Hesabu za uandikishaji BVR zinagoma

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na waandishi wa habari katika viwanja vya Bunge, mjini Dodoma jana. 
Picha na Anthony Siame. 


Dar/Dodoma. Licha ya Serikali kusisitiza kuwa uandikishaji wa wapigakura nchi nzima kwa mfumo wa BVR utakamilika Aprili 28 na Kura ya Maoni kufanyika Aprili 30, mwaka huu kama ilivyopangwa, hesabu zilizopigwa na Mwananchi zinakataa kuwianisha siku zilizosalia na idadi ya mashine za BVR zilizopo na zinazotarajiwa kuwasili. Hali hiyo imejitokeza zikiwa zimebaki siku 36 kabla ya Kura ya Maoni kufanyika, huku kukiwapo wasiwasi miongoni mwa wadau kuhusu uwezekano wa kufanikisha matukio hayo bila manung’uniko.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa uandikishaji nchi nzima utaanza siku sita kuanzia leo na kusisitiza kuwa Kura ya Maoni kuridhia au kukaa Katiba Inayopendekezwa itafanyika Aprili 30, mwaka huu kama ilivyopangwa.

Wasiwasi wa kutofanyika kwa kura hiyo katika tarehe iliyopangwa unatokana na uandikishaji wa wapigakura kwa BVR unaosimamiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ulioanza Februari 23, mwaka huu kutokamilika hata katika mkoa mmoja wa Njombe, wenye wapigakura 392,634 kati ya milioni 24 wanaotarajiwa kuandikishwa nchini kote.

Hesabu zinavyokataa

Kulingana na takwimu za NEC, BVR moja inaandikisha kati ya wapigakura 80 hadi 100 kwa siku endapo hakuna tatizo lolote, hivyo kwa kadirio la chini, iwapo BVR 7,750 zilizoagizwa na NEC zitawasili nchini kwa mafungu, zitahitajika siku 38 kuandikisha wapigakura milioni 24 wanaokusudiwa kama kazi hiyo itaanza leo.

Hata hivyo, katika uandikishaji wa majaribio na baadaye katika Mkoa wa Njombe mashine hizo zimeripotiwa kukabiliwa na changamoto mbalimbali ama za kukwama, weledi mdogo wa watumiaji na hali ya hewa, hivyo kufanya idadi iliyokusudiwa kutokamilika.

Mwandishi wa Mwananchi, Kizzito Noya aliyekuwa Makambako, Njombe wakati wa uandikishaji hivi karibuni amesema kwa wastani alishuhudia mashine moja ya BVR ikiandikisha wapigakura 60 kwa siku, idadi hiyo ikilinganishwa na watu 24,000,000 wanaokusudiwa kuandikishwa kwa BVR 7,750 nchi nzima, shughuli hiyo itachukua siku 52, wakati siku zilizosalia hadi Kura ya Maoni ni 36.

Jambo jingine linalofanya hesabu hizo kukataa ni kitendo cha mashine hizo 7,750 za BVR zilizokusudiwa, kutokuwapo zote nchini hadi sasa, licha ya NEC kusema mara kwa mara kwamba zitawasili wakati wowote.

Jana, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva alisema hata awamu ya kwanza ya mashine 3,100 za BVR bado ziko njiani.

Iwapo mashine hizo pekee zitafika na kutumika kuandikisha wapigakura hao milioni 24 zitahitajika siku 97 kukamilisha shughuli hiyo.

Mchakato huo ulianza kusuasua tangu wakati majaribio yaliyotumia BVR 250 katika majimbo ya Kilombero, Morogoro; Kawe, Dar es Salaam na Milele mkoani Katavi na baadaye katika Mji wa Makambako na mkoa mzima wa Njombe.

Hata hivyo, uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa mashine hizo 250 zimekuwa hazitumiki zote kwa kuwa baadhi zinatumika kutoa mafunzo kwa waandikishaji watakaofanya kazi hiyo nchi nzima.

Changamoto nyingine inayokwamisha shughuli hiyo ni ukata, kwa kuwa Serikali haijatoa fedha za kutosha kufanikisha shughuli hiyo, jambo ambalo limethibitishwa na Pinda kuwa fedha zilizotolewa hadi sasa ni asilimia 70 ya kiwango kilichotarajiwa.

Kauli ya Lubuva

Jaji Lubuva alisema: “Tuliamua kuanza na Njombe kutokana na BVR 250 tulizonazo kutosha katika mkoa huo wenye kata 99. Tunasubiri nyingine 7,750 kuwasili wiki ya kwanza hadi ya pili ya mwezi ujao zikitokea China.”

Alisema uandikishaji Njombe unaendelea vizuri na unatarajiwa kukamilika Aprili 12, kama ilivyopangwa.

Kuhusu uwezekano wa kura ya maoni kufanyika Aprili 30, alisema: “Kazi ya msingi kabla ya shughuli yoyote ni kuandikisha daftari la wapigakura, hivyo kama tarehe itafika bado hatujamaliza nitawaeleza, lakini mpaka sasa bado tarehe ya Aprili 30 haijabadilishwa.

“Vifaa 3,100 kati ya 7,750 viko njiani na vitakapowasili tutatangaza ratiba, tutaanza na mikoa gani na Njombe kweli wamehamasika kwani wamejitokeza kwa wingi na sisi kama tunaona hatujamaliza licha ya ratiba kututaka kuhama tunaongeza siku ili kuhakikisha kila mmoja anaandikishwa sasa mimi sielewi hao wanaosema kwamba uandikishaji unakwenda sivyo hata huko bungeni sielewi wana maanisha nini.”

 Oktoba 22 mwaka jana, Rais Jakaya Kikwete alipokutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wa Afrika wanaoziwakilisha nchi zao katika Jamhuri ya Watu wa China, aliwaeleza kwamba kura hiyo itafanyika Aprili mwaka huu.

Matumaini ya Pinda

Akizungumza na waandishi wa habari katika viwanja vya Bunge jana, Pinda alisema uandikishaji utaanza siku sita kuanzia leo na Kura ya Maoni kuridhia au kukaa Katiba Inayopendekezwa itafanyika Aprili 30, mwaka huu.

Alisema utoaji wa elimu kwa umma sambamba na kampeni za kuiridhia au kuikataa Katiba hiyo, vinaweza kufanyika wakati uandikishaji ukiendelea. Waziri Mkuu alisema Serikali imeshalipa asilimia 70 ya fedha kwa kampuni inayosambaza mashine hizo.

“Tukianza uandikishaji nchi nzima ndiyo tutaona changamoto zaidi zipo wapi na zinaweza kutupeleka katika uamuzi wa aina gani. Ila hilo litakuwa jukumu la Tume (NEC), sisi kazi yetu ni kuhangaika ili BVR zinazotakiwa ziwe zimepatikana kwa wakati,” alisema Pinda.

Akizungumzia muda wa kampeni wa siku 30 kabla ya Kura ya Maoni Pinda alisema: “Tume ndiyo inaweza kulizungumzia suala hilo kiundani. Unajua inatakiwa mpaka kufikia Aprili 28 mambo yote yawe yamekamilika na siku mbili baadaye (Aprili 30) ndiyo siku ya kura. Kama wanasema mwezi mmoja ni sawa, tunaweza kuendelea na mambo mengine huku elimu ikitolewa kwa wananchi.”

Alipoulizwa juu ya changamoto zilizojitokeza mkoani Njombe alisema Serikali iliamua kuanza uandikishaji mkoani humo ili kupata uzoefu kutokana na hali ya jiografia ya mkoa huo.

“Tulichojifunza ni kwamba katika maeneo ya mijini,  tukianza uandikishaji nchi nzima ni lazima maeneo kama hayo tuyape nafasi kubwa zaidi tofauti na vijijini,” alisema.

Alisema maeneo ya mijini lazima mashine za BVR ziwe nyingi zaidi kuliko maeneo ya vijijini kwa sababu ya idadi ya watu.

Alisema katika Mkoa wa Njombe zilipelekwa mashine za BVR 250 lakini hazikutumika zote.

“Tumetenga siku saba kwa kila kata kwa ajili ya uandikishaji nadhani zinatosha na kila kata tutaweka mashine za BVR mbili hadi tatu,” alisema Waziri Mkuu.

Aliongeza: “Mashine hizo zinatosha kabisa. Kwa uzoefu tulioupata pale Njombe hatuoni tatizo hata kidogo kwamba tunaweza kushindwa kuandikisha wananchi na kutofikia malengo tuliyoweka. Zinatosha kwa sababu leo wanaweza kuandikishia kituo kimoja na watu wakiisha wanahamia kituo kingine. Kata ina vijiji vinne hadi vitano na kila kijiji kina kitongoji kati ya vinne hadi vitano, hivyo muda wa siku saba unatosha kabisa.”

Juzi, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika aliomba mwongozo bungeni akiitaka Serikali itoe majibu ya kueleweka juu ya hatima ya uandikishaji wa wananchi katika daftari la Wapigakura ulioanzia Mkoa wa Njombe na iwapo Kura ya Maoni itafanyika Aprili 30.

Alisema kuwa muda uliobaki ni ndoto kwa Serikali kukamilisha uandikishaji huo nchini nzima, akitoa mfano kwamba ili wananchi wa Mkoa wa Njombe waweze kuandikishwa wote, uandikishaji unatakiwa kuongezwa muda hadi Aprili 28 na Spika alimjibu kuwa Serikali ingetoa maelezo.

No comments:

Post a Comment