Kamati kumi zaitesa CCM

 
Mwenyekiti wa Bunge la Katiba 


Dodoma. Kura za awali katika Kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalumu la Katiba, zinakipa wakati mgumu Chama Cha Mapinduzi,(CCM) kutekeleza azma yake inayotajwa kuwa ni kufumua Rasimu ya Katiba, ili kuondoa mapendekezo ya Muundo wa serikali tatu, baada ya wajumbe wa Zanzibar kukwamisha upatikanaji theluthi mbili.

Kwa mujibu wa taarifa za kamati, ambazo tangu juzi zimeanza kutolewa katika sura ya kwanza na sita zinazungumzia Muundo wa Muungano, wajumbe kutoka Zanzibar kwa sasa ndiyo kikwazo kikubwa kwa CCM.

Hata hivyo, uamuzi ya mwisho kuhusu Muundo wa Serikali, kati ya mbili au tatu, unatarajiwa kujulikana Alhamisi wiki ijayo, wakati kamati zote zitakapowasilisha taarifa zao na kupigwa tena kura kwa wajumbe Tanzania Bara peke yao na Zanzibar peke yao.

Iwapo wajumbe wa Zanzibar wakiitetea kwa theluthi mbili kama sasa, mapendekezo ya muundo wa serikali tatu ndiyo yatakayopelekwa kwa wananchi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, baadhi ya wenyeviti wa kamati hizo, Stephen Wassira, Ummy Mwalimu, Anna Abdalah na Paul Kimili, walitaja moja ya vifungu ambavyo vimeshindwa kupata theluthi mbili kuwa ni ibara ya kwanza kifungu cha kwanza.

Akizungumza jana Wassira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Namba Sita alisema kwamba katika kamati yake ibara hiyo imeshindwa kupata theluthi mbili, ili kuweza kufanyiwa marekebisho.

“Lakini huu siyo mwisho kama nilivyosema awali, tukirudi bungeni tutapiga kura kwa wajumbe wote na ndiyo itakuwa na uamuzi wa mwisho kama muundo wa Muungano utakuwa na Serikali tatu ama mbili, ambao utapelekwa kwa wananchi,” alisema Wassira.

Jussa, Lissu- tumeibana CCM

Jussa alisema: “Kwa taarifa za matokeo tulizonazo katika Kamati Namba 1, 2, 3, 4, 6, 10, 11 na 12 mapendekezo ya kubadilisha Rasimu katika ibara hizo mbili yamekwama. Kama CCM wakichakachua sura ya kwanza na sita, maana yake ni kwamba hapa hakuna Katiba, hakuna kura ya maoni na hakuna mwafaka.”

Vifungu hivi pia kwa mujibu wa wenyeviti wa kamati nyingine, isipokuwa kamati ya Tano, ambayo inaongozwa na Hamad Rashid, havikupata kura theluthi mbili na hivyo kubaki kama vilivyo kwenye rasimu.

Naye Lissu alisema kwa sasa CCM ndiyo inaweza kuanza mkakati wa kuvuruga Bunge kwani tayari wamejua hawana theluthi mbili ya Zanzibar ili kubadili Rasimu kama wanavyotaka.

No comments:

Post a Comment