Maelfu wafeli kidato cha pili

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo 


WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imetangaza matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Pili mwaka 2012, yanayoonyesha kuwa wanafunzi 136,923 kati ya 386,271 waliofanya mtihani huo wamefeli.


Katika matokeo hayo shule kumi zilizofanya vibaya zote ni za Serikali, zikitoka Mikoa ya Kusini. Wanafunzi kumi bora wakitoka katika shule binafsi na taasisi za dini, ambapo Mkoa wa Dar es Salaam ukiongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi waliofeli.


Akitangaza matokeo hayo jijini Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo alisema idadi ya waliofeli ni sawa na asilimia 35.5, wakiwamo wasichana 74,020 na wavulana 62,903, kwamba waliofaulu ni wanafunzi 245.9,32


Hata hivyo, alisema kuwa wanafunzi waliofeli watarudia kidato cha pili na watapewa fursa nyingine ya kurudia mtihani huo na iwapo watafeli tena watarejeshwa nyumbani.


Kwa mujibu wa matokeo hayo, Shule za St Francis ya mkoani Mbeya na Kaizirege ya Bukoba, mkoani Kagera zimetoa wanafunzi kumi bora, kati ya hao mwanafunzi wa tatu na nne pekee wakitoka Sekondari ya Kaizirege na waliobaki ni St Francis.

“Wizara imeamua wanafunzi hawa warudie tena kidato cha pili na watajiunga na wenzao wanaoingia kidato cha pili mwaka huu kuendelea nao kidato cha tatu mwakani, hivyo basi nawaomba wazazi wawape ushirikiano wa kutosha ili wajisijione wapweke hatimaye wakakata tamaa ya kusoma,” alisema Mulugo.


Hata hivyo, alisema kuwa matokeo hayo yanaonyesha kuwa katika mwaka huu, kiwango cha ufaulu kimepanda kutoka asilimia 45.4 ya mwaka 2011 na kufikia asilimia 64.5 mwaka huu ambapo watahiniwa 249,325 wataendelea na masomo ya kidato cha tatu.


“Wanafunzi waliofaulu ni sawa na asilimia 64.55 ambapo kati yao wasichana ni 133,213 na wavulana ni 136,122,” alisema Mulugo na kuongeza:


“Waliopata alama A, B na C walikuwa 127,981 na waliopata kiwango cha chini ya hapo ni 121,344, alama ya juu ya ufaulu ni asilimia 92.”
Alisema wanafunzi wote waliofanya mtihani huo, wasichana ni 187,244 na wavulana ni 199,027.


Kusini hoi
Matokeo hayo yanaonyesha kuwa shule za Serikali zilizofanya vibaya na kushika nafasi 10 za mwisho zinatoka Kanda ya Kusini. Alizitaja shule hizo kuwa ni ya Mihambwe, Diduma, Kiromba, Marambo, Mbembaleo, Kinjumbi, Litupi, Luagala, Miguruwe na Napacho.


Matokeo hayo pia yanaonyesha kuwa shule zisizo za Serikali zilizofanya vibaya mbili zinatoka Kanda ya Kusini, tano kanda ya Mashariki na mbili Kanda ya Kati. Shule hizo ni Mfuru, Pwani, Doreta, Kigurunyembe, Ruruma, At-taaun, Jabal Hira Seminari, Mkono wa Mara, Kilepile na Kiuma. Alisema kutokana na shule nyingi za Kusini kufanya vibaya, Serikali inaangalia uwezekano wa kupeleka walimu zaidi.


Kwa mujibu wa Mulugo, Mkoa wa Dar es Salaam unaongoza kwa kuwa na wanafunzi wengi waliofeli mtihani huo, licha ya kuwa na walimu wa kutosha tofauti na mikoa ya Kusini.

 Kumi bora za Serikali
Shule zilizofanya vizuri za Serikali ni Mzumbe (Morogoro), Tabora, Ilboru (Arusha), Kibaha (Pwani), Iyunga (Mbeya), Msalato (Dodoma), Malangali (Iringa), Ifunda Ufundi (Iringa), Samora Michael (Iringa) na Kilakala (Morogoro).


Kwa Upande wa shule za binafsi zilizofanya vizuri ni Kaizirege (Bukoba), Marian Wavulana (Pwani), St. Francis (Mbeya), Don Bosco (Moshi), Bethel Sabs, Marian Wasichana (Pwani), Don Bosco (Moshi), St Joseph Iterambogo Seminari, Canossa (Dar es Salaam) na Carmel.


Wanafunzi bora
Wanafunzi kumi waliofanya vizuri ni kutoka shule za binafsi na walioshika nafasi mbili za mwanzo ni wasichana kutoka Shule ya St Francis (Mbeya), ambapo wa kwanza ni Magreth Kakoko akifuatiwa na Queen Masiko.


Hata hivyo, baadaye taarifa kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi zilieleza kuwa majina hayo yana kasoro na itatoa taarifa na orodha sahihi baadaye. Kabla ya taarifa hiyo, Mulugo alibainisha kuwa wanafunzi wote kumi bora wanatoka katika shule mbili tu, St Francis na Kaizirege (Bukoba) na kwamba nafasi ya tatu na ya nne imeshikwa na wanafunzi kutoka Kaizirege ambao ni Lukundo Manase na Frank Nyantarila.


Nafasi ya tano hadi ya nane imechukuliwa na wanafunzi kutoka St Francis ambao ni Grace Msovella, Harieth Makirie, Robinnancy Mtitu na Humrath Lusheke.


Nafasi ya tisa na kumi ikachukuliwa na wanafunzi kutoka Kaizirege ambao ni Mukhusin Hamza na Anastazia Kabelinde.

No comments:

Post a Comment