Jasusi wa zamani Rwanda jela miaka 25

Simbikangwa alikuwa mkuu wa ujasusi wa Rwanda wakati wa mauaji ya Kimbari

Mahakama nchini Ufaransa, imemhukumu kifungo cha miaka 25 jela jasusi mkuu za zamani wa Rwanda Pascal Simbikangwa kwa kuhusika na mauaji ya kimbari mwaka 1994.

Simbikangwa alipatikana na hatia ya kuhusika na mauaji hayo na kutenda uhalifu dhidi ya binadamu.

Alikabiliwa na makosa ya kuchochea , kupanga na kusaidia katika juhudi za mauaji ya watutsi hasa kwa kuwapa silaha wapiganaji wa kihutu waliokuwa wanalinda vizuizi vya barabarani na kuwaua wanaume wa kabila la Tutsi, wanawake na watoto.

Simbikangwa alikanusha madai hayo.

Haijuikani kama mawakili wa Simbikangwa watakata rufaa dhidi ya uamuzi huo.

Simbikangwa,mwenye umri wa miaka 54, anatumia viti vya magurudumu baada ya kuhusika na ajali mwaka 2008 alipokuwa anaishi katika kisiwa cha Mayotte.

Maelfu ya watutsi na wahutu waliuawa mwaka 1994

Ni mwanamume wa kwanza kuhukumiwa nchini Ufaransa kuhusiana na mauaji ya Kimbari Rwanda miaka 20 iliyopita.

Upande wa mashitaka uliitaka mahakama kumfunga jela maisha Simbikangwa, baada ya kumtaja kuwa mtu mkatili na ambaye anaweza kufanya mambo mabaya zaidi ya aliyofanya.

Mawakili wake hata hivyo walisema kuwa kesi hiyo ilishinikizwa zaidi kisiasa na kuwataja mashahidi kama wasioweza kuaminika na ambao walikuwa na chuki wakati wakitoa ushahidi wao.

Takriban watu 800,000 wengi wao wa kabila la Tutsi , waliuawa katika kipindi cha siku miamoja.

No comments:

Post a Comment