Askari wawili mbaroni kwa fedha bandia

 
 Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Simiyu, Charles Mkumbo akionyesha sare za jeshi la wananchi zilizokamatwa kutoka kwa askari polisi baada ya kupekuliwa nyumbani kwake. 
Picha na Faustine Fabian 

Jeshi la Polisi mkoani Simiyu linawashikilia askari wawili wa magereza na polisi kwa kukutwa na noti bandia ikiwa pamoja na sare za Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Charles Mkumbo alisema askari hao walikamatwa juzi saa tisa mchana katika Mtaa wa Old Maswa, Kata ya Nyakabindi, wilayani Bariadi.

Alisema askari hao walifika kwenye kibanda cha Mpesa kinachomilikiwa na Mwalimu wa Shule ya Sekondari Old Maswa, Kassian Luhende (29) wakiwa na pikipiki aina ya Sunlg kwa lengo la kuweka fedha hizo katika simu.

Alisema baada ya mwalimu huyo kupokea noti 10 zenye thamani ya Sh100,000 alizitilia shaka na kuamua kuzikagua zaidi ndipo alipogundua kuwa siyo fedha halali.

Mkumbo alisema mwalimu huyo baada ya kugundua hilo aliomba msaada wa kukamatwa kwa askari hao. Alisema majirani walipofika walihoji, ndipo mmoja wao alipotoa kitambulisho kuwa yeye ni askari na mwingine kujitambulisha kuwa ni dereva bodaboda.

Alibainisha kuwa baada ya wananchi kuambiwa hivyo waliwatilia shaka zaidi na kutoa taarifa katika Kituo cha Polisi Bariadi na kisha kukamatwa.

Mkumbo aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni askari mwenye namba H 2420 PC Seleman Juma (25) ambaye ni wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) mkoani Simiyu, na mwenye namba B.6499 WDR Edmund Masaga (28) wa Magereza wilayani Bariadi.

Kamanda Mkumbo alieleza kuwa, baada ya askari hao kukamatwa mmoja wao PC Selemani alipopekuliwa katika mfuko wa suruali yake, alikutwa na noti nyingine za bandia za Sh100,000.

Mbali na hilo Mkumbo alisema askari huyo alipopekuliwa nyumbani kwake alikutwa na sare za JWTZ ambazo ni kaptula nne, fulana mbili, kombati moja pamoja na kitambaa.

Alisema uchunguzi zaidi unaendelea ili kubaini mtandao mzima wa usambazaji wa noti bandia ndani ya mkoa na kwamba baada ya uchunguzi kukamilika askari hao watachuliwa hatua za kinidhamu pamoja na kisheria.

No comments:

Post a Comment