Simu yawa mkombozi wa wajawazito Kilindi


Afya ya Mama na mtoto ni muhimu katika maendeleo ya kila Taifa. Ni vyema afya za kundi hili zizingatiwe kwa kiasi kikubwa ili kuepusha vifo hivyo.

Kilindi. Wengi kati yetu wanaifahamu simu kwa matumizi yao ya mawasiliano ambayo huitumia kuzungumza kirafiki au kutumiana ujumbe.

Kwingineko, simu inatumika kwa majukumu mengine yakiwamo ya tiba na imeonyesha mafanikio na kuwa mkombozi.

Wilayani Kilindi mkoani Tanga, imebainika kuwa teknolojia ya kisasa  inayoitwa Simu ya Teknolojia ya Utoaji wa Huduma ya Afya Ngazi ya Jamii  kwa Kutumia Data (MHEALTH) imefanya maajabu.

Huduma hiyo iliyoanzishwa na Mradi wa Afya Mama na Mtoto Kupitia Shirika la World Vision imewezesha wahudumu wa afya ya jamii kuwasaidia kinamama na watoto wanaozaliwa.

Mhudumu wa afya, Pili Juma anaeleza kuwa walipewa simu hizo mahususi kwa utoaji wa huduma kwa mama na mtoto chini ya umri wa miaka mitano na kwamba  zina uwezo mkubwa wa kutoa mwongozo kwao (wahudumu).

Anasema kuwa badala ya kutumia vitabu, sasa wanao mfumo rahisi wa kutumia simu unaomwezesha mhudumu kutoa huduma kwa mjamzito na kubaini matatizo yake.

Anaongeza kuwa simu hiyo inamwongoza mtumiaji wake kubaini tatizo alilonalo mjamzito na kama anatakiwa apelekwe kwenye kituo cha afya au hospitali ili kuokoa maisha yake, hufanyika hivyo haraka.

“Simu hizi zimerahisisha  utoaji huduma, hatuendi tena kupeleka taarifa kwenye vituo vya afya kwa kutumia mafaili au karatasi, hivyo taarifa za wajamzito na watoto zinapaikana kupitia teknolojia hii,” anasema.

Anaongeza kuwa teknolojia hiyo inawawezesha kuchukua maelezo ya mjamzito moja kwa moja kwenda kwa ofisa mradi huo, vituo vya afya au hospitali ya wilaya.

Simu inavyofanya kazi

Mtaalamu huyo anaeleza kuwa simu hiyo inamwonyesha mtoa huduma anapomtembelea mjamzito nyumbani anapokuwa na mimba chini ya miezi minne kwa mara ya kwanza anatakiwa apewe elimu ya kuhudhuria kliniki, kujua dalili za hatari wakati wa ujauzito na ushiriki wa wenza wao.

Pia, inamwonyesha mtoa huduma  akitoa elimu ya lishe bora wakati wa ujauzito na anaponyonyesha, wakati anapotaka kujifungua na kutoa ushauri wa kupima Ukimwi na kuzuia maambukizo yake kwenda kwa mtoto atakayejifungua.

Huduma nyingine itamwezesha mhudumu kutoa elimu kwa mama mjamzito kupima malaria na kumpima mtoto wake aliye na umri chini ya miaka mitano na kutoa ushauri kwa waume zao wahudhurie kliniki.

Aidha, mtoa huduma anapomtembelea mama huyo kwa mara ya pili atatoa elimu kwa kuyarudia yote aliyomweleza wakati alipomtembelea kwa mara ya kwanza.

Kwa mara ya tatu,  mtoa huduma atatoa elimu kwa mama huyo jinsi ya kumhudumia mtoto atakayezaliwa, dalili za hatari baada ya kujifungua ili akiziona aende kituo cha afya.

Pia, simu hiyo itamwonyesha mtoa elimu kwa mama mwenye Virusi vya Ukimwi (VVU) kuhusu  namna ya kumnyonyesha mtoto wake na kutumia uzazi wa mpango na kuzuia maambukizi katika jamii.

Ofisa Mradi wa Afya wa Afya Mama na Mtoto Wilaya ya Kilindi, Jacqueline Kawiche anaeleza kuwa mradi huo kwa kushirikiana na Shirika  la D-Tree wametoa simu hizo kwa wahudumu wa afya ya jamii ambazo zina programu inayoitwa Com- Care.

Kawiche anasema mhudumu wa afya anapokwenda kumtembelea mjamzito hataenda na makaratasi, hivyo atatumia simu hiyo ambayo ina mwongozo wa Wizara ya Afya wa kutumia Bango Kitita.

“Mwongozo ule wa Wizara ya Afya ambao kwa sasa unatolewa kwenye kaya kupitia makaratasi, sasa unatolewa kwa njia ya simu,” anaeleza.

Faida ya teknolojia hiyo ya simu inamrahisishia  mhudumu wa afya kufanya kazi  na  hivyo anapomhoji mjamzito ambaye ana matatizo hatarishi simu yake hutoa ishara  kuwa mama huyo apelekwe kituo cha afya.

Teknolojia hiyo ya simu inasaidia ukusanyaji wa taarifa kwa wakati, mfano mjamzito anapotembelewa kwenye kaya yake, taarifa hizo zinafika kwa ofisa afya, zinafika kituo cha afya au zahanati husika na baadaye zinatunzwa  kwenye mfumo wa taarifa kwenye hospitali ya wilaya.

Taarifa hizi za mama mjamzito zinakwenda kwa wakati na humsaidia mhudumu wa afya kutoa rufaa ya kumpeleka kituo cha afya kama atagundulika ana dalili hatarishi.

No comments:

Post a Comment