Kesi ya kusafirisha twiga hai kusikilizwa leo


Moshi. Kesi ya uhujumu uchumi ya kusafirisha wanyamapori hai wakiwamo twiga wanne kutoka Tanzania kwenda Jiji la Doha Qatar, itaendelea kusikilizwa leo kwa siku mbili mfululizo.

Twiga hao na wanyama wengine walitoroshwa kwenda Uarabuni Novemba 26, mwaka 2010 kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia) kwa kutumia ndege kubwa ya Jeshi la Qatar.

Washitakiwa katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi ni pamoja na raia wa Pakistan, Kamran Ahmed, Hawa Mang’unyuka, Martin Kimath na Michael Mrutu ambao wote wako nje kwa dhamana.

Wanyama waliotoroshwa kwenda Doha wenye thamani ya Dola 113,715 za Marekani sawa na Sh170.5 milioni za Tanzania, walisafirishwa kwa kutumia maboksi marefu huku wakitumia ndege hiyo. Ushahidi ambao tayari umeshatolewa mahakamani unaeleza kuwa wanyama hao walikamatwa katika maeneo ya Mto wa Mbu, Elboreti na Engaruka wilayani Monduli.

No comments:

Post a Comment