Mgaya anusurika kung'olewa Tucta

Nicolaus Mgaya 


Dar es Salaam: Siku chache baada ya Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), Ayoub Omar kuvuliwa wadhifa wake, imebainika kuwa Katibu Mkuu wa shirikisho hilo, Nicolaus Mgaya naye amenusurika kung’olewa kwenye wadhifa wake.


Mgaya aliliambia Mwananchi jana kuwa njama za kumng’oa kwenye wadhifa huo zilipangwa na wapinzani wake ambao walitoa hoja dhaifu bila ushahidi kuwa ana uhusiano wa wanawake (hawakutajwa).


“Hoja zao hazikuwa na maana, walikuwa wakihisi tu kuwa natembea na mwanamke fulani bila kuwa na ushahidi, pia suala hilo halihusiani na utendaji wangu wa kazi,” alisema Mgaya na kuongeza:


“Unajua katika umoja wowote lazima kuwe na majungu watu wanaweza kuwa na sababu zao nyingi tu, hivyo sikuona ajabu niliposikia nafanyiwa zengwe.”
Alisema hoja za kutakiwa kung’oka zilijadiliwa na kumalizwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji kilichomalizika juzi, ndiyo maana hazikuibuka tena katika kikao cha Baraza Kuu la Tucta kilichomalizika jana jioni.


“Ripoti ya kikao cha utendaji ndiyo huletwa katika kikao cha baraza kuu na kwa kuwa suala hilo halikuwa na ushahidi lilikwisha hukohuko,” alisema Mgaya.
Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya kikao cha Baraza Kuu la Tucta kilichomalizika jana jioni zilisema kuwa baadhi ya wajumbe waliibua hoja kwamba Mgaya ameshatimiza miaka 61, hivyo anatakiwa kustaafu kwa mujibu wa sheria.


“Baadhi ya wajumbe waliibua hoja hiyo lakini haikuwa na nguvu, ila pamoja na hayo jambo hili lazima litakuja kumbana Mgaya baadaye,” zilieleza taarifa hizo.
Ayoub alivuliwa wadhifa wake juzi kwa mujibu wa Katiba ya Tucta kifungu cha 16.6.8 kinachoeleza kuwa kiongozi wa shirikisho hilo atakoma
kuendelea kushikilia ofisi ikiwa atastaafu kwa mujibu wa sheria.


Mgaya alisema pamoja na Ayoub kuwa na kazi mpya baada ya kustaafu lakini alipoteza sifa ya kuendelea kuwa Mwenyekiti kwa kuwa katiba inaeleza kwamba kiongozi lazima awe mwajiriwa katika sekta ya umma au ile binafsi.


Mgaya alisema kwa sasa nafasi ya Omari inakaimiwa na Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Notibuga Masikini na kwamba ataendelea na wadhifa huo kwa miezi 12.
“Mwakani tutakuwa na mkutano mkuu wa kazi ambapo pamoja na mambo mengine tutapata nafasi ya kuchagua mwenyekiti mpya, Katiba ipo wazi kama siyo mwajiriwa huwezi kuendelea na wadhifa wowote,” alisema Mgaya.


Katika maelezo yake, Ayoub alisema kuwa viongozi wenzake walikuja na hoja kwamba hakuwa na kazi kwani alikuwa amestaafu katika kiwanda cha Mbolea Mbeya, lakini alisisitiza kuwa baada ya kustaafu alipata kazi sehemu nyingine.


Wakati hayo yakitokea, habari nyingine zinasema wajumbe wa Baraza Kuu la Tucta kutoka mikoa ya Mbeya, Arusha na Dodoma walihoji mapato na matumizi ya Tucta, huku wakitaka kujua kiasi cha fedha kilichopatikana kutokana na kodi ya majengo ya shirikisho hilo.

Maombi ya Lwakatare yapangiwa jaji

 
Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare akifunguliwa pingu alipofikishwa katika chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini  Dar es Salaam hivi karibuni.

Dar es Salaam. Maombi ya Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare kupinga utaratibu wa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kumfutia mashtaka kisha kumkamata na kumfungulia tena mengine, tayari yamepangiwa jaji wa kuyasikiliza.

Habari zilizopatikana jana na kuthibitishwa na mmoja wa mawakili wanaomtetea Lwakatare, zinadai maombi hayo yamepangwa kusikilizwa na Jaji Lawrence Kaduri. Hata hivyo, tarehe ya kusikilizwa kwa maombi hayo haijapangwa.


Lwakatare anayekabiliwa na kesi ya ugaidi na mwenzake Ludovick Joseph, kupitia kwa jopo la mawakili wanaomtetea, wiki iliyopita aliwasilisha maombi Mahakama Kuu Dar es Salaam akipinga uamuzi wa DPP kuwafutia mashtaka kisha kuwakamata na kuwafungulia tena mashtaka hayo.


Siku hiyohihyo alipowasilisha maombi hayo, Mahakama Kuu ilitoa hati ya kuita majalada yanayohusiana na kesi yao, ikiiamuru Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iwasilishe majalada hayo mahakamani hapo.


Majalada hayo namba 37 na namba 6 yote ya mwaka 2013, yalishawasilishwa Mahakama Kuu, kwa awamu mbili. Jalada la kwanza, namba 37 liliwasilishwa Mahakama Kuu Jumatatu na jalada la pili namba 6 liliwasilishwa Jumanne, wiki hii.


Katika maombi yake Mahakama Kuu yaliyowasilishwa chini ya hati ya dharura, yakiambatanishwa na hati ya kiapo cha Wakili Peter Kibatala, Lwakatare anaomba mahakama hiyo iitishe majalada hayo na ifanye marejeo ya mwenendo wa kesi katika Mahakama ya Kisutu.


Kwa mujibu wa maombi hayo ya marejeo namba 14 ya mwaka 2013, lengo la kuiomba mahakama hiyo iitishe majalada hayo ni kufanya uchunguzi ili kujiridhisha yenyewe kuhusu usahihi na uhalali wa mwenendo wake.
Pia, wanaomba Mahakama Kuu ifanye marejeo na/au kutengua hati ya Mkurugenzi wa Mashtaka kuwafutia mashtaka watoa maombi (Nolle Prosequi), kabla ya kuwakamata na kuwafungulia tena mashtaka hayohayo.


Sambamba na hayo, wanaomba Mahakama Kuu iamuru Mahakama ya Kisutu itoe uamuzi wa maombi ya dhamana, uliokuwa umepanga kutolewa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Emillius Mchauru, Machi 20, mwaka huu katika kesi namba 37.


Maombi mengine ni kurejea, au kutengua mwenendo wa kesi katika kesi namba 6 iliyofunguliwa baada ya hati ya kuwafutia mashtaka watoa maombi hao, badala yake mwenendo wa kesi katika kesi namba 37 uendelee.


Pia, wanaomba Mahakama Kuu iamue kwamba utaratibu uliotumiwa na wajibu maombi (Jamhuri) kutoa hati ya kuwafutia mashtaka watoa maombi katika kesi namba 37, ilikuwa kinyume cha sheria na/au haukuwa sahihi.


Lwakatare na mwenzake, Joseph, wanakabiliwa na kesi ya ugaidi katika Mahakama ya Kisutu, wakikabiliwa na mashtaka manne ya kula njama na kufanya mipango ya kumteka, kisha kumdhuru kwa sumu Dennis Msacky.


Walikamatwa Machi 13, mwaka huu na kupandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza Jumatatu, Oktoba 18, ambako walisomewa mashtaka hayo, ambayo waliyakana, baada ya kuulizwa kama wanayakubali au la.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI MACH 29

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
DSC03384

Wasichana wadogo waongoza kuambukizwa VVU nchini

Rais Jakaya Kikwete 

Ripoti ya viashiria vya Ukimwi nchini katika mwaka 2011/12 imeonyesha kuwa wasichana wenye umri wa kati ya miaka 23 na 24 wameambukizwa virusi vya Ukimwi kwa asilimia 6.6, ikilinganishwa na wavulana wa umri huo ambao ni asilimia 2.8.


Akisoma ripoti hiyo jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania, (Tacaids), Dk Fatuma Mrisho alisema kiwango cha wasichana wa umri huo wenye virusi ni mara mbili zaidi ya wavulana.


Akizindua ripoti hiyo, Rais Jakaya Kikwete alisisitiza Watanzania na sekta zote zinazojihusisha na mapambano dhidi ya Ukimwi, zitilie mkazo umuhimu wa kukomesha unyanyapaa na kuhamasisha upimaji wa hiari.


“Watanzania zaidi ya milioni mbili wamefariki tangu Ukimwi ugundulike miaka 30 iliyopita, tunatakiwa tupambane kwa dhati kabisa,” alisema Rais Kikwete.
Alipongeza ongezeko la idadi ya watu waliopima kwa hiari na kuwataka wanaume kupima badala ya kuwaachia jukumu hilo wanawake.


Rais pia alizitaka taasisi za Ukimwi, kudhibiti kasi ya maambukizi katika miji mikubwa na katika barabara kuu zikiwemo za Chalinze na Njombe.
“Maeneo hayo yanahitaji nguvu zaidi, hata maeneo yenye kiwango kidogo cha maambukizi nayo yasibweteke yanahitaji tahadhari,” alisema.


Kuhusu tohara kwa wanaume, Rais Kikwete alisisitiza zaidi tohara kwa wanaume na kwamba wasiotahiriwa wanaongeza kasi ya maambukizi kwa asilimia 60 na wanaotahiriwa wanapunguza kwa asilimia 60 pia.


Kwa upande wake, Dk Kikwete alisema maambukizi kwa vijana wenye umri mdogo yanatokea wakati vijana hao wana umri wa kati ya miaka 15 na 19 na matokeo yake kuwa wazi katika umri wa miaka 23 na 24. Alisisitiza kuwa matokeo haya ni kama ya sensa na kwamba si kila Mtanzania mwenye umri wa miaka 14 hadi 49 amepimwa.


“Kwa jumla asilimia 2.0 ya wasichana na wavulana wenye umri wa miaka 15 hadi 24 wana maambukizi ya virusu,” alisema. Hata hivyo ripoti hiyo ilionyesha kuwa kasi ya maambukizi kwa Tanzania nzima, imepungua kutoka asilimia 5.8 mwaka 2008 hadi kufikia asilimia 5.1 mwaka 2011/2012.


Utafiti wa kwanza wa aina hii ulifanywa mwaka 2003 -2004 ambapo maambukizi yalikuwa asilimia 7.06.
Utafiti mwingine ulifanyika mwaka 2009-2010 ambapo maambukizi yalishuka toka asilimia 7 hadi asilimia 5.8


Pia, ripoti hiyo ilionyesha kuwa asilimia tisa ya wasichana na 10 ya wavulana wenye umri wa miaka 15 na 24 walianza kujamiiana kwa mara ya kwanza kabla ya kutimiza miaka 15.
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa Mkoa wa Njombe una maambukizi ya juu zaidi ya asilimia 14.8 ya maambukizo kuliko mikoa yote Tanzania.


Maeneo ya visiwani yana asilimia ndogo zaidi ya maambukizi ambapo Unguja ilikuwa na asilimia 1.2 na Pemba asilimia 0.5 tu
“Matokeo ya ripoti hii yatatupa mwanya zaidi wa kujua nini kifanyike na wapi nguvu iongezwe katika kupambana na maradhi haya hatari,” alisema Kikwete.


Takwimu za sasa zinaonyesha kuwa maeneo ya mijini yana maambukizi mengi zaidi ambapo kwa wanawake ni asilimia 6.2 na wanaume ni asilimia 3.8
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa zaidi ya robo ya Watanzania walioko kwenye ndoa wana maambukizi ya Ukimwi.

 Ripoti hiyo ya kwanza na ya aina yake ilichambua pia idadi ya wenza kati ya wanaume na wanawake ambapo kwa Tanzania nzima, asilimia 21 ya wanaume walikuwa na mwenza zaidi ya mmoja wakati ni asilimia nne tu ya wanawake walikuwa na mwenza zaidi ya mmoja.
“Uwiano wa wanaume wenye miaka 15 hadi 49 ambao walikuwa wamejamiiana na wenza wawili au zaidi miezi miwili iliyopita ni zaidi ya mara tano ya uwiano wa wanawake,” ilisema ripoti hiyo.


Uzinduzi wa ripoti hiyo ulihudhuriwa pia na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri Wa Fedha Dk William Mgimwa, waziri wa afya, Dk Hussein Mwinyi, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Sedicy Mecky na wadau mbalimbali wa Ukimwi nchini na nje ya nchi.

Hatima ya vigogo waliosimamishwa Tanesco kitendawili



Dar es Salaam. Bodi ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) imeendelea kusuasua kutoa majibu sahihi kuhusu hatima ya vigogo watatu, waliosimamishwa kazi mwaka jana kwa tuhuma za ubadhirifu na matumizi mabaya ya ofisi.
Tayari bodi hiyo imeunda jopo la watu sita kuwahoji maofisa hao kabla ya kutoa uamuzi, lakini zaidi ya mara tatu Mwenyekiti wake, Jenerali mstaafu Robert Mboma anapotafutwa kuelezea kilichobainika baada ya kuhojiwa kwa vigogo hao, amekuwa akieleza kuwa kazi hiyo itaanza baada ya wiki moja.

Uamuzi wa kuwahoji maofisa hao ulikuja baada ya bodi hiyo kukabidhiwa ripoti na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuonyesha upungufu kadhaa wa utendaji kwa watumishi hao.

Katika maelezo yake ya jana, Mboma alisema: “Tumeshapata jopo la watu sita ambao watakuwa katika makundi mawili yenye watu watatu, tumechelewa kuanza kuwahoji kwa sababu tulikuwa tukichambua mafaili ya watu wanaounda jopo hili.”
“Pia, tulikuwa tukipitia ushauri wa watu mbalimbali, ili kutokuwa na watu ambao wana mgongano wa kimasilahi na maofisa hawa wa Tanesco.”

Tangu Januari mwaka huu, Jenerali Mboma ameshazungumza na gazeti hili zaidi ya mara tatu, kila alipokuwa akiulizwa juu ya suala hilo, alisema kazi ya kuwahoji maofisa hao ingeanza baada ya wiki moja.

Maofisa hao ambao wanasubiri kuhojiwa ni Naibu Mkurugenzi Mtendaji Huduma za Shirika, Robert Shemhilu, Ofisa Mkuu wa Fedha, Lusekelo Kassanga na Meneja Mwandamizi Ununuzi, Harun Mattambo.

Katika maelezo yake, Jenerali Mboma alisema ripoti ya CAG inaonyesha kuna kasoro hasa ununuzi usiofuata taratibu na ubadilishaji fedha za kigeni (dola).

“Kikubwa alichogundua CAG ni ununuzi usiofuata taratibu na suala la kubadilishwa kwa Dola za Marekani benki, ambazo Shirika halina akaunti,” alisema Mboma na kuongeza:

“Benki ambayo shirika halina akaunti na ambayo wangeweza kubadilishia fedha hizo ni Benki Kuu (BoT) pekee, lakini haikufanyika hivyo jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu.”
Alisema baada ya jopo kumaliza kuwahoji watuhumiwa hao, litawasilisha mapendekezo kwa bodi ambayo itatoa uamuzi wake.

Maofisa hao walisimamishwa kazi Julai 14, mwaka jana, sambamba na aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, William Mhando ambaye baadaye alifukuzwa kazi.

Kima cha chini kutangazwa mwezi ujao

Dar es Salaam. Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka amesema mwezi ujao wanatarajia kutangaza kima cha chini cha mshahara kwa wafanyakazi wa sekta zote.

Akizungumza jana wakati wa mkutano kuhusu sekta ya Hifadhi ya Jamii kwa Baraza Kuu la Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), alisema kwa muda mrefu kiwango cha kima cha chini cha mshahara kwa wafanyakazi wa sekta zote kilikuwa hakijabadilishwa.

“Kwa muda mrefu tulikuwa hatujatangaza kima cha chini cha mshahara, lakini nafurahi kuwajulisha tu kwamba mwezi ujao tutatangaza rasmi,”alisema Kabaka.

Pia alitahadharisha kuhusu utitiri wa vyama katika sehemu moja ya kazi kushauri waajiri wasiruhusu wafanyakazi waanzishe kwa sababu vitakosa nguvu ya kujadiliana na mwajiri katika kufunga mikataba ya hiyari .

Waziri huyo alisema sekta ya hifadhi ya jamii ina idadi ndogo ya wanachama waliojiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii ukilinganisha na idadi ya nguvu kazi iliyopo ambayo ni milioni 22.

Awali Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii, Irene Isaka alisema hadi sasa michango katika mifuko hiyo imefikia Sh 1.4 trilioni na kwamba mafao yanayolipwa yamepanda kutoka Sh500 bilioni hadi kufikia Sh 724 bilioni.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI MACH 28

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.