Kesi ya kusafirisha twiga hai kusikilizwa leo


Moshi. Kesi ya uhujumu uchumi ya kusafirisha wanyamapori hai wakiwamo twiga wanne kutoka Tanzania kwenda Jiji la Doha Qatar, itaendelea kusikilizwa leo kwa siku mbili mfululizo.

Twiga hao na wanyama wengine walitoroshwa kwenda Uarabuni Novemba 26, mwaka 2010 kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia) kwa kutumia ndege kubwa ya Jeshi la Qatar.

Washitakiwa katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi ni pamoja na raia wa Pakistan, Kamran Ahmed, Hawa Mang’unyuka, Martin Kimath na Michael Mrutu ambao wote wako nje kwa dhamana.

Wanyama waliotoroshwa kwenda Doha wenye thamani ya Dola 113,715 za Marekani sawa na Sh170.5 milioni za Tanzania, walisafirishwa kwa kutumia maboksi marefu huku wakitumia ndege hiyo. Ushahidi ambao tayari umeshatolewa mahakamani unaeleza kuwa wanyama hao walikamatwa katika maeneo ya Mto wa Mbu, Elboreti na Engaruka wilayani Monduli.

Lugola: JK amemziba mdomo Warioba

Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Kangi Lugola.

Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Kangi Lugola amesema hotuba iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete imemziba mdomo Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.

“Tulitarajia itakuwa hivyo na ndiyo maana kulikuwa na ubishi kwa nini Rais Jakaya Kikwete asingetangulia kwa mujibu wa kanuni halafu ndiyo aje Mwenyekiti wa Tume wa Mabadiliko ya Katiba, Jaji  Warioba,” alisema.

Alisema hotuba  iliyotolewa na Rais Kikwete imekwenda mbali zaidi kwa sababu na yeye alikuwa anachangia katika utungaji wa katiba kutokana na kuchambua kifungu kwa kifungu.

“Nimemsikiliza...nimeyatafakari yale yote ambayo ameyatoa kwenye hutuba yake...kwa sababu alitoa msamiati kwamba tumia akili ya kuambia na uchanganye na ya kwako...basi ametuambia na sisi tutaenda kuchanganya na akili yetu katika kutunga katiba ya wananchi,” alisema.

Naye, Mjumbe wa Bunge hilo, Aden Rage alisema watahakikisha kwamba wanachukua ushauri wa Rais Kikwete ikiwa ni pamoja na kuweka maslahi ya taifa mbele.

“Tutaweka maslahi ya taifa mbele...interest (maslahi) ya nchi kwanza...tutashindana kwa hoja, na kuwahakikishia wananchi kupata katiba inayofaa,” alisema.

Bunge hatarini kuvunjika,adai mjumbe

Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mustapha Akunaay.

Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mustapha Akunaay, amesema kuna hatari kubwa la Bunge hilo kuvunjika kutokana na kauli iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete alipokuwa akihutubia wajumbe wa bunge hilo.

Akunaay ambaye pia ni Mbunge wa Mbulu (Chadema), alisema bila tahadhari, kuna hatari kubwa ya Bunge hilo kuvunjika.

Alitoa kauli hiyo, kufuatia Rais Kikwete kuzungumzia kwa undani na kusema muundo wa serikali tatu haufai na hauwezi kutekelezeka.

Alisema wao kama wajumbe na wabunge hawakutakiwa kulizungumzia suala la serikali mbili au tatu kwa sababu suala hilo lilishaamuriwa na wananchi.

“Rais Kikwete amezungumzia sana kuhusu serikali mbili kwa hiyo amewachanganya watu kuhusu muundo wa serikali mbili au tatu, sasa hali hii itakuwa ngumu zaidi kwenye kufanya uamuzi,” alisema.

“Maana dakika za mwisho kaja kusema kwamba msije mkaanza kung’ang’ania mambo ya kura, lazima mfanye mambo ya makubaliano...kwa hiyo mimi nimeachwa asilimia 30 kwa 70, alisema.

Mtendaji wa kijiji auawa kwa mapanga

Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Zelothe Steven.

Kundi la watu wasiofahamika, wamemuua kwa kumcharanga mapanga, Mtendaji wa kijiji cha Chakama kata ya Mwenge, Halmashauri ya mji wa Masasi mkoani Mtwara, Selemani Eckoni (32).

Mtendaji wa kijiji cha Mwenge, Mely Karim, alisema kuwa tukio hilo la kinyama lilitokea usiku wa kuamkia jana katika kijiji cha Mwenge wakati mtendaji huyo akiwa nyumbani kwake amejipumzisha.

Karim alisema taarifa za kuuawa kwa mtendaji huyo zilianza kuenea kijijini hapo jana asubuhi baada ya baadhi ya watu kusikia sauti ya mtoto wa marehemu, Makala Selemani (6), mwanafunzi wa Shule ya Msingi Mwenge akipiga mayowe kuomba msaada baada ya yeye kuona baba yake akiwa amelala nje ya nyumba yao akivuja damu kichwani huku pembeni yake kukiwa na kitanda cha kamba.

Alisema kufuatia mayowe ya mtoto huyo, wananchi walikusanyika katika nyumba ya marehemu na kukuta mtendaji huyo tayari amefariki dunia huku akiwa na majeraha makubwa kichwani.

Alisema baada ya watu hao kufanya mauaji hayo, waliingia ndani ya nyumba ya marehemu na kuchukua pikipiki moja aina ya Sanlg, deki moja ya televisheni na simu aina ya Nokia.

Kaka wa marehemu, Hassan Issa, alisema alipelekewa taarifa za kuuawa kwa ndugu yake akiwa nyumbani kwake.

Issa alisema alikwenda nyumbani kwa marehemu na kupiga simu polisi kuelezea taarifa za mauaji hayo.

Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Zelothe Steven, alithibisha kutokea kwa mauaji hayo.

Hata hivyo, Kamanda Steven alisema chanzo cha mauaji hayo hakijafahamika na hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa kuhusiana na mauaji hayo.

Baadhi ya ndugu wa marehemu wameliambia NIPASHE kuwa wakati wa uhai wake, mtendaji huyo aliyeacha watoto wanne, alikuwa akiishi peke yake.

Mbunge Kigwangalla mbaroni

Mbunge wa Nzega, Dk. Khamis Kingwangalla (CCM).

Mbunge  wa Nzega, Dk. Khamis Kingwangalla (CCM), ametiwa mbaroni na Jeshi la Polisi katika tukio la vurugu kwenye machimbo ya dhahabu.

Vurugu hizo ziliibuka jana katika machimbo ya dhahabu ya Mwashina yaliyopo wilayani Nzega, Tabora na Jeshi la Polisi kulazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya wachimbaji wadogo waliokuwa wakiandamana wakiongozwa na mbunge huyo.

Wananchi hao walikuwa wakiandamana jana kuanzia eneo la Isunga Ngwanda kuelekea katika machimbo hayo kupinga kitendo cha serikali kufunga machimbo hayo ambayo wamekuwa wakichimba dhahabu kwa muda mrefu na kuwasaidia kupata riziki.

Vurugu hizo ambazo zilianza majira ya mchana, zilisababisha watu wengine kadhaa kutiwa mbaroni sambamba na Dk. Kigwangalla.

Dk. Kigwangalla akizungumza na NIPASHE kwa simu muda mfupi baada ya kutiwa mbaroni, alisema wakiwa katika maandamano hayo polisi walianza kuwatawanya waandamanaji kwa mabomu ya machozi na yeye alifanikiwa kutoroka.

Hata hivyo, baadaye polisi walifanikiwa kumkamata na kumuweka ndani na hadi jana saa 10:45 jioni, mbunge huyo alikuwa bado chini ya ulinzi wa polisi huku waandamanaji wakiwa wametawanyika.

“Soma facebook yangu, nimenusurika kufa na sasa nimekamatwa na polisi na kuwekwa ndani…baada ya askari kuwatawanya wananchi kwa risasi za moto. Nitatoka kwenye mawasiliano sasa hivi,” alisema Dk. Kigwangala wakati akizungumza na NIPASHE.

Dk. Kigwangalla katika mtando wake wa facebook alisema katika vurugu hizo kijana mmoja aliyekuwa karibu naye alipigwa risasi baada ya riasi hiyo kumkosa yeye.

“Nimenusurika kuuawa muda si mrefu. Mungu mkubwa. Askari kwenye gari ananiambia na bahati yako nimekukosa, nililengwa kichwa....kijana mmoja aliyekaa mbele yangu amepigwa risasi kwenye paji la uso, sijui kama amenusurika,” alisema na kuongeza:

 “Vijana wamenilinda kwa ujasiri bila hofu. Leo askari wamenikamata kwa staha. Siwezi kukubali kamwe dhuluma ya mabepari dhidi ya wanyonge. Niliwaahidi na niliapa kuwatetea.”

Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Bituni Msangi, alisema alijulishwa kuwapo kwa vurugu hizo na Mkuu wa Polisi wa wilaya (OCD).

“Nipo nje ya wilaya, lakini nimepata taarifa kutoka kwa OCD kwamba kumetokea vurugu ila sijafahamu vurugu hizo zimesababishwa na nini,” alisema Msangi.

Hata hivyo, taarifa ambazo zililifikia gazeti hili jana  jioni, zilieleza kuwa wachimbaji  watano akiwamo mbunge huyo waliokamatwa sambamba na mbunge huyo wamewekwa katika kituo kikuu cha polisi wilayani humo.
 

Boti la wakimbizi lazama Ziwa Albert


Mili 25 imepatikana Ziwa Albert baada ya boti iliyokuwa imebeba wakimbizi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuzama.

Wakimbizi wa mapigano mashariki mwa Congo

Wakimbizi hao walikua wakitoroka kutoka kambi ya wakimbizi ya Kyangwali wilayani Hoima magharibi mwa Uganda, wakirejea kwao.

Kwa sasa Jeshi la polisi linaendelea na jitihada za kutafuta miili zaidi. Kamanda wa polisi wa eneo hilo John Ojukuna amesema watu 43 wameokolewa. Boti iliyozama inadhaniwa kuwa ilikua imebeba zaidi ya wakimbizi 100.

Wengi wa wakimbizi hao ni wale waliokimbia mapigano mashariki mwa Congo mwaka jana.

Mwendeshaji wa boti hiyo amekamatwa na jeshi la polisi na inadaiwa kuwa alikua amelewa. Wakimbizi waliookolewa wameambia polisi kuwa alikuwa mlevi na alikua akiendesha boti hiyo kwa kasi sana.

Hii sio mara ya kwanza ajali ya boti kuua watu katika Ziwa Albert kutokana na kujaza abiria na mizogo kupita kiasi.Miaka minne iliyopia boto nyingine ilizama na kusababisha vifo vya watu 70.

Waponea kifo mikononi mwa Boko Haram


Jeshi linaendelea kuwasaka wapiganaji wa Boko Haram

Wasichana waliotekwa nyara na kundi lenye itikadi kali za kidini, Boko Haram nchini Nigeria, wameielezea BBC ukatili walio upitia mikononi mwa kundi hilo.

Wakati wakizuiwa, wasichana hao walishuhudia watu kadhaa wakiwemo baadhi wanaotoka kijiji kimoja na wapiganaji wa kundi hilo, wakikatwa shingo.

Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 23, ameiambia BBC kwamba ameona kiasi ya raia hamsini wakiuawa mbele yake na Boko Haram.

Hili limefanyika miezi kadhaa iliyopita katika kambi moja katika eneo la mashambani, la kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.

Wakati huo huo msichana mwingine alieleza jinsi wapiganaji hao walivyo mlazimisha kumuua mwenziwe ambaye pia alitekwa nyara.

Wote walifanikiwa kutoweka kutoka kambi hizo na sasa wanaishi mafichoni.

Jeshi la Nigeria linasema linaendelea kuwasaka wapiganaji wa kundi la Boko Haram katika eneo hilo lililo mashinani.

Wapiganaji hao wanaendelea kuyashambulia miji na vijiji katika kiwango cha kushtusha ambapo zaidi ya raia mia tano wameuawa katika wiki za kwanza za mwaka huu.

Simu yawa mkombozi wa wajawazito Kilindi


Afya ya Mama na mtoto ni muhimu katika maendeleo ya kila Taifa. Ni vyema afya za kundi hili zizingatiwe kwa kiasi kikubwa ili kuepusha vifo hivyo.

Kilindi. Wengi kati yetu wanaifahamu simu kwa matumizi yao ya mawasiliano ambayo huitumia kuzungumza kirafiki au kutumiana ujumbe.

Kwingineko, simu inatumika kwa majukumu mengine yakiwamo ya tiba na imeonyesha mafanikio na kuwa mkombozi.

Wilayani Kilindi mkoani Tanga, imebainika kuwa teknolojia ya kisasa  inayoitwa Simu ya Teknolojia ya Utoaji wa Huduma ya Afya Ngazi ya Jamii  kwa Kutumia Data (MHEALTH) imefanya maajabu.

Huduma hiyo iliyoanzishwa na Mradi wa Afya Mama na Mtoto Kupitia Shirika la World Vision imewezesha wahudumu wa afya ya jamii kuwasaidia kinamama na watoto wanaozaliwa.

Mhudumu wa afya, Pili Juma anaeleza kuwa walipewa simu hizo mahususi kwa utoaji wa huduma kwa mama na mtoto chini ya umri wa miaka mitano na kwamba  zina uwezo mkubwa wa kutoa mwongozo kwao (wahudumu).

Anasema kuwa badala ya kutumia vitabu, sasa wanao mfumo rahisi wa kutumia simu unaomwezesha mhudumu kutoa huduma kwa mjamzito na kubaini matatizo yake.

Anaongeza kuwa simu hiyo inamwongoza mtumiaji wake kubaini tatizo alilonalo mjamzito na kama anatakiwa apelekwe kwenye kituo cha afya au hospitali ili kuokoa maisha yake, hufanyika hivyo haraka.

“Simu hizi zimerahisisha  utoaji huduma, hatuendi tena kupeleka taarifa kwenye vituo vya afya kwa kutumia mafaili au karatasi, hivyo taarifa za wajamzito na watoto zinapaikana kupitia teknolojia hii,” anasema.

Anaongeza kuwa teknolojia hiyo inawawezesha kuchukua maelezo ya mjamzito moja kwa moja kwenda kwa ofisa mradi huo, vituo vya afya au hospitali ya wilaya.

Simu inavyofanya kazi

Mtaalamu huyo anaeleza kuwa simu hiyo inamwonyesha mtoa huduma anapomtembelea mjamzito nyumbani anapokuwa na mimba chini ya miezi minne kwa mara ya kwanza anatakiwa apewe elimu ya kuhudhuria kliniki, kujua dalili za hatari wakati wa ujauzito na ushiriki wa wenza wao.

Pia, inamwonyesha mtoa huduma  akitoa elimu ya lishe bora wakati wa ujauzito na anaponyonyesha, wakati anapotaka kujifungua na kutoa ushauri wa kupima Ukimwi na kuzuia maambukizo yake kwenda kwa mtoto atakayejifungua.

Huduma nyingine itamwezesha mhudumu kutoa elimu kwa mama mjamzito kupima malaria na kumpima mtoto wake aliye na umri chini ya miaka mitano na kutoa ushauri kwa waume zao wahudhurie kliniki.

Aidha, mtoa huduma anapomtembelea mama huyo kwa mara ya pili atatoa elimu kwa kuyarudia yote aliyomweleza wakati alipomtembelea kwa mara ya kwanza.

Kwa mara ya tatu,  mtoa huduma atatoa elimu kwa mama huyo jinsi ya kumhudumia mtoto atakayezaliwa, dalili za hatari baada ya kujifungua ili akiziona aende kituo cha afya.

Pia, simu hiyo itamwonyesha mtoa elimu kwa mama mwenye Virusi vya Ukimwi (VVU) kuhusu  namna ya kumnyonyesha mtoto wake na kutumia uzazi wa mpango na kuzuia maambukizi katika jamii.

Ofisa Mradi wa Afya wa Afya Mama na Mtoto Wilaya ya Kilindi, Jacqueline Kawiche anaeleza kuwa mradi huo kwa kushirikiana na Shirika  la D-Tree wametoa simu hizo kwa wahudumu wa afya ya jamii ambazo zina programu inayoitwa Com- Care.

Kawiche anasema mhudumu wa afya anapokwenda kumtembelea mjamzito hataenda na makaratasi, hivyo atatumia simu hiyo ambayo ina mwongozo wa Wizara ya Afya wa kutumia Bango Kitita.

“Mwongozo ule wa Wizara ya Afya ambao kwa sasa unatolewa kwenye kaya kupitia makaratasi, sasa unatolewa kwa njia ya simu,” anaeleza.

Faida ya teknolojia hiyo ya simu inamrahisishia  mhudumu wa afya kufanya kazi  na  hivyo anapomhoji mjamzito ambaye ana matatizo hatarishi simu yake hutoa ishara  kuwa mama huyo apelekwe kituo cha afya.

Teknolojia hiyo ya simu inasaidia ukusanyaji wa taarifa kwa wakati, mfano mjamzito anapotembelewa kwenye kaya yake, taarifa hizo zinafika kwa ofisa afya, zinafika kituo cha afya au zahanati husika na baadaye zinatunzwa  kwenye mfumo wa taarifa kwenye hospitali ya wilaya.

Taarifa hizi za mama mjamzito zinakwenda kwa wakati na humsaidia mhudumu wa afya kutoa rufaa ya kumpeleka kituo cha afya kama atagundulika ana dalili hatarishi.

Usiyoyajua kuhusu uchunguzi wa miili ya maiti nchini Tanzania

Selemani Uliza akionyesha kitanda cha kusafishia na kuchunguza miili ya marehemu.

Maiti ya Adrian Louis iliokotwa kando ya barabara kuu ya kwenda Lukuledi wilayani Masasi katika Mkoa wa Mtwara.

Haikuwa na jeraha lolote. Ndugu zake walipopata taarifa za msiba, waliuchukua mwili na kuusitiri harakaharaka.

Hawakuwa na wasiwasi wowote wa kutaka kujua chanzo cha kifo cha ndugu yao kwani waliamini kuwa amefariki dunia kwa sababu ya kuzidiwa na ulevi, kwa kuwa siku zote alikuwa mlevi kupindukia. Kumbe, walikuwa wamekosea, kwani siku hiyo Louis hakuwa amelewa, bali kifo chake kilisababishwa na majambazi waliompora fedha kabla ya kumnyonga  hadi kufa.

Yapo matukio mengi ya namna hiyo katika sehemu mbalimbali nchini, lakini mengi kati ya hayo hayafanyiwi uchunguzi wa kujua chanzo.

Daktari wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa na Kiongozi wa Idara ya Uchunguzi wa Vifo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Innocent Mosha anasema ni muhimu kufanya uchunguzi wa sababu za kifo ili kujiondolea shaka au wasiwasi wa kipi kilisababisha kifo hicho.

Dk. Mosha anaelezea maana ya uchunguzi wa kifo na kusema kuwa ni  kitendo cha madaktari kutafuta chanzo kilichosababisha kifo cha mtu na kujiridhisha au ndugu kuridhika pasipo shaka.

“Watanzania walio wengi bado hawafahamu umuhimu wa kufanya uchunguzi wa vifo vya ndugu zao, jambo ambalo linasababisha wakati mwingine kupoteza ushahidi au kukosa  cheti cha kifo ambacho kina umuhimu mkubwa katika masuala ya mirathi,” anasema Dk Mosha

Anasema uchunguzi wa kifo si kwa ajili ya polisi wa upelelezi tu, bali ni mchakato unaotakiwa kufanywa  na ndugu wa marehemu ili kujiridhisha na sababu ya kifo cha ndugu yao.

Anaongeza kuwa tatizo kubwa hapa nchini ni kuwa watu wengi hawaelewi maana na umuhimu wa kuchunguza miili ya ndugu zao ili kujua chanzo au sababu za vifo vyao.

Mchakato wa Uchunguzi

 Kwanza, Dk. Mosha anasema uchunguzi wa kifo kwa matukio yanayohusisha polisi, huhitaji taarifa ya utangulizi ambapo polisi hutakiwa kutoa maelezo ya awali kuhusu marehemu.

Anasema pia kuwa katika matukio hayo, ndugu zaidi ya mmoja  huhitajika kwa ajili ya kumtambua marehemu,  sanjari  na kujaza fomu ya maelezo mafupi. “Baada ya polisi kutoa maelezo yao ambayo kwa kawaida huwa ni mafupi, daktari huendelea na uchunguzi wake kulingana na ujuzi wake,” anasema.

 Anaeleza kuwa zipo hatua kadhaa za kufanya uchunguzi wa kifo ambazo  hazina budi kufuatwa. Anazitaja kuwa marehemu huchunguzwa  sehemu za nje za mwili akiwa na nguo zake.

“Hapo daktari huangalia mazingira ya nje, kwa mfano nguo alizovaa; iwapo zina damu; damu imeingiaje, kama zimechanika  na zilikuwa katika mazingira gani. Utambuzi huu wa awali wakati marehemu amevaa nguo zake, huweza kutuonyesha mazingira ya nje iwapo kulikuwa na purukushani kabla ya kifo au la,” anasema.

Baada ya hapo, Dk. Mosha anasema daktari hutakiwa kwenda hatua ya pili ya kuchunguza ndani ya mwili ambapo mwili wa marehemu huchunguzwa kwa umakini mkubwa kama kuna chochote kitakachoashiria sababu ya kifo chake.

 Kwa mfano, Dk. Mosha anasema majeraha ya mwili huangaliwa, pia mazingira ya majeraha hayo.

Anaongeza kuwa hapo daktari anaweza kujua iwapo marehemu alipigwa alizama majini, alikunywa maji mengi au  kuzamishwa majini.

“Kama mtu amezama majini ni rahisi kujua kwani macho yake huwa na mshipa midogo midogo iliyovilia damu. Mwingine huwa na kitu kinachoitwa ‘Perypheral discoloration’ ambapo  kisigino cha marehemu huwa na rangi ya bluu kwa sababu ya kukosa hewa ya oksijeni.” Mtaalamu huyo anasema wakati mwingine uchunguzi wa vifo hivi ni  muhimu kwani husaidia kujua iwapo mtu amefia majini au aliuawa, kisha akatupwa kwenye maji.

Uchunguzi wa mwingine wa vifo vya marehemu huweza kuhusisha kumpasua mwili na kisha kuangalia ogani kama ini, figo, mishipa ya damu, utumbo na kifua.

 Pia, mwili wa marehemu huangaliwa kama kuna uvimbe usoni, mapafu kujaa maji na wakati mwingine mapafu hutolewa na kupimwa kama yameingia maji na maji hayo ni ya aina gani.

 Kuna watu wanaofariki wanaodhaniwa kuwa wamejinyonga kuna utaalamu wa kuangalia kama kweli wamejinyonga au walinyongwa na kutundikwa.

Anasema uchunguzi wa kifo cha marehemu si lazima kuukatakata mwili,  bali wakati mwingine  wataalamu wanaweza kuchukua maelezo au kukata  sehemu ndogo tu ya mwili huo.

“Wakati mwingine iwapo mgonjwa amefariki dunia kwa kuugua malaria au aliletwa hospitali akiwa anaumwa ugonjwa huo na kama amekufa, basi ili kuthibitisha sababu ya kifo hicho, tunaweza kukata tishu kuangalia dalili za malaria katika mwili, kuangalia rangi ya manjano katika macho au wakati mwingine kipande cha ini kinachunguzwa,” anasema.

Gharama za uchunguzi

Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi wa Muhimbili, Dk.  Praxeda Ogweyo anasema  gharama za uchunguzi kwa watu wa kawaida ni  Sh200,000, lakini kwa raia wa kigeni ni 800,000. Anasema kwa madaktari wanaotaka kufanya uchunguzi wa vifo kwa sababu za kitaaluma hawatozwi gharama zozote na kwa polisi gharama zao hulipwa na serikali.

Dk. Ogweyo anasema ni wakati kwa Watanzania kujifunza na kuujua umuhimu wa uchunguzi wa vifo vya ndugu zao kwa kuwa husaidia kusuluhisha migogoro ndani ya familia.

“Kama ndugu wanahisi  kuwa kifo cha ndugu yao kina utata basi uchunguzi unasaidia. Mara nyingi mtu anapofariki ghafla huleta utata kwa jamii,” anasema

Dhana au mazoea

Dk. Mosha anasema kuna dhana zilizozoeleka kuwa  kama mtu ameuawa, basi sura ya muuaji huonekana kwenye macho ya marehemu, lakini anasema  hilo halina ukweli kwani kinachoonekana machoni ni kuvilia kwa damu au kuvimba kwa macho kwa sababu kama za kunyongwa.

Takwimu za uchunguzi

Kuhusu hilo, Dk. Mosha anasema  Watanzania wengi hawafanyi uchunguzi wa vifo vya marehemu ndugu zao kwa sababu ya dhana potofu kuwa ndugu zao hukatwakatwa au kuibiwa baadhi ya viungo. “Wengi wanaochunguza vifo vya marehemu ni polisi kwa sababu za kipolisi na madaktari kwa sababu za kitaaluma. Lakini watu wa kawaida bado hawana uelewa kuhusu uchunguzi wa vifo.”  Kwa mfano, takwimu za  hapa Muhimbili zinaonyesha kuwa uchunguzi wa vifo vya marehemu unaofanywa kwa maombi ya ndugu ni watu wawili hadi wa tatu kwa mwezi wakati uchunguzi unaofanywa kwa maombi ya polisi ni matukio sita hadi saba kwa wiki.

Sababu za kuchunguza miili

 Dk. Mosha anasema, uchunguzi wa miili ya marehemu una umuhimu mkubwa katika kufahamu sababu za kifo na kujiridhisha.

Lakini pia, uchunguzi huu huwasaidia madaktari kujifunza kutorudia makosa ya kitabibu au kujua kifo kilisababishwa na nini wakati wa matibabu. “Kwa mfano mtu aliyepata ajali akaumia kichwa, madaktari huangalia jeraha la kichwani  pekee. Hata hivyo, baadaye uchunguzi wa kifo huonyesha kuwa  utumbo wa marehemu ulipasuka na ndicho chanzo cha kifo, tunajiridhisha,” anasema.

Sheria na uchunguzi wa kifo

Kisheria, uchunguzi wa kifo cha marehemu unatakiwa kufanyika ndani ya saa 24 iwapo mgonjwa alikuwa akiugua maradhi kama malaria.

 “Iwapo mtu amefariki dunia halafu kuna daktari alikuwa akimwangalia, basi uchunguzi wake unatakiwa kufanyika ndani ya siku 14 na hapa si lazima kumpasua marehemu.

Kisheria, wiki mbili zikipita hata daktari aliyekuwa akimtibu hawezi kumfanyia ‘post- mortem’ kwani hana nguvu za kisheria kufanya hivyo,” anasema.

Wakili wa Kujitegemea wa Kampuni ya Kakamba and Partners, Mathew Kakamba anasema kisheria uchunguzi wa kifo husaidia kupata uthibitisho wa kina kuhusu chanzo au sababu ya kifo.

“Kama watu wanadai marehemu alinyweshwa sumu, basi ripoti ya post-mortem (uchunguzi baada ya kifo) huleta kithibitisho kama ni kweli ni sumu na ni sumu ya aina gani na imesababisha vipi kifo,” anasema

Anasema  ripoti hii huondoa utata.   Huweza kubadili mwelekeo  wa kesi.

Mauaji Darfur vita vikiendelea

Askari wa Sudan
Askari wa kikosi cha Sudan katika jimbo la Darfur

Shirika la haki za binadamu Human Rights Watch linasema makumi kadhaa ya watu waliuawa katika ghasia zinazoendelea katika jimbo la Darfur nchini Sudan.

Shirika hilo linasema viongozi wa kijamii katika vijiji viwili wametoa orodha ya majina ya raia takriban arobaini waliouawa katika wiki chache zilizopita kwenye makabiliano baina ya vikosi vinavyounga mkono serikali na vile vya waasi.

Human Rights Watch linasema wanavijiji wengine makumi kadhaa walishambuliwa, baadhi yao wakipigwa na makombora ya ndege za kijeshi. Shirika la msalaba mwekundu limesema mmoja wa wafanyakazi wake aliuawa jana.

Umoja wa Mataifa unasema mwaka huu pekee zaidi ya watu laki mbili wameyakimbia makazi yao jimboni Darfur.

AU yazidisha vita dhidi ya Al Shabaab

Al Shabaab

Mamia ya wanajeshi wa Muungano wa Afrika wanaukaribia mji muhimu wa Koryoley, ulio umbali wa kilomita 90 Kusini Magharibi mwa mji mkuu Mogadishu.

Mji wa Koryoley, umekuwa chini ya udhibiti wa kundi la wanamgambo la Al Shabaab kwa miaka mitano iliyopita.

Mwandishi wa BBC aliye katika eneo hilo anasema kuwa wanajeshi hao wako umbali wa kilomita 10 kutoka mjini humo.

Anasema kuwa ikiwa wanajeshi hao wataukomba mji huo, utakuwa ukombozi wao mkubwa wa mji tangu kuanza harakati hizo dhidi ya Al Shabaab mwezi Machi mwaka jana wakiungwa mkono na Umoja wa Mataifa.

Wanajeshi hao wamefanikiwa kukomboa miji mingine muhimu na hata kuwatimua wapiganaji hao kutoka katika ngome zao kubwa.

Wengi wa wanajeshi wa AU ni kutoka Uganda, wakisaidiwa na wanajeshi wa Kenya, Burundi na sasa Ethiopia pamoja na wanajeshi wa Somalia.

BABA AUA MTOTO WAKE WA MIAKA SABA KISA ETI NI MZURULAJI

KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA KAMISHNA MSAIDIZI MWANDAMIZI WA POLISI
 AHMED Z. MSANGI 

MTOTO AITWAYE IREENE MARCO MBEMBELA (07) MWANAFUNZI CHEKECHEA SHULE YA MSINGI MIGOMBANI NA MKAZI WA SOGEA ALIFARIKI DUNIA WAKATI AKIENDELEA KUPATIWA MATIBABU KATIKA KITUO CHA AFYA TUNDUMA.

MAREHEMU ALIPIGWA KWA KUTUMIA FIMBO SEHEMU MBALIMBALI ZA MWILI WAKE HADI KUPOTEZA FAHAMU  NA BABA YAKE MZAZI  ALIYEFAHAMIKA KWA JINA LA MARCO MBEMBELA (30) MKAZI WA SOGEA – TUNDUMA.

TUKIO HILO LILITOKEA TAREHE 19.03.2014 ALFAJIRI HUKO SOGEA KATA NA TARAFA YA TUNDUMA WILAYA YA MOMBA KWA TUHUMA KUWA ANATABIA YA  KUZURURA OVYO KATIKA NYUMBA ZA WATU.

KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA KAMISHNA MSAIDIZI MWANDAMIZI WA POLISI AHMED Z. MSANGI ANATOA WITO KWA WAZAZI/WALEZI KUTUMIA BUSARA KATIKA KUWAELEKEZA NA KUWAONYA WATOTO WAO BADALA YA KUWAPIGA KWANI NI HATARI KWA AFYA NA MAISHA YAO.

Kikwete na ujumbe mzito

Rais Jakaya Kikwete 


Dodoma. Rais Jakaya Kikwete kesho ataambatana na ujumbe mzito wa marais wastaafu wa pande zote za Muungano, wake wa waasisi wa taifa na mawaziri wakuu wastaafu atakapokwenda kuzindua Bunge Maalumu la Katiba.

Hatua ya Rais kuambatana na ujumbe huo imepongezwa na viongozi wa vyama vikuu vya upinzani nchini, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na mwenzake wa Chadema, Freeman Mbowe.

Mbali na viongozi hao, Rais Kikwete pia ataambatana na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein na Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad.

Wanaotarajiwa kuwamo katika msafara huo ni Rais wa pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi, Rais wa tatu, Benjamin Mkapa na marais wastaafu wa Zanzibar, Dk Salmin Amour na Amani Abeid Karume, Mama Maria Nyerere na Mama Fatma Karume.

Miongoni mwa mawaziri wakuu wastaafu wanaotarajiwa kuwamo ni pamoja na Jaji Joseph Warioba, ambaye juzi aliwasilisha bungeni hapo Rasimu ya Katiba kwa kutoa hotuba iliyoliteka Bunge kwa jinsi alivyofafanua mambo mengi yenye utata kuhusu muundo wa Muungano.

Mawaziri wakuu wengine ni Cleopa Msuya, John Malecela, Dk Salim Ahmed Salim, Frederick Sumaye pamoja na Edward Lowassa na Mizengo Pinda ambao ni wajumbe wa bunge hilo.

Wengine walioalikwa ni mabalozi wa nchi mbalimbali, wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, viongozi wa dini, vyama vya wafanyakazi, vyama vya siasa, wafugaji, wakulima, wavuvi na wawakilishi wa sekta binafsi.

Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Yahaya Khamis Hamad aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Rais Kikwete atahutubia Bunge hilo kwa mujibu wa Kanuni ya 75 (1).

Rais Kikwete atapokewa katika Viwanja vya Bunge na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta na baadaye kukagua gwaride maalumu kabla ya kuhutubia Bunge kuanzia saa 10:00 jioni.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa jana, baada ya Rais kuhutubia saa 11:35 jioni, aliyekuwa mwenyekiti wa muda wa bunge hilo, Pandu Ameir Kificho atatoa neno la shukurani kabla ya Rais kupiga picha za kumbukumbu na wajumbe wa Bunge hilo.

Suala la hotuba ya Rais Kikwete limekuwa sehemu ya mjadala katika Bunge hilo kutokana na baadhi ya wajumbe kuhoji sababu za Jaji Warioba kuwasilisha Rasimu kabla ya Rais kuzindua Bunge kwa mujibu wa kanuni.

Mjadala huo uliwafanya baadhi ya wajumbe kumzuia Jaji Warioba Jumatatu iliyopita kuwasilisha rasimu hiyo kama ilivyokuwa imepangwa hadi kilipofanyika kikao cha maridhiano siku hiyohiyo usiku na kufikia mwafaka kwamba Mwenyekiti huyo wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba awasilishe Rasimu juzi na Rais ahutubie kesh

Lipumba, Mbowe na Mtatiro

Akizungumzia ujumbe huo, Profesa Lipumba alisema hiyo inaonyesha jinsi mkuu huyo wa nchi alivyolipa uzito bunge hilo.

Profesa Lipumba ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), ulioundwa na baadhi ya wajumbe wa bunge hilo alisema ni jambo jema kwa Rais kulizindua Bunge hilo kwa kuwa ndiye mwasisi wa mchakato wa Katiba Mpya... “Ujio wake utasherehesha Bunge hili na nasaha zake zitatusaidia.”

Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni alisema tendo la kuandika Katiba ni kubwa na linalohusu wananchi wote hivyo ni dhahiri kuwa marais wastaafu na wake wa waasisi wa Muungano wana fursa ya kipekee kuhudhuria uzinduzi huo.

“Nina hakika wapo viongozi wengine walioalikwa. Kwa msingi huu, sina tatizo na ushiriki au ualikwa wao kwani bado wana heshima katika jamii kama viongozi wastaafu,” alisema na kuongeza:

“Ni matumaini yangu kuwa hotuba ya Rais itasaidia kupunguza hofu na hisia hasa kwa makundi yanayohasimiana katika Bunge hili na siyo kuongeza hofu na ufa.”

Alisema wapo viongozi wa Bunge ambao wamekuwa wakiwaona baadhi ya viongozi kama ni wafanya fujo... “Bunge la Katiba ni tofauti na Bunge la kawaida na linahitaji kuvumiliana na kustahimiliana sana wanachokitazama kama fujo kwa wengine ni staili muhimu ya kudai kusikilizwa. Walichokiona kama fujo kimesaidia wabunge wote na hata Watanzania kusikia kwa kina taarifa ya mheshimiwa Warioba. Fujo zile ndizo zilizozaa saa nne alizopewa mheshimiwa Warioba na timu yake na kuleta utulivu mkubwa katika nchi.”

Alisema kilichoonekana kama rabsha na fujo kwa Rais wakati alipozindua Bunge la 10 ndicho kilichozaa mchakato huu wa Katiba. Katika Bunge hilo, wapinzani walisusia hotuba ya Rais Kikwete ambayo pamoja na mambo mengine, alitangaza kuanza kwa mchakato wa Katiba Mpya.

Mjumbe wa Bunge hilo, Julius Mtatiro alisema anatarajia Rais atasisitiza umuhimu wa maridhiano, maelewano, kuheshimiana baina ya wajumbe na kuwataka watilie maanani masilahi ya taifa badala ya kundi mojamoja au vyama.

Malaysia:Shughuli zaendelea kuisaka ndege

Picha za kinachodhaniwa kuwa mabaki ya ndege ya Malaysia nchini Australia
Ndege na meli kutoka nchi mbali mbali zinaendelea kuitafuta mabaki ambayo huenda yanatokana na ndege ya Malaysia iliyopotea takriban wiki mbili zilizopita ikiwa imebeba takriban watu 240.
Matumaini ya kutatua kitendawili hicho yaliongezeka baada ya Australia kutoa picha za Satelaiti za vitu viwili vilivyoonekana baharini vuikidhaniwa kuwa vifusi vya ndege hiyo.
Hata hivyo hadi kufikia sasa hakuna cha maana kilichopatikana.
Afisa mmoja mkuu wa New Zealand amesema operesheni hiyo ilitatizwa na kuchafuka kwa bahari na kutoona vizuri.
Meli ya mizigo ya Norway ilitumia taa kuyatafuta mabaki hayo pasina kufanikiwa.

Kizungumkuti cha amani Sudan Kusini


Makamu wa Rais wa zamani wa Sudan Kusini Riek Machar analaumiwa kwa kupanga njama ya mapinduzi

Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya Sudan Kusini na waasi wanaoongozwa na aliyekuwa naibu wa rais wa nchi hiyo Riek Machar yanatarajiwa kuanza tena leo mjini Addis Ababa Ethiopia.

Mazungumzo hayo yaliahirishwa mapema mwezi huu baada ya mazungumzo ya hapo awali kukwama.

Aidha, pande zote mbili zimetuhumiwa kwa kukiuka mkataba wa kusitisha mapigano uliotiwa saini mwezi Januari.

Mnamo siku ya Jumatano, mataifa ya magharbi yanayohusika na mgogoro huu wa Sudan Kusini katika kuutafutia suluhu la kudumu, walitishia kuwawekea vikwazo wahusika wakuu kwenye mgogoro huo ikiwa hawatausuluhisha.

Mazungumzo ya kuzipatanisha pande hizo hayajapiga hatua kwa wiki mbili zilizopita huku wahusika wakilaumiana.

Serikali na waasi wanalaumiana kwa kuyumbisha mazungumzo ya amani

Nao mkataba wa amani uliotiwa saini kusitisha vita pia haujafanikiwa katika kumaliza mgogoro huo.

Baadhi ya wanadiplomasia kutoka nchi za magharibi, wamehoji ikiwa viongozi wamejitolea kikweli kutafuta muafaka huku kila mhusika akimlaumu mwenzake kwa kizungumkuti kilichoko.

Mazungumzo hayo yanaanza tena baada ya wiki mbili ya kusitishwa kwake, ingawa wajumbe wamesema haijulikani ikiwa pande hizo mbili zitakuwepo.

Maswala makuu yanayoyumbisha mazungumzo hayo, ni matakwa ya waasi wa Sudan Kusni kwamba wafungwa wanne wa kisiasa ambao bado wanazuiliwa, sharti waachiwe huru.

Wanne hao walilaumiwa kwa kupanga njama ya mapinduzi dhidi ya serikali ya Rais Salva Kiir wakiongozwa na aliyekuwa makamu wa Rais Riek Machar

Majibizano kati ya Marekani na Urusi UN


Mabalozi wa Marekani na Urusi wameshambuliana katika Umoja wa mataifa.
Majibizano makali yameshuhudiwa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo mataifa mengi yameshutumu
uamuzi wa Urusi kunyakua eneo la Crimea,kilele hatahivyo ilikuwa majibizano makali baina ya mabalozi wa Marekani na

Urusi .

Balozi wa Urusi, Vitaly Churkin, alisema kuwa watu wa Crimea walikuwa wamefanya maamuzi yao juu ya siku zao za

usoni.

Naye Balozi wa Marekani, Samantha Power akajibu akisema kile kinachotajwa na Urusi kama kura ya maoni ni kura

bandia.

Akikasirishwa na matamshi ya Power, Bwana Churkin alisema kuwa Balozi Power alikuwa amejishushia hadi kufikia

kiwango cha magazeti ya udaku.

Balozi huyo wa Urusi pia alitisha kuwa huenda Urusi ikakataa kushirikiana na Marekani katika maswala mengine muhimu

ya kimataifa iwapo Marekani itaendelea na msimamo wake juu ya Ukraine.

Majibizano hayo makali yanaendelea wakati Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon anapoelekea Urusi kufanya

mashauriano na Rais Putin kwa lengo la kutafuta suluhu ya kidiplomasia.

Mkuu wa Majeshi nchini Ukraine, Andriy Parubiy, amesema Serikali yake inafanya kila juhudi kuwarejesha nyumbani

wanajeshi wake na familia zao walio eneo la Crimea, kufuatia hatua ya Urusi ya kunyakua Crimea.

Ulevi wa Shisha washika kasi

Mtumiaji wa shisha akipata kilevi hicho


Dar es Salaam. Umeibuka ulevi mpya nchini ambao umethibitika kuwateka vijana hasa wa jiji la Dar es Salaam, huku kukiwa na taarifa za kitaalamu kwamba ulevi huo una athari za kiafya kwa watumiaji.

Ulevi huo ni kupitia starehe au anasa mpya ya uvutaji shisha; ulevi ambao watengenezaji hutumia chombo maalumu chenye bomba la kutolea moshi, ambacho huwekwa tumbaku, maji na moto.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa tumbaku huwekwa katika chombo hicho na kuunguzwa kwa moto, kisha moshi wa tumbaku hupita kwenye maji na huingia kwenye bomba, kisha watumiaji huanza kuvuta.

Sehemu maarufu ambako shisha inauzwa ni Ufukwe wa Coco, maeneo ya Kinondoni, Mwananyamala, Sinza Barabara ya Shekilango na maeneo kadhaa ya mitaa ya mjini.

Mmoja wa watumiaji wa shisha, Ismail Ndunguru alisema yeye na vijana wenzake hutumia siku za mwisho wa wiki kwenda kuburudika kwa uvutaji katika hoteli moja iliyopo mjini, Mtaa wa Garden jijini Dar es Salaam.

“Kuvuta shisha kwa siku nzima ni Shilingi 10,000, mkimaliza, mnarudisha bomba. Tukiwa vijana wengi inafurahisha sana kuvuta,” alisema Ndunguru.

Taarifa za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaeleza kuwa, mkupuo mmoja wa shisha, una kemikali hai 4,800 na kwamba kemikali hizo husababisha saratani ya mapafu, maradhi ya moyo na maradhi ya mfumo wa upumuaji.

WHO inaeleza kuwa, kiasi cha uvutaji wa shisha kwa saa moja ni sawa na kuvuta sigara 100 au 200.

Daktari Bingwa wa magonjwa ya ndani ya mwili na mfumo wa hewa, Meshack Shimwela alisema madhara ya shisha ni kama yale yanayosababishwa na uvutaji wa sigara pengine na zaidi kutokana na kilevi hicho kuwa na tumbaku nyingi.

Dk Shimwela alisema licha ya kuwa watengenezaji na wavutaji wa shisha hudai kuwa haina madhara kwa sababu huchanganywa na maji, lakini bado madhara yake ni makubwa.

“Maradhi yote yanayosababishwa na uvutaji wa sigara ndiyo yanayosababishwa na shisha, kwa mfano saratani ya mapafu na mdomo, kifua kikuu na mzio ambao unaweza kusababisha pumu,” alisema Dk. Shimwela.

Dk. Shimwela alisema ni vizuri watumiaji wakajua madhara ya shisha, badala ya kuchukulia kuwa ni mtindo wa maisha tu au starehe isiyo na madhara.

Hivi karibuni, Profesa Twalib Ngoma, Mkurugenzi wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, alisema asilimia 40 ya saratani zote nchini zinasababishwa na matumizi ya tumbaku.

Biashara inavyofanyika

Shisha inauzwa katika sehemu kadhaa za starehe za Jiji la Dar es Salaam kwa sasa na maeneo yanayouza bidhaa hiyo yanafahamika kama ‘shisha lounge au shisha point’.

Mwandishi wa Mwananchi akiambatana na Ndunguru walikwenda hadi Kinondoni katika hoteli moja ambako wavutaji wa shisha walikuwa wakiendelea ‘kuburudika’ huku wakipuliza moshi hewani.

Waliitozwa Sh15,000 kisha nao waliletewa chombo cha kuvutia. Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa unaonyesha kuwa bei ya shisha hutegemea sehemu inapouzwa, hivyo huuzwa kati Sh10,000 na 70,000.

Ndunguru alisema shisha haina madhara kwake ingawa alipovuta kwa mara ya kwanza, alikohoa sana lakini sasa anaiona kuwa kiburudisho kinachompa faraja kama wavutaji wa sigara na kwamba hamu ya kuvuta kila mara imeingia mwilini mwake.

Ilibainika kuwa kwenye shisha huwekwa ladha kadhaa kama vile vanila, strawberry, mint, chocolate au kahawa ili kuwavutia wavutaji. Ladha hizo zinatajwa kuwa kivutio cha mabinti ambao wameingia kwa kasi kwenye uvutaji huo.

Kadhalika uchunguzi ulibaini kwamba wanafunzi wa shule za sekondari na vyuo vikuu, kwa makundi hujikusanya na kuchanga fedha kwa ajili ya kuvuta shisha.

Habari zaidi zinadai kuwa wafanyabiashara wa shisha hivi sasa wanachanganya dawa za kulevya kama heroin na bangi katika shisha kama kivutio kwa watumiaji.

“Hii ni biashara kubwa sana sasa hivi, kwa siku moja, mimi naingiza zaidi ya Sh150,000 kwa kuuza bomba la shisha,” anasema mfanyabiashara mmoja wa Kinondoni.

Muuzaji wa shisha katika eneo la Coco Beach, Said Coco alisema biashara hiyo ni nzuri na kwamba wateja wamekuwa wakiongezeka kadiri kila siku.

Coco alisema wateja wake wakubwa ni vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 40 ambao huvuta shisha kila mwishoni mwa wiki.

Hata hivyo, alikanusha habari kwamba wafanyabiashara wanaweka dawa za kulevya na bangi kwenye shisha, ingawa anasema kama wapo wanaofanya hivyo basi wanaharibu starehe hiyo ambayo yeye anasema haina madhara.

Serikali inasemaje?

Waziri wa Afya, Dk Seif Rashid alisema anafahamu kuwa shisha imepata umaarufu nchini hususan Dar es Salaam, lakini ni vigumu kuwakamata watumiaji.

Alisema wizara haiungi mkono matumizi ya shisha kwani inafahamu kuwa ni kilevi hatari pengine kuliko sigara za kawaida na pombe.

“Shisha ni hatari na sisi hatuungi mkono, lakini hatuwezi kuwakamata watumiaji kama ambavyo hatuwezi kuwakamata walevi wa sigara na pombe. Lakini tunawaasa watengenezaji wa shisha kuweka nembo ionyeshayo kuwa ni kilevi hatari,” anasema.

Dk. Rashid alisema matumizi ya tumbaku yanasababisha maradhi mengine hasa saratani ambayo inasababisha kiharusi, maradhi ya moyo na ngozi.

Kwa upande wake Kamishna wa Polisi Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa alisema hana taarifa za ongezeko la matumizi ya shisha nchini, ingawa aliwahi kuona kilevi hicho nchini Misri.

Nzowa alisema ikiwa itagundulika kuwa shisha ina wingi wa Nicotine, atachukua hatua kali dhidi ya wahusika, huku akitoa mfano wa kilevi cha kuber kilichowahi kupigwa marufuku.

Asili ya shisha

Shisha ni jina lenye asili ya Misri (sheesha) lenye maana ya bomba la maji lililounganishwa kwenye kontena.

Tumbaku iliyochanganywa na ladha ya matunda, hujazwa kwenye chombo mfano wa chetezo, moto huwekwa kati na sehemu moja huwekwa maji.

Moshi wenye harufu au ladha hutoka kupitia bomba hilo na kuvutwa.

Mvutaji huvuta kwa kutumia bomba (huweza kuwa la plastiki) na mabomba mengine yanaweza kutumiwa na kutupwa (disposable).

Athari zake kiafya

Kuharibu ogani; Shisha inatajwa kuwa na hewa ya carbon monoxide ambayo huingia kwenye mapafu na kuchukua nafasi ya hewa safi ya oxygen, hivyo ogani muhimu kuharibika.

Saratani; Shisha ina wingi wa nicotine, kiwango cha kemikali za tar, carbon monoxide, metali za kiwango cha juu kama cobalt na lead ambavyo ni visababishi vya saratani.

Utegemezi (adiction); Uvutaji wa shisha husababisha kutengenezwa kwa kiwango kikubwa cha nicotine kwenye damu, hivyo mtu akishazoea kuvuta hawezi kuacha kwani kilichomo kwenye shisha huvutwa kwenye neva za fahamu na kusababisha mishipa hiyo kwenye ubongo kuhisi kupata faraja na raha ya kipekee.

Maradhi ya kuambukiza; Uvutaji wa shisha hutumia bomba ambalo watu kadhaa hushirikiana. Hali hii husababisha maradhi ya kuambukiza kama Kifua Kikuu (TB) na hepatitis B (homa ya ini).

Mwanasheria Mkuu SMZ haujui waraka wa Kificho

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Muda wa Bunge Maalumu la Katiba, Amir Pandu Kificho akimkaribisha kwenye kiti, Mwenyekiti wa Kudumu wa Bunge hilo, Samuel Sitta baada ya kuapishwa kushika nafasi hiyo, bungeni Dodoma jana.  
Picha na Emmanuel Herman 


Zanzibar. Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Masoud Othman Masoud amesema hajawahi kuuona waraka ulioandikwa na Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW) na kusainiwa na Spika Pandu Ameir Kificho unaopendekeza Tanganyika na Zanzibar kuwa na mamlaka huru za dola na kuwasilishwa mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Akizungumza na Mwananchi AG Masoud amesema waraka huo ulitayarishwa na kamati ya uongozi chini ya Mwenyekiti wa kamati hiyo Spika Kificho, baada ya kufanyika vikao vilivyowahusisha wajumbe wa kamati ya uongozi ya Baraza hilo na kutoa mapendekezo yake.

Masoud alisema licha yeye kuwa si mjumbe wa kamati hiyo lakini huingia kama mjumbe mualikwa, ambapo kikao cha kwanza alishiriki kujadili mambo ya msingi yanayotakiwa kuwasilishwa katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba kama maoni ya taasisi lakini hakumbuki kuhudhuria kikao cha mwisho ambacho kiliandaa mapendekezo hayo.

“Mpaka sasa waraka uliowasilishwa mbele ya Tume ya Jaji Warioba bado sijauona kwa macho yangu, siwezi kusema kama ulikuwa waraka halali au batili ila nasikia mivutano inayojitokeza miongoni mwa wajumbe wake,” alisema AG Masoud.

Alisema Baraza kama Taasisi lilitoa maoni kama walivyotoa maoni baadhi ya makatibu wakuu wa SMZ na taasisi nyingine ambazo zinaguswa au kufanya kazi zinazohusiana na mambo ya msingi yaliomo katika orodha ya mambo ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Aidha, alisema kama kamati ya uongozi ya Baraza akidi ya wajumbe ikitimia ina uwezo wa kutoa mapendekezo kwa niaba ya taasisi na kusema si mwafaka kwa sasa kumjadili Spika peke yake, kama kuna ukiukwaji wa sheria au kanuni za Baraza kulikojitokeza.

Pia Mwanasheria Mkuu huyo wa SMZ alibeza kitendo cha Baraza la Wazee wa CCM kuondoa imani kwa Spika Kificho na kumtaka ajiuzulu, badala yake alisema kama kuna makosa yamefanyika, basi kamati nzima ya uongozi ya Baraza hilo inatakiwa ijiuzulu.

“Si haki na sahihi kumshinikiza Spika ajiuzulu, kama kuna kasoro zimefanyika, kamati nzima ya uongozi ya BLW nayo inapaswa kuwajibika. Suala hilo halikuwa la Spika ila ni la taasisi,” alisema Mwanashseria Mkuu huyo wa SMZ.

Alisema kimsingi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar haina maoni wala mapendekezo yake kuhusu mabadiliko ya muundo wa Muungano uweje na hata Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, hajawahi kuweka bayana msimamo wake kama kiongozi Mkuu wa Zanzibar.

Hata hivyo AG Masoud alikiri kuwa msimamo pekee ambao Dk Shein amekuwa akiutetea ni ule wa chama chake wa kuendelea kuwapo muundo wa Muungano wa Serikali mbili ambao hautokani na msimamo wa SMZ.

Mwanasheria Mkuu huyo pia alisema ni mapema kwake kutoa tathmini na mwelekeo wa mjadala wa Bunge la Katiba kama Zanzibar itaweza kufikia malengo yake ya kupata katiba yenye masilahi na Zanzibar, kutokana na mgawanyiko uliopo wa wajumbe kutoka Zanzibar uliojitokeza unaoegemea sera za vyama na itikadi za kisiasa.

Baraza la Wazee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar tayari limetoa tamko la kupoteza imani na Spika Kificho kwa kitendo chake cha kuandika waraka unaopendekeza Zanzibar na Tanganyika zipate mamlaka huru za dola, bila ya kuwepo kwa mapatano na uamuzi wa pamoja wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Wazee hao wamesema hiyo ni aina ya hujuma na usaliti kinyume na utaratibu wa hadhi ya Spika aliyekabidhiwa dhamana hiyo nyeti katika mgawanyo wa madaraka chini ya mihimili mitatu.

Kwa upande wake Spika Kificho amekiri kuwa hakuna uamuzi wa pamoja uliofikiwa na Baraza lake katika kupendekeza aina ya muundo wa mfumo wa Muungano, kutokana na pande mbili za kisiasa za CCM na CUF kila moja kuwa na msimamo wake kisera.

Kificho ameendelea kusisitiza kuwa waraka aliousaini na kuuwasilisha mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya Jaji Joseph Warioba, ulijadiliwa na kuridhiwa na kamati ya uongozi jambo ambalo limekanushwa na Mnadhimu wa Baraza hilo upande wa CCM, Salmin Awadh Salmin ambaye alisema waliotoa mapendekezo hayo ni kigenge cha watu watano kinyume na utaratibu wa pamoja wa kamati ya uongozi yenye wajumbe 15.

Malaysia:Juhudi za kuisaka ndege zashika kasi

Marekani pia imejiunga na juhudi za kuitafuta Ndege ya Malaysia

Wiki moja tangu ndege ya Malaysia iliyokuwa imewabeba abiria 239 kutoweka, juhudi za kimataifa kuisaka ndege hiyo bado zinaendelea.

Mataifa kumi na mbili sasa yamejiunga pamoja kuisaidia serikali ya Malaysia na msako huo, juhudi zenyewe zikijikita zaidi Magharibi mwa rasi ya Malaysia.

Marekani imesema kuwa inatuma manowari zake za kivita, pamoja na ndege maalum ya uchunguzi katika maeneo ya Bengal, Bahari ya Andaman na sehemu za Bahari hindi.

Mnamo Ijumaa taarifa ziliibuka kuwa ndege hiyo ilituma mawasiliano katika kituo cha trafiki ya ndege kwa karibu saa tano baada ya taarifa ya kupotea kwake kutolewa.

Taarifa zinasema kuwa mawasiliano hayo yanaweza kusaidia katika kujua iliko ndege hiyo na ndio maana Marekani ikaamua kutuma meli zake za kivita katika Bahari Hindi.

West Brom yamtimua Nicolas Anelka


Nicolas Anelka

Mchezaji wa klabu ya soka ya West Brom, Nicolas Anelka amefutwa kazi kwa kosa la utovu wa nidhamu.

Klabu hiyo iliamua kuchukua hatua hiyo baada ya Anelka kutangaza kupitia mtandao wa kijamii kuwa anaacha kazi.

Anelka alisema kuwa anaondoka katika klabu hiyo baada ya kukosa kutatua tofauti zilizopo kati yake na Albion kuhusu ishara yake yenye utata ambayo inasemekana kuwa ya kibaguzi dhidi ya wayahudi.

Mshambuluaji huyo mwenye umri wa miaka 35, alipigwa marufuku kutocheza mechi tano na kutozwa faini ya pauni 80,000 na shirikisho la soka Uingereza ,kwa kufanya ishara hiyo, baada ya kuingiza bao dhidi ya klabu ya West Ham mwezi Disemba.

West Brom imechukua hatua ya kumfuta kazi Anelka kutokana na ishara hiyo na pia kwa sababu ya matamshi yake kwenye mtandao wa kijamii.

Ishara hii inapigiwa debe na msanii wa Ufaransa Diedonne M'bala M'bala

Awali aliachishwa kazi mwa muda na Albion, wakati klabu hiyo ilipokuwa inafanya uchunguzi wake binafsi.

Mapema siku ya Ijumaa, Anelka alitangaza kwenye mitandao ya kijamii kuwa anaondoka katika klabu hiyo.

Aliandika: "kufuatia mazungumzo kati yangu na maafisa wa klabu, kuna masharti kadhaa ambayo wamenipa kabla ya kujiunga tena na klabu hiyo, Masharti ambayo siwezi kuyakubali.''

Hata hivyo klabu ilisema kuwa masharti yaliyotolewa kwa Anelka ni pamoja na kumtaka awaombe msahama mashabiki , wadhamini na jamii kwa ujumla kwa athari iliyotokana na ishara yake aliyoifanya Disemba tarehe 28 na pili akubali kutozwa faini.

Jasusi wa zamani Rwanda jela miaka 25

Simbikangwa alikuwa mkuu wa ujasusi wa Rwanda wakati wa mauaji ya Kimbari

Mahakama nchini Ufaransa, imemhukumu kifungo cha miaka 25 jela jasusi mkuu za zamani wa Rwanda Pascal Simbikangwa kwa kuhusika na mauaji ya kimbari mwaka 1994.

Simbikangwa alipatikana na hatia ya kuhusika na mauaji hayo na kutenda uhalifu dhidi ya binadamu.

Alikabiliwa na makosa ya kuchochea , kupanga na kusaidia katika juhudi za mauaji ya watutsi hasa kwa kuwapa silaha wapiganaji wa kihutu waliokuwa wanalinda vizuizi vya barabarani na kuwaua wanaume wa kabila la Tutsi, wanawake na watoto.

Simbikangwa alikanusha madai hayo.

Haijuikani kama mawakili wa Simbikangwa watakata rufaa dhidi ya uamuzi huo.

Simbikangwa,mwenye umri wa miaka 54, anatumia viti vya magurudumu baada ya kuhusika na ajali mwaka 2008 alipokuwa anaishi katika kisiwa cha Mayotte.

Maelfu ya watutsi na wahutu waliuawa mwaka 1994

Ni mwanamume wa kwanza kuhukumiwa nchini Ufaransa kuhusiana na mauaji ya Kimbari Rwanda miaka 20 iliyopita.

Upande wa mashitaka uliitaka mahakama kumfunga jela maisha Simbikangwa, baada ya kumtaja kuwa mtu mkatili na ambaye anaweza kufanya mambo mabaya zaidi ya aliyofanya.

Mawakili wake hata hivyo walisema kuwa kesi hiyo ilishinikizwa zaidi kisiasa na kuwataja mashahidi kama wasioweza kuaminika na ambao walikuwa na chuki wakati wakitoa ushahidi wao.

Takriban watu 800,000 wengi wao wa kabila la Tutsi , waliuawa katika kipindi cha siku miamoja.

Kesi ya kukutwa na sare za polisi yaahirishwa


Dar es Salaam. Kesi inayomkabili James Hassani (45),anayekabiliwa na mashtaka ya kujifanya askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani na kukutwa na sare za jeshi hilo imeahirishwa hadi Machi 26 mwaka huu.

Kesi hiyo imeahirishwa baada ya mshtakiwa kuugua ugonjwa wa mafindofindo na kudai kuwa hataweza kufika mahakamani. Hii ni mara ya tatu kwa kesi hiyo kuahirishwa baada ya Februari 26 mwaka huu Mahakama kuiahirisha kesi hiyo baada ya shahidi wa pili katika kesi hiyo kuwa mgonjwa.

Hakimu Janeth Kinyage aliahirisha kesi hiyo hadi Machi 26, mwaka huu itakapoendelea kusikilizwa na mshtakiwa alirudishwa rumande. Kesi hiyo ipo katika hatua ya kutoa ushahidi na tayari shahidi wa kwanza ameshatoa ushahidi wake.

Hata hivyo, Mahakama ya Wilaya ya Ilala ilimfungia dhamana Hassani, baada ya kubaini kuwa mshtakiwa huyo alikuwa na kesi nyingine iliyosababisha kutoroka katika Gereza la Msanga lililopo mkoani Dodoma alipokuwa akitumikia kifungo cha miaka 30 jela.

CCM, Chadema kufunga kampeni za ubunge kesho


Iringa. Kampeni za uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kalenga zinatarajiwa kufungwa kesho huku CCM ikitarajia kumaliza kampeni zake katika ngome ya Chadema iliyopo eneo la Kidamali.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana anatarajia kuongoza ufungaji huo huku Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akitaraji kuongoza maandamano ya kufunga mkutano wa kampeni hizo.

Katibu wa CCM mkoani hapa, Hassan Mtenga alisema Katibu Mwenezi wa CCM Mkoa, Dk Yahya Msigwa, viongozi wa Jumuiya ya Wazazi Taifa, Khamis Dadi (Katibu) na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Abdallah Bulembo ni miongoni mwa watakashiriki kufunga kampeni hizo.

Timu ya kampeni ya CCM inaratibiwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Phillip Mangula ambaye ameweka kambi katika Kata ya Ifunda, inayoaminika kuwa ni moja ya ngome ya Chadema .

Wengine ni Katibu wa CCM Mkoa wa Mtwara, Shaibu Akwilombe makatibu wa CCM wa wilaya zaidi ya 10 ambao wameweka kambi kwenye kata 13 na vijiji vilivyopo jimboni humo.

Mkutano wa Chadema unatarajiwa kufanyika katika Kata ya Ifunda, Jimbo la Kalenga kwa mwenyekiti kuongoza maandamano pamoja na jopo la wabunge 40 wa chama hicho. Uchaguzi mdogo wa Kalenga unatarajiwa kufanyika Machi 16,baada ya kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Marehemu Dk William Mgimwa.

Wakati huo huo, Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva amevitaka vyama vya ushirika kuwarudishia shahada zao wakazi wa Kalenga ili waweze kupiga kura.

Vita dhidi ya Al Shabaab vinaathiri raia-UN

Mwanajeshi wa serikali akishika doria mjini Mogadishu

Umoja wa mataifa umesema kuwa mashambulizi makubwa ya kijeshi yaliyofanywa nchini Somalia na Wanajeshi wa Umoja wa Afrika, AMISOM, dhidi ya makundi ya wapiganaji wa Kiislamu, yanaweza kuwaathiri watu milioni tatu katika maeneo ya katikati na Kusini mwa nchi hiyo.

Mashambulizi hayo yanayowahusisha maelfu ya wanajeshi wa AU, yaliyoanzishwa juma lililopita na sasa yamesambaa hadi katika maeneo ya jangwa na milima.

Umoja wa Mataifa umeongezeka kusema kuwa umo katika hali ngumu zaidi Nchini Somalia.

Kwa sasa inaisaidia Umoja wa Afrika kwa hali na mali pamoja na vifaa vinavyohitajika kupambana na wapiganaji wa Kiislamu, na pia misaada ya kibinadam.

Inaunga mkono Jeshi moja kwa moja katika kutekeleza mashambulio makali dhidi ya makundi ya wapiganaji wa kiislamu yaliyo katika vuguvugu la Al-Shaabab.

Lakini kitengo kingine cha Umoja wa Mataifa kinachoshughulikia mashirika ya utoaji misaada ya kibinadamu, sasa yanatahadharisha kuhusiana na makali yanayotekelezwa na wanajeshi hao dhidi ya wananchi.

Shambulio mjini Mogadishu

Mashirika hayo pia yanasema wapiganaji wa Kiislamu kwa upande wao wanawahamasisha wananchi dhidi ya operesheni hiyo ya kijeshi inayojumuisha wanajeshi kutoka mataifa wanachama pamoja na wanajeshi wa serikali ya Somalia.

Siku za kwanza kwanza za operesheni hiyo kali, hasa katika maeneo ya vijijini, haikuwa rahisi kwa wafanyi kazi wa Umoja wa Mataifa kujua kilichokuwa kikiendelea.

Lakini tayari maelfu ya watu wanaingia katika mji wa Baidoa ulioko katikati mwa Somalia unadhibitiwa kwa sasa na Wanajeshi wa umoja wa mataifa kukimbia mapigano au kujaribu kupanga mashambulizi.

Bensouda kukata rufaa kesi ya Katanga

Fatou Bensouda

Mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya Kimataifa ya uhalifu ICC, Fatou Bensouda amesema huenda akakata rufaa hukumu iliyotolewa kwa mbabe wa zamani wa kivita nchini Congo Germain Katanga.

Katanga alipatikana na hatia nne za uhalifu wa kivita na hatia moja ya uhalifu dhidi ya binadamu, lakini akaondolea makosa kuhusu ubakaji.

Wapiganaji wake walishutumiwa kuwabaka wanawake na kuwateka huku wakiwatumia kama watumwa wa ngono.

Makundi ya wanawake nchini Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Congo yameelezea hasira na masikitiko yao kutokana na hatua ya mahakama hiyo ya ICC ya kumuondolea Bwana Gatanga makosa hayo.

Wakati wa ziara yake katika mji mkuu wa DRC, Kinshasa, Bensouda alisema kuwa huenda akakata rufaa dhidi ya uamuzi huo wa mahakama.

''Majaji hawakumuhumu kuhusiana na mashtaka ya unyanyazaji wa kimapenzi, mashtaka ambayo tulikuwa tumemshtaki nayo, pamoja na ile ya kuwasajili watoto jeshini'' Alisema Bensouda.

Bensouda, amesema kuwa wanachunguza hukumu hiyo kwa undani na kuchunguza ikiwa kuna dosari kadhaa za kisheria ambazo wanaweza kutumia kukata rufaa.

''Majaji kwa hekima zao walihisi kuwa bwana Katanga hakuhusika moja kwa moja na mashtaka hayo. Nadhani waadhiriwa wanafurahia kuwa ofisi yake inafuatilia suala hili, ili kuhakikisha kuwa mashtaka mazito kama hayo yanachunguzwa.'' Aliongeza Bensouda.

Kuhusiana na kesi inayomkabili rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, makamu wake William Ruto na mwandishi wa habari Joshua arap Sang, Bensouda alisema kuwa ''Nimeonyesha wazi kuambatana na ombi niliowasilisha mbele ya mahakama, kuhusiana na changa moto tunazopata, baada ya mashahidi wakuu kujiondoa kwa sababu kadhaa''.

Bensouda amesema kuwa itakuwa vigumu sana kwa ofisi yake kuendelea na kesi hizo kama ilvyopangwa baada ya mashahidi wakuu kujiondoa.

''Nimewafahamisha majaji kuwa tulikuwa na mashahidi kadhaa wakuu ambao walikuwa tayari kutoa ushahidi kuhusiana na matukio muhimu nchini Kenya, lakini wameomba kujiondoa kutoka kwa kesi hiyo.

Na kama unavyofahamu mashtaka haya pia ni mazito, na kabla ya kwenda mahakamani mtu anapaswa kuwa na uhakika wa kuwa na ushahidi ambao utakidhi mahitaji muhimu ili kuhakisha kuwa washukiwa wanahumiwa.'' Alisema Bensouda.

Zeidan akanusha kufutwa kazi


Aliyekuwa Waziri mkuu wa Libya Akihutubia Wanahabari

Aliyekuwa waziri mkuu wa Libya, Ali Zeidan, amepuuzilia mbali kura ya kutokuwa na imani naye iliyotangazwa na Bunge la taifa hilo mapema juma hili iliyopeleekea kufutwa kwake.

Ameiambia shirika la habari la Channel France 24 kuwa kura hiyo ya kutokuwa na imani naye illikuwa imejengwa kwa misingi ya uwongo huku pia akikanusha madai ya ufisadi dhidi ya serikali yake.

Ali Zeidan aliondolewa Ofisini mnamo siku ya Jumanne baada ya meli ya mafuta kutoka bandari inayodhibitiwa na waasi kufaulu kuvunja nanga ya wanajeshi wa wanamaji wa Libya kuingia bahari kuu na kutoroka.

Bwana Zeidan alifaullu kuondoka nchi hiyo licha ya kupingwa marufuku ya kutosafiri nje ya taifa.

T.B Jushua adai ndege ya Malaysia iliyopotea kimaajabu imezama kwenye tope baharini

T.B Jushua

Wakati ambapo dunia ikiweka jitihada zote kuisaka ndege ya shirika la Malaysia aina ya Boing 777 iliyopotea ikiwa na watu 239 wakati ikielekea Beijing, mhubiri maarufu wa Nigeria T.B Joshua ametoa utabiri kuwa ndege hiyo imezama baharini!

Jumapili iliyopita, T.B Joshua ameeleza kanisani kwake (SCOAN) kuwa ndege hiyo ilianguka na imezama ndani kabisa kwenye tope za bahari na kwamba hivi karibuni vipande vya ndege hiyo vitaanza kuonekana vikielea.

“Ndege hiyo iko ndani kabisa ya bahari. Baadhi ya vipande vitaanza kuonekana vikielea baharini muda wowote kuanzia sasa." Alisema T.B Joshua.

“Roho zao zipumzike kwa Amani. Tunaomba bwana azipe familia zao na wapendwa wao nguvu/uimara kushinda upotevu huu. Maombi yetu na upendo viko nao, nchi ya Malaysia na nchi nyingine ambazo zilikuwa na abiria katika ndege hiyo.” Alisema T.B Joshua kwa mujibu wa mtandao wa Nigeria wa Informationnng.

Hayo ni mambo ya imani!

Wakati dunia ikiwa bado haijafahamu ilipo ndege hiyo, wizara ya mambo ya nje ya China imeitaka Malaysia kuharakisha juhudi zake za kuitafuta ndege hiyo iliyokuwa na abiria 154 raia wa China kati ya abiria 239 waliokuwa katika ndege hiyo.

Ndege hiyo ilipotea mwishoni mwa juma na kumekuwa na mashaka kwamba huenda ni bomu au utekaji nyara unaweza kuwa uliiangusha ndege hiyo.

Waziri mkuu wa Libya azuiwa kusafiri

ali zeidan

Kiongozi wa mashtaka Nchini Libya Abdel-al-Qader Radwan amemzuia Waziri mkuu wa taifa hilo aliyevuliwa madaraka, Ali Zeidan, kusafiri nje ya taifa hilo hadi pale uchunguzi dhidi yake utakapokamilika.

Anatuhumiwa kwa madai ya ubathirifu wa pesa za umma.

Bwana Zeidan amesimamishwa kazi mapema siku ya Jumanne na Bunge la taifa hilo, baada ya Wabunge kudai kuwa meli ya mzigo ya Korea Kaskazini iliyokuwa imezuiliwa baada ya kunaswa ikibeba mafuta ghafi toka bandari moja linalokaliwa na waasi huko Libya, ilivunja nanga na kusafiri baharini.

Kura ya kutokuwa na imani na Bwana Zeidan iliitishwa baada ya meli hiyo iliyokuwa na bendera ya Korea Kaskazini kuabiri na kufikia maji makuu ya mipaka ya kimataifa baharini.

Mafuta hayo yalikuwa yamenunuliwa kutoka kwa waasi wanaodhibiti bandari ya Al- Sidra.

Wabunge hawana imani na Waziri Mkuu

Bunge la Libya limemuachisha kazi Waziri huyo mkuu, baada ya kupitisha agizo la kutokuwa na imani naye.

Hilo limeafikiwa baada ya meli ya Korea Kaskazini kuingia katika bandari ya taifa hilo na kuondoka na mafuta ghafi bila idhini ya serikali.

Makundi ya wapiganaji yamekuwa yakidhibiti baadhi ya bandari ya taifa hilo mashariki mwa taifa, tangu Julai mwaka jana na kuuza mafuta nje ya taifa.

Mwaandishi wa BBC Rana Jawad anatuarifu kutoka Tripoli.

Meli ya Mafuta iliyonaswa na wanajeshi ikisafirisha mafuta ghafi kisiri

Bunge la Libya limekuwa likijadiliana namna ya kumtimua Waziri mkuu Ali Zeidan kwa miezi kadhaa sasa.

Wabunge 200 wa taifa hilo walipiga kura na kupata maoni 124 iliyotosha kumuondoa madarakani.

Serikali ya mpito

Kiwanda cha mafuta nchini Libya

Waziri wa sasa wa ulinzi Abdullah Al-Thani amechukua mahala pake kama kama kaimu waziri mkuu.

Anatarajiwa kuhudumu kwa kipindi cha majuma mawili, kuruhusu bunge kukubaliana kumteuwa mridhi wa wadhifa huo.

Chama cha Libya National Congress, tume ya kwanza ya uchaguzi ndio yenye majukumu ya kumteuwa waziri mkuu mpya.

Lakini shinikizo kali limekuwepo Nchini humo la kutaka Bunge livunjwe.

Bwana Zeidan amekuwa akilaumu baadhi ya wanasiasa katika tume hiyo, hasa kutoka ndani ya vyama vya kiislamu ya kutaka kumtimua toka uongozini.

Hatua hiyo ya hivi punde inatazamiwa kuibua maswala mbalimbali ya udhibiti wa uongozi Nchini Libya, inapojikakamua kutafuta uungwaji mkono kutoka pembe zote za Nchi.

'Oscar Pistorius alipenda sana Bunduki'


Pistorius akiwa mahakamani

Katika ushahidi unaoendelea kutolewa dhidi ya mwanariadha mlemavu wa Afrika Kusini, Oscar Pistorius, rafiki ya mwanariadha huyo, ameambia mahakama kuwa Pistorius alipenda sana bunduki

Darren Fresco, alisema kuwa alikuwa naye mara mbili alipokuwa na bunduki aliyoiofyatua katika sehemu ya umma.

Bwana Pistorius wakati mmoja alifyatua bunduki yake akiwa ndani ya mkahawa , ingawa yeye ndiye aliyelaumiwa kwa hilo,alisema bwana Fresco said.

Mwanariadha huyo amekanusha madai ya kumuua mpenzi wake kwa maksudi, akisema kuwa alidhania kuwa ni mwizi aliyevamia nyumba yake.

Bwana Fresco alisema kuwa katika tukio lengine, alikuwa anaendeshagari lake wakati ambapo Pistorius alipofyatua tena bunduki yake baada ya polisi kumzuia kuendesha gari lake kwa kasi.

Alisema kuwa Pistorius alikasirika baada ya polisi kuchukua dunduki yake iliyokuwa kwenye kiti cha nyuma ya gari lake na kumwambia: '' hauruhusi kugusa bunduki ya mtu mwingine, ikiwa chochote kitatokea atakuwa wa kulaumiwa.''

Mwandishi wa BBC nchini humo, Pumza Fihlani anasema kuwa Pistotius katika kikao cha Jumanne alikuwa mtulivu ikilinganishwa na Jumatatu.

Aliketi akiwa kimya na kuandika baadhi ya maneno yaliyokuwa yanasemwa.

Ushahidi wa Fresco, ulitoa taswira ya mchezaji huyo alivyopenda maisha ya kifahari akiwa na rafiki zake. Alipenda magari, wanawake warembo , bunduki na kwamba aliwashukia sana polisi.

Aliyekuwa mpenzi wa Oscar pia alitoa ushahidi sawana huo mahakamani, wiki ya kwanza ya kuzikilizwa kwa kesi hiyo.