengo la kujitafutia njia ya ‘kutafuna’ pesa hizo za serikali.

Akizungumza na NIPASHE Jumapili kwa njia ya simu toka wilayani Nzega, Nkwabi alikiri na kusema kiasi cha Sh.milioni 7.4, zimewekwa katika akaunti yake Novemba 30, mwaka huu katika benki ya NMB tawi la Nzega kutokana na kutekeleza maamuzi ya Kamati ya Maendeleo ya Kata (OBC).

"Kweli kiasi hicho kimewekwa katika akaunti yangu ya NMB tawi la Nzega, lakini nimetekeleza maagizo ya OBC yaliyonitaka nifanye hivyo...hizo ni kati ya Sh.milioni 13 zilizotolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa shule," alisema Nkwabi.

Nkwabi alisema Sh.milioni sita kati ya 13, zilitumika kununulia vifaa vya ujenzi yakiwemo mabati, lakini kiasi kilichobaki kamati iliamua ziwekwe kwenye akaunti binafsi hadi hapo watakapofungua ya kamati ya ujenzi.

“Kweli pesa ziliingia tangu Juni mwaka huu, lakini kutokana na kuhofia kurejeshwa zilikotoka, ikaamuriwa nyingine zitumike kwa kununulia vifaa na nyingine ziwekwe kwenye akaunti yangu,” alisema.

 “Tunaamini lengo la viongozi hao na kamati yao, walikuwa na mpango wa kutafuta njia ya kuudhoofisha mradi huo ikiwa ni pamoja na kuhamisha ujenzi ambao tayari ulikuwa umeanza sehemu iliyopendekezwa na wananchi na kupeleka kwingine, lakini mbaya ni pesa za mradi kuwekwa akaunti binafsi,” alisema mmoja wa wananchi walalamikaji.

Aidha, walielekeza shutuma kwa Diwani wao, Alex Nyasani kwa kuruhusu ujenzi kufanyika wa shule kufanyika sehemu nyingine bila kuhusisha vikao vya wananchi wenye kutoa maamuzi.

Lakini wananchi hao wanasema, mvutano uliopo sasa na viongozi wao ni kushindwa kuwaeleza kuiendeleza shule hiyo ambayo ilipewa baraka na viongozi wa serikali na pesa zake kupewa halmashauri ili izigawe kwa ajili ya muendelezo wa shule hiyo ambayo mpaka sasa madarasa yake mawili yamesimama hatua ya madirishani.

Pia, wananchi hao walisema madarasa ya shule hiyo yamejengwa sehemu yenye nafasi na pia ni jirani na ilipo hosteli ya wanawake wa shule ya Puge, jengo la utawala na maabara, hivyo kuanzishwa kwa ujenzi mwingine kunaashiria ‘utafunaji’ wa pesa hizo.

Hata hivyo, diwani wa kata hiyo, Nyasani akizungumzia shutuma hizo za wananchi wa kata yake, alisema hayana msingi kutokana na kinachofanyika ndicho kinachotakiwa kwa ajili ya maendeleo ya kata ya Puge.

Wakati Nkwabi akikiri kuweka pesa za ujenzi wa shule katika akaunti yake, diwani Nyasani alimtetea na kusema hakuna kitu kama hicho, na kuirushia mpira kamati ya maendeleo ya kata.

Usafiri Ubungo ni balaa tupu

Kituo cha mabasi Ubungo 

WAKATI abiria wanaendelea kulalamikia kupanda kwa nauli za mabasi yaendayo mikoani, hali ya usafiri katika Kituo Kikuu cha mabasi Ubungo imezidi kuwa mbaya.


Hali hiyo imekuja kutokana na kuwapo kwa abiria waliokwama kuelekea mikoa ya kaskazini na nyanda za juu kusini kutokana na uchache wa mabasi.


Mwananchi lilishuhudia abiria wakiwa wamekwama kituoni hapo bila ya kupata ufumbuzi kuhusu safari zao huku wakiwatupia lawama wamiliki wa mabasi, kuwa ndio chanzo cha usumbufu wanaoupata.


Walidai kuwa wamiliki hao wamekuwa wakifanya makosa na hatimaye kufungiwa kwa kampuni zao hali inayosababisha kuwapo kwa uhaba wa mabasi.


Wakizungumzia usumbufu huo, baadhi ya abiria walisema hali hiyo imekuja baada ya kuwapo kwa abiria wengi wanaokwenda mikoani kwa ajili ya sherehe za mwisho wa mwaka.
“Sisi tuko hapa kituoni tangu asubuhi na bado hatujapata uhakika wa safari kwani abiria ni wengi, ikichangiwa na uhaba wa magari uliojitokeza kwa sasa, tunapata usumbufu wa kuja kituoni na kurudi nyumbani,” alisema mmoja wa abiria hao.


Abiria huyo aliyetajitambuliasha kwa jina moja la Jesca alidai kuwa baadhi ya kampuni zinazomiliki mabasi hayo, zimekuwa zikifanya makosa ya mara kwa mara ambayo yanaweza kuepukika na matokeo yake, wanajikuta wakifungiwa kutoa huduma.


“Kuna makosa mengine yasiyo ya lazima ambayo yanaweza kuepukika ni vyema kampuni miliki zikachukua tahadahari napema ili kuepuka adha unayo tukumba,” alisema Bibi Jesca
Abiria waliokwama katika kituo hiko ni wale wanosafiri kutoka jijini Dar es Salaam kwenda mikoa ya Tanga, Moshi, Arusha na mikoa ya Iringa na Mbeya.

Arfi atupa kadi ya Chadema kikaoni

 Makamu Mwenyekiti wa chadema  Taifa, Said Arfi 

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimezidi kuandamwa na migogoro baada ya jana kuibuka mwingine mkubwa katika kikao chake cha ndani mkoani Katavi kiasi cha kumfanya Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Said Arfi, kutupa kadi yake ya uanachama.


Huu ni mgogoro wa pili mkubwa kuripotiwa katika kipindi cha juma moja lililopita baada ya ule wa wilayani Karatu ambako pamoja na mambo mengine uliishia kwa Kamati Kuu kuusimamisha uongozi wote wa chama hicho wilaya.


Taarifa zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kuwa Arfi ambaye ni Mbunge wa Mpanda Mjini, alitishia kujitoa Chadema jana, katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya chama hicho Mikoa ya Katavi na Rukwa kilichoketi Namanyere, Nkasi na kufikia uamuzi wa kumsimamisha Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Mkoa wa Rukwa, Laurent Mangweshi.


Katika kikao hicho, Arfi anadaiwa kuichukua kadi yake ya Chadema na kumtupia Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Rukwa, John Mallack akitangaza kuachia nyadhifa zote alizonazo, kisha kuondoka ukumbini, kabla ya kufuatwa na wazee wa chama hicho na kumsihi aichukue kadi yake hiyo.


Alifikia hatua hiyo baada ya kutokea sintofahamu kati ya wajumbe wa kikao hicho katika uamuzi huo uliofikiwa kwa kupiga kura za ndiyo na hapana.
Vyanzo vya habari kutoka ndani ya kikao hicho vilifafanua kuwa Arfi alikerwa na kauli iliyotolewa na Mangweshi kuwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita, alipokea rushwa kutoka kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.


Vyanzo hivyo vya habari vimeeleza kuwa kutokana na hali hiyo, Arfi alipandwa na hasira na kuamua kumrushia kadi Mallack kisha kutoka nje ya ukumbi.


“Hatua hiyo ilifanya wajumbe wa kikao hicho nao kutoka nje ya ukumbi na kuanza kumbembeleza ili asichukue uamuzi huo na kisha wakamwekea kadi yake ya uanachama katika mfuko wake wa shati,” alisema mmoja wa makada hao.


Arfi mwenyewe hakupatikana jana kuzungumzia tukio hilo baada ya simu ya mkononi kuita muda wote bila kupokewa na hata alipotumiwa ujumbe, hakujibu.


Mallack akizungumza na gazeti hili kwa simu alikiri Arfi kurusha kadi mezani kisha kutoka nje ya ukumbi, lakini akasema suala hilo lilishughulikiwa na wazee na kumalizwa.
“Ni kweli unajua huyu ni Makamu Mwenyekiti wetu wa Taifa, sasa inapotokea vijana wadogo wakamtuhumu kwa tuhuma za uongo na ambazo hazipo inatia hasira, ndiyo maana huyo kijana tumemvua uongozi,” alisema Mallack.

Tuhuma za Mangweshi
Mangweshi alisimamishwa uongozi baada ya kutuhumiwa kwa mambo mbalimbali ya kiutendaji ndani ya chama hicho ikiwamo kumkashifu Arfi.


Katika mkutano wake na waandishi wa habari, Mallack alisema kuwa Magweshi amevuliwa uongozi baada ya chama hicho kujiridhisha kuwa alitenda makosa hayo.
Alisema kamati ya ushauri ilimwita ili kujibu tuhuma mbalimbali zilizokuwa zikimkabili ikiwamo kutoa taarifa zisizo rasmi bila kufuata taratibu za chama.


“Pia amepatikana na hatia ya kuandika barua za kashfa na kuzipeleka makao makuu ya chama kumkashifu Arfi pamoja na viongozi wengine wa chama akiwamo Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa.


Katibu Mwenezi wa Chadema Mikoa ya Rukwa na Katavi, John Matongo alisema kabla ya kupewa adhabu ya kusimamishwa, amewahi kuonywa mara kadhaa lakini ameshindwa kujirekebisha.“Hali hiyo ya mwenyekiti ingeachwa iendelee, ingeweza kuleta mgawanyiko na uchonganishi kwa viongozi wa kitaifa,” alisema.


Hata hivyo, inaelezwa kuwa kikao hicho hakikuendeshwa kwa amani baada ya pande mbili zinazovutana kutofautiana waziwazi kuhusu uamuzi wa kumsimamisha mwenyekiti huyo kiasi cha kulazimu hatua hiyo ifikiwe kwa kupiga kura.
Kura hizo zilipigwa na wajumbe 36 na matokeo yakaonyesha kuwa 24 waliafiki uamuzi huo na 12 kuukataa.
Akizungumza na mwandishi wetu, Magweshi alisema “Sina taarifa yoyote juu ya tukio hilo kwani sina barua rasmi.”
Alipoulizwa kama alishiriki kikao hicho, alikubali na kusema kilikuwa kikijadili mambo mbalimbali ya chama hicho.

Tanga nako si shwari
Uongozi wa Chadema mkoani Tanga umeapa kumshughulikia Katibu wa Baraza la Vijana mkoani hapa, (Bavicha), Deogratias Kisandu kwa kile kilichoelezwa kuwa ni utovu wa nidhamu.


Akizungumza na waandishi wa habari, katibu wa chama hicho Mkoa wa Tanga, Saidi Mbwete alisema kitendo cha Katibu huyo kumtaka Dk Slaa ajiuzulu kwa kumiliki kadi ya CCM ni utovu wa nidhamu.


“Kurudisha kadi ya chama cha awali, ni hiari ya mwenye kumiliki kadi hiyo kwani ni yake kwa sababu ameinunua na kuilipia,” alisema Mbwete.

Mgogoro wa Karatu
Wakati hayo yakiendelea mgogoro wa Wilaya ya Karatu, umechukua sura mpya baada ya wajumbe wa Kamati ya Utendaji Wilaya hiyo kugoma kujiuzulu kwa maelezo kuwa Kamati Kuu ya Chadema haina mamlaka ya kuwaondoa.


Wakati viongozi hao wakitoa tamko hilo jana, tayari Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo wa Chadema, Benson Kigaila ametua Karatu jana, kufanya maandalizi ya mikutano ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuanzia Jumamosi hadi Jumapili ili kukutana na viongozi wa chama hicho wadau wake katika kile kinachoelezwa kuweka “mambo sawa.”


Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Karatu, Moshi Darabe na Mbunge wa Karatu, Mchungaji Israel Natse walisema jana kwamba wamesikitishwa na uamuzi ya kamati kuu ya kutangaza kusimamisha kamati hiyo yenye wajumbe 17 bila kuwasikiliza.


Darabe alisema awali, Kamati ya Utendaji ya Karatu, ndiyo ilikuwa inawatuhumu baadhi ya viongozi kwa kudhoofisha chama hicho na kushauri wachukuliwe hatua ambao ni Diwani wa Karatu Mjini, Jubilate Mnyeye, Katibu wa Wilaya hiyo, Raurence Bortha, Mwenyekiti wa Bavicha Wilaya, Joseph Mtui na Katibu wake, Melkiori Mao.


“Sasa kamati kuu iliwaita na kuwahoji, tulitarajia wangetoa uamuzi kuhusiana na tuhuma tulizowapa lakini kusimamisha kamati nzima tunadhani si sahihi na pia ni ukiukwaji wa katiba ya chama,” alisema Darabe.


Natse alisema kikatiba, wanaamini kamati ya utendaji inaweza kuwajibishwa na mkutano mkuu wa wilaya na siyo kamati kuu.


Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema jana kuwa kimsingi, uamuzi uliofanyika ni wa kuisimamisha kamati ya utendaji kufanya kazi na si kuivunja au kuifukuza.


Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo alisema wakati huu ambao kamati hiyo imesimamishwa, Kamati Kuu ya chama ndiyo inayofanya uangalizi wa moja kwa moja kwa Wilaya ya Karatu kupitia mfumo itakaouweka hadi uamuzi mwingine utakapotolewa.

Hukumu rufaa ya Lema yaiva

 

Habari zilizopatikana jana kutoka mahakamani hapo zilisema kuwa jopo la majaji watatu waliosikiliza rufaa hiyo limeshakamilisha kuandika hukumu yake na kwamba itasomwa kesho kuanzia saa 3:00 asubuhi.

Lema ambaye ni kada wa Chadema, alivuliwa ubunge Aprili 5, mwaka huu katika hukumu iliyotolewa na Jaji Gabriel Rwakibalia kutokana na kesi iliyofunguliwa na makada watatu wa CCM; Mussa Mkanga, Happy Kivuyo na Agnes Mollel, wakipinga ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa 2010.

Pamoja na kumvua ubunge, Jaji huyo pia alimwagiza Msajili wa Wilaya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha kuiarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), kuhusu Lema kutiwa hatiani na kuhukumiwa kwa Kifungu cha 114 cha sheria ya uchaguzi ambacho kinamnyima kupiga au kupigiwa kura kwa kipindi cha miaka mitano.

Matumizi ya kifungu hicho ni miongoni mwa hoja zilizowasilishwa na Lema kupitia kwa mawakili wake akidai Jaji alikosea kwa sababu makosa yaliyomvua ubunge hayaangukii kwenye vitendo vya rushwa, kuzuia watu kupiga kura.

Jaji Rwakibarila alimvua Lema ubunge baada ya kuridhika kuwa alitumia lugha na kauli za udhalilishaji dhidi ya aliyekuwa mgombea wa CCM, Dk Batilda Burian), inayoangukia kwenye Kifungu cha 113.

Kutokana na hukumu hiyo, Lema, kupitia kwa mawakili wake Method Kimomogoro na Tundu Lissu alikata rufaa Mahakama ya Rufani, akiwasilisha hoja 18 za kuipinga.

Hukumu ya Jaji Rwakibarila pia ilipingwa na mawakili wa Serikali waliokuwa wakimwakilisha Mwanasheria Mkuu katika shauri hilo, Timon Vitalis na Juma Masanja ambao wanadai haina hadhi ya kuitwa hukumu kutokana na kujaa dosari za kisheria.

Hata hivyo, wakati Lema akikata rufaa, warufaniwa; Mkanga, Mollel na Kivuyo nao waliwasilisha rufaa kupitia kwa Mawakili wao, Alute Mughwai na Modest Akida kupinga uamuzi wa Jaji Rwakibarila kutupilia mbali baadhi ya madai yao.

Lema na mmoja wa wakili wake, Kimomogoro jana walithibitisha kwa nyakati tofauti kupokea hati za kuitwa mahakamani kusikiliza hukumu hiyo.

Taarifa kwamba hukumu itasomwa kesho zilitawala Jiji la Arusha jana na viongozi wa Chadema wakiongozwa na Katibu wa Mkoa, Amani Golugwa walionekana wakijiandaa kuelekea Dar es Salaam kusikiliza uamuzi huo.
Akizungumza kwa simu jana alasiri, Golugwa alisema ataongoza kundi la wanachama na viongozi zaidi ya 40 kutoka Arusha kwenda Dar es Salaam leo.

Rufaa
Rufaa hiyo ilisikilizwa na jopo la Majaji, Salum Massati, Bernard Luanda wakiongozwa na Jaji Nathalia Kimaro.

Siku ya usikilizwaji upande wa wajibu rufaa waliweka pingamizi dhidi ya rufaa ya Lema, wakidai kuwa ilikuwa na dosari za kisheria, huku wakiomba Mahakama hiyo itupilie mbali bila kutoa nafasi yoyote ya kukatwa upya.

Katika uamuzi wake dhidi ya pingamizi hilo, Novemba 8, 2012 Mahakama ya Rufani ilitupilia mbali rufaa hiyo ya Lema baada ya kukubaliana na hoja za pingamizi lakini ikatoa fursa ya kukatwa upya katika muda wa siku 14 kwa mujibu wa Kifungu cha 111 cha Kanuni za Mahakama ya Rufani.
Baada ya kufanya marekebisho hayo ndani ya muda huo kama alivyoamuriwa na Mahakama, ilisikilizwa Desemba 4, 2012.

Hoja za warufani
Lema aliyeibuka na ushindi wa zaidi ya kura 19,000 dhidi ya Dk Burian, anadai Jaji Rwakibarila alimvua ubunge kwa kuzingatia ushahidi wa mdomo usio na nyaraka za kuuthibitisha kinyume cha sheria.

Alitoa hoja 18 kupinga hukumu hiyo na pia alimtuhumu Jaji Rwakibarila kutozingatia ushahidi wake na mashahidi wake watatu kwa madai kuwa walikuwa wanachama na viongozi wa Chadema, hivyo walikuwa na masilahi, lakini papohapo akakubali na kutumia ushahidi wa wanachama na viongozi wa CCM.

Kwa upande wake, Wakili Vitalis alidai kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ilikosea kutengua ubunge wa Lema, kwa madai ya kutumia lugha za matusi, akidai kuwa Bunge limeruhusu wanasiasa kutukanana kwenye kampeni.

Alisema kwa mujibu wa Kifungu cha 108 cha Sheria ya Uchaguzi , Sura ya 313 ya 2010, matusi si miongoni mwa mambo ambayo yanaweza kutengua matokeo ya uchaguzi na kwamba Bunge liliruhusu kutukana kutoka na kufanya marekebisho ya  Sheria ya Uchaguzi ya 1995 baada ya hukumu ya kesi kati ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Aman Walid Kabouru.

Vitalis alidai kuwa sheria ilikuwa ikiruhusu matokeo ya uchaguzi kutenguliwa kutokana na lugha za matusi, lakini baada ya hukumu ya kesi ya Kabouru Januari 1995, Julai mwaka huo Bunge lilifanya marekebisho na kuondoa suala la matusi katika mambo yanayoweza kutengua uchaguzi.

Pia alidai kuwa kifungu cha 108 (2) cha Sheria ya Uchaguzi kinaeleza aina za ubaguzi zinazokatazwa ni pamoja na wa kidini na kikabila na kwamba aina nyingine kama makazi (Uzanzibar, Ubara) hazijatajwa.

Wakili  Vitalis alidai kuwa wajibu rufaa hawakuwa na haki ya kufungua kesi kupinga ushindi wa mrufani (Lema), kwa kasoro zilizotokea wakati wa kampeni kwa sababu hawakuwa wahusika katika mchakato wa kampeni za uchaguzi huo.

Vitalis alidai kuwa anayepaswa kufungua kesi mahakamani kwa madai ya lugha ya matusi ni yule aliyetukanwa kwa kuwa hayo ni maumivu ya mtu binafsi na kwamba hata anapokufa, madai yake nayo hufa wala hayawezi kuendelezwa na mtu mwingine.
“Sasa iweje kwa mtu ambaye yuko hai lakini watu wengine ndiyo waje mahakamani kufungua kesi?” alihoji wakili huyo.

Warufaniwa
Hata hivyo, hoja hizo zilipingwa na Wakili Mughway akidai kuwa si kweli kwamba Bunge limeruhusu kauli za matusi kwenye kampeni.

“Sikubaliani na maneno ya AG (kupitia Wakili Vitalis) kuwa ni ruksa wanasiasa kutukanana,” alisema na kusisitiza kuwa madhumuni ya kukataza vitendo hivyo ni kudumisha siasa safi na kuhakikisha nchi inatawaliwa na siasa safi.

Alisema kwa mujibu wa Kanuni ya 2 (2) (b), viongozi na wagombea hawatakiwi kutumia lugha za matusi wala kejeli za namna yoyote wala udhalilishaji wa namna yoyote.

Katika rufaa yao, warufaniwa hao walidai kuwa Jaji Rwakibalira alikosea katika hukumu yake kwa kuchanganya vituo vilivyotolewa ushahidi na mashahidi wanne na hatimaye akakataa ushahidi mmojawapo, pamoja na tarehe za ratiba ya kampeni za CCM na Chadema.

Pia walidai  Jaji alikosea kwa kuamua kuwa hata kama Lema kwenye kampeni zake alidai kuwa Dk Burian ni mkazi wa Zanzibar, na hatafaa kwa hiyo  ukazi si sifa ya kuchaguliwa kuwa mbunge.

Mbivu, mbichi darasa saba wakati wowote

Naibu Waziri wa wizara hiyo, Phillip Mulugo

Wizara  ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, inatarajia kutangaza matokeo ya Mtihani wa Taifa wa darasa la saba uliofanyika Septemba, mwaka huu wiki hii au mwanzoni mwa wiki ijayo.

Naibu Waziri wa wizara hiyo, Phillip Mulugo, aliliambia NIPASHE kutoka Mbeya kuwa wamepanga matokeo ya darasa la saba yatolewe wiki hii na kama itashindikana, basi mwanzoni mwa wiki ijayo.

Tangu wiki iliyopita, wananchi wamekuwa wakiuliza matokeo ya darasa saba ili kama watoto wao watamechaguliwa kuendelea kidato cha kwanza, wafanye maandalizi.

Imekuwa kama mazoea miaka ya nyuma matokeo ya mitihani darasa la saba kutolewa kabla ya  Krismas.

Hata hivyo, mwaka huu wananchi wameingiwa na wasiwasi kutokana na kusalia siku chache kufikia Krismasi.

Katibu wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), Dk. Joyce Ndalichako, alisema watahiniwa 894,881 walifanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka huu.

Alisema kati ya watahiniwa hao waliosajiliwa, wavulana ni 426,285 sawa na asilimia 47.64 na wasichana 468,596 sawa na asilimia 52.36.

Mitihani hiyo ya mwaka huu ilifanyika  kwa mfumo mpya wa usahihishaji unajulikana kama ‘Optical Mark Reader’ (OMR).

Watahiniwa walitumia fomu maalum za teknolojia kujibia maswali zitakazosahihishwa kwa mashine maalum.

Mfumo huo una lengo la kupunguza ubabaishaji wa matokeo kwa ujumla kwa watahiniwa hao.

CHANZO: NIPASHE

Polisi Dar bado wawasaka walioua, kupora milioni 150/-


Jeshi  la polisi nchini limesema linaendelea na uchunguzi wa kuwabaini waliohusika na tukio la uporaji wa Sh. milioni 150 eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na NIPASHE, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala, Marietha Minangi, alisema jeshi la polisi bado linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo na hakuna mtuhumiwa mwingine aliyekamatwa.

Alisema polisi wanaendelea kuwahoji vijana wawili wasukuma mikokoteni wanaotuhumiwa kuhusika na tukio hilo na kama watabaini kuwa hawakuhusika, watachiwa.

Kamanda Minangi alisema mpaka sasa fedha hizo zilizoibiwa hazijapatikana.

Hata hivyo, alisema polisi wanahisi majambazi wawili waliofanikiwa  kukimbia, walitoroka na kiasi hicho cha fedha.

Alisema majeruhi wa tukio hilo wanaendelea vizuri katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Tukio hilo la ujambazi lilitokea juzi katika mtaa wa Livingstone na  Mahiwa eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam.

Mbali na kuchukua kiasi hicho cha fedha, majambazi hao waliwaua watu wawili na kuwajeruhi wengine watatu.


JICHO LETU KATIKA MAGAZETI DESEMBA 20

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.