Diwani mbaroni kwa kufunga ofisi za serikali

Mkuu wa Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanya, Benson Mpesya akitoa maelekezo kwa fundi ili kufungua mlango unaodaiwa kufungwa na diwani na watu wengine watatu. Picha: Mohab Dominick.

Watu  watatu  akiwamo  Diwani wa Kata ya Mwendakulima ya Halmashauri ya Wilaya ya  Kahama mkoani Shinyanga,  Ntabo Majhabi wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kufunga ofisi za serikali za mtendaji wa kata hiyo.

Wanadaiwa kutenda kosa hilo wiki iliyopita  asubuhi baada ya mtendaji wa kata hiyo,  Cecilia Clement kupigiwa simu na mlinzi wa ofisi hizo, Joseph Katambi na kumpa taarifa za tukio hilo liliofanywa na wananchi 15 walioambatana na diwani huyo.

Kwa mujibu mtendaji huyo, waliamua kuibadilisha kamati ya sungusungu ya kata hiyo hali ambayo ilianza kuleta malalamiko na minong’ono na kwamba huenda ni chanzo cha watuhumiwa hao kufunga ofisi hizo.

Aliwataja wengine walikamatwa kuwa ni fundi selemala,Hamisi Abbas  na Makaka Benedictor,  wakazi wa kata hiyo.

Kufuatia hali hiyo Mkuu wa Wilaya ya Kahama,  Benson Mpesya akiongozana na kamati ya ulinzi ya kata na askari polisi, walifika katika ofisi hiyo  kushuhudia mlango huo ulivyofungwa kwa kuwekewa kipande cha bati na kupigiliwa misumari  na mawe.

Mpesya  alitoa amri ya kuvunjwa kwa bati hilo chini ya ulinzi wa polisi na kuamuru waliohusika akiwamo diwani huyo kukamatwa na kutiwa mbaroni.

Akizungumzia kitendo hicho Mpesya, alisema ni fedheha na kisichoweza kuvumilika .

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment