Mgaya anusurika kung'olewa Tucta

Nicolaus Mgaya 


Dar es Salaam: Siku chache baada ya Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), Ayoub Omar kuvuliwa wadhifa wake, imebainika kuwa Katibu Mkuu wa shirikisho hilo, Nicolaus Mgaya naye amenusurika kung’olewa kwenye wadhifa wake.


Mgaya aliliambia Mwananchi jana kuwa njama za kumng’oa kwenye wadhifa huo zilipangwa na wapinzani wake ambao walitoa hoja dhaifu bila ushahidi kuwa ana uhusiano wa wanawake (hawakutajwa).


“Hoja zao hazikuwa na maana, walikuwa wakihisi tu kuwa natembea na mwanamke fulani bila kuwa na ushahidi, pia suala hilo halihusiani na utendaji wangu wa kazi,” alisema Mgaya na kuongeza:


“Unajua katika umoja wowote lazima kuwe na majungu watu wanaweza kuwa na sababu zao nyingi tu, hivyo sikuona ajabu niliposikia nafanyiwa zengwe.”
Alisema hoja za kutakiwa kung’oka zilijadiliwa na kumalizwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji kilichomalizika juzi, ndiyo maana hazikuibuka tena katika kikao cha Baraza Kuu la Tucta kilichomalizika jana jioni.


“Ripoti ya kikao cha utendaji ndiyo huletwa katika kikao cha baraza kuu na kwa kuwa suala hilo halikuwa na ushahidi lilikwisha hukohuko,” alisema Mgaya.
Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya kikao cha Baraza Kuu la Tucta kilichomalizika jana jioni zilisema kuwa baadhi ya wajumbe waliibua hoja kwamba Mgaya ameshatimiza miaka 61, hivyo anatakiwa kustaafu kwa mujibu wa sheria.


“Baadhi ya wajumbe waliibua hoja hiyo lakini haikuwa na nguvu, ila pamoja na hayo jambo hili lazima litakuja kumbana Mgaya baadaye,” zilieleza taarifa hizo.
Ayoub alivuliwa wadhifa wake juzi kwa mujibu wa Katiba ya Tucta kifungu cha 16.6.8 kinachoeleza kuwa kiongozi wa shirikisho hilo atakoma
kuendelea kushikilia ofisi ikiwa atastaafu kwa mujibu wa sheria.


Mgaya alisema pamoja na Ayoub kuwa na kazi mpya baada ya kustaafu lakini alipoteza sifa ya kuendelea kuwa Mwenyekiti kwa kuwa katiba inaeleza kwamba kiongozi lazima awe mwajiriwa katika sekta ya umma au ile binafsi.


Mgaya alisema kwa sasa nafasi ya Omari inakaimiwa na Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Notibuga Masikini na kwamba ataendelea na wadhifa huo kwa miezi 12.
“Mwakani tutakuwa na mkutano mkuu wa kazi ambapo pamoja na mambo mengine tutapata nafasi ya kuchagua mwenyekiti mpya, Katiba ipo wazi kama siyo mwajiriwa huwezi kuendelea na wadhifa wowote,” alisema Mgaya.


Katika maelezo yake, Ayoub alisema kuwa viongozi wenzake walikuja na hoja kwamba hakuwa na kazi kwani alikuwa amestaafu katika kiwanda cha Mbolea Mbeya, lakini alisisitiza kuwa baada ya kustaafu alipata kazi sehemu nyingine.


Wakati hayo yakitokea, habari nyingine zinasema wajumbe wa Baraza Kuu la Tucta kutoka mikoa ya Mbeya, Arusha na Dodoma walihoji mapato na matumizi ya Tucta, huku wakitaka kujua kiasi cha fedha kilichopatikana kutokana na kodi ya majengo ya shirikisho hilo.

No comments:

Post a Comment