Kamati ya Bunge yaivaa Tirdo kwa udanganyifu


KAMATI ya Hesabu za Mashirika ya Umma (Poac), imempa onyo kali Kaimu Mkurugenzi wa wa Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (Tirdo) Ludovick Manege,baada ya kubainika kuwa alikuwa akitoa maelezo ya uongo ya kushindwa kuwaruhusu wakaguzi kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG) kufanya ukaguzi wa gharama za vifaa vya ofisini vilivyonunuliwa Ujerumani na shirika hilo vyenye thamani ya Sh155milioni.

Mbali na onyo hilo, kamati hiyo pia imemtaka CAG kufanya ukaguzi maalumu ili kubaini kiasi cha fedha kinachotumika kwa ajili ya uendeleshaji wa shughuli mbalimbali yakiwamo malipo hewa ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Shirika hilo, Asifael Nanyaro.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kaimu Mwenyekiti wa kamati, Mohamed Chombo alisema kuwa, watendaji wa Tirdo walishindwa kutoa ushirikiano kwa wakaguzi kutoka Ofisi ya CAG wakati walipokwenda kukagua vifaa hivyo, jambo ambalo liliwafanya wakae zaidi ya saa matano.

“Tunakupa onyo kali ili iwe fundisho siku nyingine unapokuja kuzungumza na kamati kuacha kusema uongo, hii inaonyesha wazi kuwa, hata utendaji wao ni wa ubabaishaji, jambo ambalo limesababisha kutudanganya,” alisema Chombo.

Alisema,Nanyaro, aliidhinishiwa kulipwa fedha hizo za pango la nyumba bila ya kufuata taratibu za kisheria wakati alikuwa akiishi kwenye nyumba za Serikali.

“Kitendo cha Mkurugenzi wa zamani kulipwa Sh22milioni kama pango la nyumba wakati alikuwa akiishi kwenye nyumba za Serikali ni ubadhirifu, jambo ambalo kamati yetu imebaini kwa kushirikiana na ripoti ya CAG,”aliongeza. Manege alikiri kuwapo kwa tatizo hilo na kudai kuwa, mkurugenzi huyo mstaafu alipewa fedha hizo kimakosa,lakini walijaribu kumshawishi ili arudishe alikataa.

“Tulimshawishi kurudisha fedha hizi lakini alikataa, badala yake alitujibu kuwa, yeye ni mteule wa Rais na kwamba ametoka jeshini hivyo alistahili malipo hayo,” alisema Manege.

Aliongeza Menejimenti iliwasilisha suala hilo Wizara ya Viwanda na Biashara ili waweze kuangalia njia mbadala ya kurudisha fedha hizo Hazina. Alisema kutokana na hali hiyo wakaandaa utaratibu wa kumkata fedha kwenye mafao yake ili waweze kurudisha fedha hizo ambazo zililipwa kinyume na sheria.

Kwa mujibu wa Chombo, kamati hiyo itamwita Waziri wa Viwanda na Biashara, Abdalah Kigoda ili waweze kujadiliana jinsi ya uteuzi wa mkurugenzi mpya kwenye shirika hilo hivi karibuni, jambo ambalo wanaamini linaweza kuboresha utendaji.

No comments:

Post a Comment