Mbowe ambana Pinda bungeni

Mboye 


SAKATA la gesi limetua rasmi bungeni baada ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Freeman Mbowe kuitaka Serikali iweke hadharani mikataba ya utengenezaji wa bomba la kusafirishia gesi hiyo kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam ili kuondoa usiri uliogubika mradi huo.
Mbowe alitoa wito huo jana alipokuwa akimuuliza Waziri Mkuu, Mizengo Pinda maswali bungeni katika kipindi cha Maswali na Majibu kwa Waziri Mkuu.

“Mheshimiwa Waziri ni dhahiri kuwa vurugu za Lindi na Mtwara zimesababishwa na mawasiliano hafifu kati ya Serikali na wananchi, ikiwamo kauli za viongozi wa Serikali na CCM je, ni kwa nini Serikali isiwachukulie hatua za uwajibikaji watumishi wa Serikali na vyombo vya ulinzi na usalama ambao wanaonekana dhahiri kuhusika,” alihoji Mbowe.


Kiongozi huyo wa upinzani alimtaka Waziri Mkuu kueleza ni kwa nini Serikali isiweke wazi mikataba yote ya gesi ili kuondoa hofu iliyojengeka kwa wananchi kwamba kumekuwa na hali ya ufisadi.


Akijibu swali hilo, Pinda aliwataka wabunge kutumia utaratibu mzuri wa kupata mikataba hiyo akisema haiwezekani ikawekwa hadharani.


Mbali na jibu hilo, Pinda alivitupia lawama vyama vya siasa akisema vimechangia kwa kiasi kikubwa mgogoro wa gesi mkoani Mtwara.

Licha ya juzi kueleza kuwa kulikuwa na mgogoro wa viongozi ndani ya mkoa huo pamoja na CCM, jana alikwepa swali la kutaka wahusika wawajibike na badala yake akasema suala hilo liko juu yake.


Alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali lingine la Mbowe ambaye alimtaka Pinda kutoa kauli juu ya nani aliyesababisha mgogoro wa Mtwara uliosababisha maafa.


Hata hivyo, alitangaza neema kwa waathirika kwamba Serikali inaangalia namna ya kuwapunguzia gharama wale wote waliopatwa na matatizo hayo ikiwamo kuwalipa fidia.
“Vyama vya siasa vimechangia kwa kiasi kikubwa katika kupotosha jambo hilo, ushindani wa chaguzi zinazokuja umejitokeza pia,” alijibu Pinda.


Kiongozi huyo alisema wanaofanya uchochezi huo wanafanya bila ya kujua kwamba unaweza kuwakumba watu wote wakiwamo hao wanaofanya hivyo.
“Tutalaumiana wengi lakini ni vyema kuweka mambo hadharani na kwamba ni hatari kufanya mambo kama hayo kwani amani ya nchi ni lulu ambayo ikipotea inaweza kuwa tabu kuipata.”


Alipinga hoja ya Mbowe kuwa Serikali inatekeleza majukumu yake baada ya shinikizo na maandamano ya wanasiasa.

Alilieleza Bunge kuwa wananchi wa Mtwara wanaweza kupoteza fursa nyingi kutokana na wawekezaji kuanza kuondoka wakikwepa vurugu na kukimbilia Msumbiji ambako kuna dalili za gesi pia.


Kamati ya Makinda yayeyuka
Jana, Spika wa Bunge Anne Makinda aliliambia Bunge kuwa Kamati aliyotarajia kuiunda haitakuwapo kutokana na ukweli waliokuwa wakiutaka kutoka Mtwara kuelezwa na Waziri Mkuu.

 Akiahirisha Bunge mchana wa Januari 29, mwaka huu, Makinda alitangaza kuwa angeunda kamati ya Bunge kwenda Mtwara kuangalia mgogoro huo.
“Kutokana na ukweli uliotolewa na Waziri Mkuu leo bungeni, naomba nimshukuru sana kwa dhati kwa kulishughulikia tatizo la Mtwara, lakini nieleze kuwa nilikusudia kuunda tume kwa ajili ya kwenda kutazama suala hilo, lakini tayari tumepata ukweli hivyo naona haina haja ya kuunda tume hiyo,” alitangaza Makinda.

Moto bungeni
Hoja binafsi ya Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia inayokosoa mfumo wa elimu Tanzania kwa shule za msingi na sekondari kuwa ni dhaifu na hauleti matumaini kwa wanafunzi, ilizua mjadala mzito bungeni jana baada ya Serikali kukataa pendekezo lake la kuunda kamati maalumu ya kutafuta chanzo cha tatizo hilo.


“Kutokana na hayo, ninaliomba Bunge lako tukufu kuunda Kamati Teule ya Bunge kuchunguza kina cha udhaifu huo wa kimfumo katika sekta ya elimu hapa nchini na kupendekeza hatua za kuchukua ili taifa liondokane na aibu ya udhaifu huo,” alisema Mbatia.


Baada ya hoja hiyo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa alipangua hoja moja baada ya nyingine na kuliomba Bunge lisikubali kuundwa kwa kamati teule, bali liiagize Serikali kushughulikia suala hilo.


Baada ya Dk Kawambwa kutoa hoja hiyo, Mbatia alisimama na kuikataa akisema kile alichokiainisha juu ya udhaifu hakifanani na kutaka kuundwa kamati kupitia kila hatua yenye udhaifu.


Baada ya Mbatia kusema hayo, ulizuka ubishi baada ya Spika Makinda kutaka kujadiliwa kwa mabadiliko ambayo Serikali inataka au hoja ya Mbatia iendelee.


Akichangia hoja hiyo, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu alisema kuna kila sababu ya kuunda kamati lakini iwe teule ya Bunge.
“Tunatakiwa tujadili kwanza hoja iliyoko mezani na si kujadili mabadiliko ya hoja Mheshimiwa Spika, hoja aliyotoa Mbatia isibadilishwe kwa kuwa ni kinyume na kanuni za Bunge lako tukufu,” alisema Lissu.


Baadaye walisimama wabunge zaidi ya watatu wakitaka kuchangia lakini Spika Makinda alitoa nafasi kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi ambaye alisema: “Tukiunda tume itachukua muda... Hoja iliyotolewa na Mbatia ni ya msingi, sasa kamati za Spika zishirikiane na Wizara ya Elimu kufanya kazi hiyo.”


Mbunge wa Nyamagana (Chadema), Ezekiah Wenje alisema haiwezekani Bunge likakubali Serikali ijichunguze yenyewe kwa kuwa ni kitu ambacho hakikubaliki na ni kinyume cha kanuni za Bunge.


Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka (CCM) alisema kuna matatizo katika sera, mitalaa na muhtasari na kusema sasa ni kazi ya Bunge kupata tume stahiki.

Kumi wafa kwa ajali ya boti Zanzibar

Msemaji wa Mkuu wa Polisi nchini, Advera Senso 


George Njogopa

BOTI ya abiria iliyokuwa ikitokea Pangani mkoani Tanga kwenda Zanzibar ikiwa na watu 32 juzi usiku ilizama katika eneo la Nungwi, Mkoa wa Kaskazini Zanzibar ambapo watu 10 wanahofiwa kuwa wamepoteza maisha.


Taaarifa zilizofikia gazeti hili jana jioni zilisema kati ya abiria 27 na wafanyakazi watano waliokuwa kwenye boti hiyo, ni watu 20 tu waliokuwa wameokolewa wakati wengine 10 wakiwa hawajulikani walipo.


Msemaji wa Mkuu wa Polisi nchini, Advera Senso alisema jahazi liitwalo Sunrise liliondoka Tanga juzi saa 2:00 usiku kuelekea Zanzibar, lakini lilipigwa na dhoruba katika eneo la Nungwi.


“Mpaka sasa watu 22 wameokolewa akiwamo nahodha Abdallah Selemani, kumi wanatafutwa ijapokuwa wanahofiwa kuwa wameishakufa. Kati ya hao ni watoto watatu na watu wazima ni saba,”alisema Senso katika ujumbe alioutuma kupitia simu yake ya mkononi.


Aliendelea: “Boti kutoka Tanga ipo kwenye eneo la tukio kusaidia uokozi na wakazi wa Kaskazini Unguja wamepokea watu waliookolewa na kuwapa huduma. Taarifa zaidi tunaendelea kufuatilia Tanga na Zanzibar”.


Hata hivyo idadi ya watu waliookolewa kwa mujibu wa Senso ilitofautiana na ile iliyokuwa imetolewa awali na Kamanda wa Wanamaji na Bandarini Zanzibar, SP Martin Lisu aliyesema juhudi za kuwaokoa abiria hao zilikuwa zikiendelea na kwamba waliokuwa wamepatikana wakiwa hai ni watu 21.

Lisu alisema abiria hao walionusurika kifo walipelekwa hospitalini kwa ajili ya kuchunguzwa afya zao na wengine walipatiwa huduma za kwanza kutokana na mshtuko walioupata.


“Kusema kweli tulifanikuwa kuwaokoa abiria 21 na wengine siwezi kusema kama wamezama ila nachoweza kusema ni kwamba bado hatujawapata,” alisema Kamanda Lisu na kuongeza:
“Taarifa nilizonazo ni kwamba, hii boti ilikuwa ikitokea Pangani, ilipofika eneo la Nungwi ikakubwa na dhoruba kali na kisha kuanza kupoteza mwelekeo”.

Eneo la Nungwi
Eneo la Nugwi lina historia ya kusababisha ajali za mara kwa mara na mara ya mwisho ndiko ilitokea ajali ya meli ya MV Spice Islander iliyosababisha vifo vya zaidi ya watu 400 mwaka 2011.


Ajali hiyo ilielezwa kusababishwa na uzembe wa baadhi ya watendaji ikiwemo kukosekana kwa ukaguzi kabla ya meli hiyo kuondoka.Taarifa zilizema kuwa meli hiyo ilizidisha idadi ya abiria na mizigo hivyo ilipofika eneo la Nungwi ilizidiwa na kuanza kuzama.


Katika kujaribu kusaka ukweli wa mambo, Rais wa Zanzibar, Dk Ally Mohamed Shein aliunda tume maalumu kuchunguza mazingira yaliyosababisha ajili hiyo.
Ripoti ya tume hiyo ilifichua uzembe uliojitokeza kwenye mamlaka husika na kupendekeza hatua kadhaa ili kuimarisha hali ya usafiri kwenye maji.


Ajali nyingine kubwa ni ya meli ya MV Skagit iliyotokea mwaka jana ikiwa inakaribia katika bandari ya Zanzibar, ambayo hatua za awali za uokoaji zilishindikana na kusababisha vifo vya mamia ya watu.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI FEB.1

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

Kijana atuhumiwa kunajisi kitoweo


WAKAZI wa Kata ya Bashnet,  Wilaya ya Babati, mkoani Manyara wamelaani kitendo cha mkazi mmoja wa kata hiyo kuwaingilia mbuzi, na wameitaka Serikali kumchukulia hatua kali za kisheria.

Baadhi ya wakazi wa eneo hilo wakiwamo wafugaji wamesikitishwa na kitendo hicho cha kijana huyo kuwaingilia mbuzi wao.

Mmoja kati ya wakazi hao, Abraham Mlundi alisema juzi ni mara ya tano kwa kijana huyo kumuingilia mbuzi wa mkazi mmoja wa eneo hilo, kitendo ambacho ni kinyume na mila na desturi.

Mlundi alisema imekuwa ni tabia ya muda mrefu kwa kijana huyo kuwaingilia mbuzi hasa nyakati za jioni na kwamba, akishafanya kitendo hicho anahama eneo hilo kwenda kujificha vijiji vya mbali.

“Hadi hivi sasa hatujatambua lengo lake anapowaingilia mbuzi hao, ingawa  wengine wanadai ni vitendo vya ushirikina na wengine wanahisi anafanya hivyo kutokana na kukosa mke hajaoa,” alisema Mlundi.

Alisema hii ni mara ya tano kwa kijana huo kuwaingilia mbuzi na kwamba, wamekuwa wakifanya jitihada kuhakikisha anakamatwa ili afikishwe kwenye vyombo vya sheria.

“Siku ya mwisho kufanya tukio hilo, kijana huyo alitaka kuuawa ila alikimbia kwani alikutwa amembana mbuzi kwenye zizi,” alisema Mlundi.
Hata hivyo, Mtendaji wa Kijiji cha Bashnet, Omary Mwanditi alithibitisha tukio hilo na kwamba, kijana huyo amekuwa na tabia ya kuwaingilia mbuzi.

“Tunaendelea kumtafuta kijana huyo kwani vitendo anavyovifanya siyo vya kiungwana, pia ni kinyume cha ustaarabu kwenye mila na desturi kwa Watanzania,” alisema.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI JAN.31

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.