Mkutano wa Msigwa, bodaboda waingia dosari

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa akiwa amebebwa na madereva bodaboda kabla ya kuanza kwa mkutano wake na waendesha vyombo hivyo vya usafiri uliofanyika mjini humo jana. Picha na Geofrey Nyang’oro 

Na Geofrey Nyang’oro na Berdina Majinge, Mwananchi

Iringa. Jeshi la Polisi limelazimika kutumia nguvu ikiwamo kupiga risasi za moto hewani ili kutuliza vurugu zilizoibuka katika eneo la mkutano ulioitishwa na Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa.

Katika mkutano huo, mbunge huyo alikuwa na lengo la kuzungumza na waendesha pikipiki maarufu bodaboda pamoja na kusikiliza kero zao.

Hata hivyo, wakati Mchungaji Msigwa akiwa ameitisha mkutano huo, Mwenyekiti wa Chama cha Madereva Bodaboda (CMB) Manispaa ya Iringa, Joseph Mwambopa aliitisha mwingine kwa wanachama wake muda huo huo katika Viwanja vya Mwembetogwa.

Hali hiyo ilielezwa kama njia ya kuleta vurugu ingawa waendesha bodaboda wengi walihudhuria mkutano ulioandaliwa na mbunge huku idadi ndogo ikihudhuria kwa Mwambopa aliyekuwa na msimamo tofauti.

 

Kuanza kwa vurugu

Vurugu hizo zilianza muda mfupi baada ya Mwambopa na watu waliokuwa wakimuunga mkono kuwasili katika mkutano wa Mchungaji Msigwa na kushinikiza kuingia kwa nguvu.

Baadhi ya washiriki walipinga hatua ya kiongozi huyo wa waendesha bodaboda kuingia kwa madai kwamba hawamtaki kutokana na kitendo chake cha kuwakataza wanachama wake kutoshiriki mkutano huo.

Hatua hiyo iliibua mzozo na kusukumana jambo lililosababisha polisi kufika eneo hilo na kupiga risasi za moto hewani ili kutuliza ghasia na hatimaye kumkamata Mwambopa na kuondoka naye.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Msigwa aliwataka vijana wakiwamo waendesha bodaboda kuepuka kutumiwa na wanasiasa kama daraja la kufikia malengo yao. “Uongozi ni zaidi ya misaada, kiongozi anapaswa kuwaonyesha watu njia ya kufikia mafanikio,”alisema Msigwa.

Pia aliwashauri waendesha bodaboda kuanzisha chama kingine kama wanaona kuna sababu ya kufanya hivyo.

No comments:

Post a Comment