Balozi Radhia Msuya
Tanzania yajitosa kumsaidia Ruto
Serikali ya Tanzania, imeiomba Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kuruhusu Makamu wa Rais wa Kenya, William Ruto kutohudhuria baadhi ya mashauri ya kesi yake ili kuweza kutimiza majukumu mengine ya kiserikali.
Mwanasheria Mkuu wa Tanzania, Jaji Fredrick Mwita aliandika barua kwenda ICC Jumatatu wiki hii akitetea hoja ya Ruto kutaka asihudhurie baadhi ya vikao vya kesi hiyo.
Katika barua yake, Jaji Werema alisema kuruhusu Ruto kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi kutaimarisha ushirikiano baina ya ICC na washirika.
Hata hivyo, maombi hayo yanayotaka Ruto kuruhusiwa kutohudhuria kesi hiyo binafsi yamesimamishwa baada ya mwendesha mashtaka wa ICC, Fatou Bensouda kuyawekea pingamizi na sasa yanasubiri uamuzi wa majaji.
Hii ni mara ya pili kwa Tanzania, kuwasiliana na ICC kwani iliwahi kuwasilisha ombi la kutaka kesi hiyo ya kina Ruto isikilizwe Tanzania au Kenya.
Hata hivyo, mpango huo ulikwama baada ya majaji kuupinga kwa kura za hapana.
Mwandishi Sang ajitetea
Mwandishi wa habari wa kituo cha KASS FM Joshua Arap Sang, amekamilisha ungwe ya kwanza ya utetezi wake kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) na kueleza kuwa hakuhusika kwa namna yoyote kuchochea machafuko yaliyojiri baada ya uchaguzi nchini Kenya.
Sang aliwasilisha utetezi wake katika hali ya kujiamini huku akionyesha sura yenye matumaini na kuiambia mahakama kuwa, kesi inayomkabili imetengenezwa ili kukatiza ndoto yake ya kuwa mtangazaji bora duniani .
Mwandishi huyo ambaye anatetewa na mawakili wanaoongozwa na Wakili Katwa Kigen, alipangua hoja zilizowasilisha na upande wa mashtaka kwa kutumia historia ya maisha yake aliyoyaelezea kuwa ni ya kumcha Mungu na uadilifu.
Kama ilivyo kwa washtakiwa wengine, Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto, Sang anadaiwa kuratibu na kupanga mashambulizi na kusababisha zaidi ya watu elfu moja kupoteza maisha.
Pia anadaiwa kuendesha kampeni ya uchochezi kupitia vipindi mbalimbali vya redio baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu wa 2007.
Mbele ya jopo la majaji wanaosikiliza kesi hiyo, Sang alisema historia ya maisha yake inaeleza vyema namna alivyokuwa msaada kwa jamii, ikiwamo kushiriki kikamilifu shughuli za kanisa hivyo kutuhumiwa kuwa alihusika kwenye mauwaji ni dhihaka kubwa kwake.
“Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu ambaye kwake yeye nimepata nguvu na kusimama hapa. Nafahamu fika ipo siku mahakama hii itasimama katika haki na kuniachia huru. Itamwachia huru mwandishi wa habari.
“Lakini pia napenda niiarifu mahakama hii kuwa mimi ni kiongozi wa kwaya tena nategemewa sana na wenzangu, sasa kuambiwa kuwa nimeratibu mauaji ya raia ni jambo linalonisononesha sana tena limenivuruga mno,” alieleza Sang.
Katika kile kilichoonekana kama njia ya kuupa nguvu utetezi wake, Sang mbali ya kuelezea uzoefu wa kazi yake lakini alirudia mara kadhaa kutamka maneno yaliyotafsiri hisia zake dhidi ya kesi hii.
“Kusema kweli haya mashtaka yamenisononesha na kunivuruga. Mimi ni mzazi na pia ni mume mwema, itakuwaje sasa nithubutu kufanya jambo hili la kuua wenzangu, haiwezekani. Nimesikitika na kusononeka sana”.
Uzoefu wake
Baadaye aligeukia kipengele kilichohusu uzoefu wa kazi yake ambapo alitetea utendaji wake akisema; wakati wote alikuwa akifanya kazi kwa kuzingatia miiko na madili.
“Mimi ni mtangazaji wa siku nyingi tena nimefanya kazi hii katika vituo zaidi ya vitatu ambavyo vyote ni vya kidini, sasa huko kote nisifanye hilo la kuchochea mauaji nije kulifanya hapa Kass FM. Hiyo siyo kweli kabisa na hii kesi imeletwa kwa ajili kunivurugia tu safari yangu ya kuendelea kuwa mtangazaji.
Aliongeza: “Potelea mbali najua Mungu yupo na ataendelea kunipigania. Natambua kuwa mimi nilizaliwa kuwa mtangazaji na hadi leo nitabakia kuwa hivyo.”alisema
Aliiambia mahakama hiyo kuwa kazi ya utangazaji alianza kuipenda alipokuwa kijana mdogo na wakati fulani alilazimika kufuatilia matangazao yaliyokuwa yakirushwa na kituo cha BBC kwa ajili ya kujifunza na kupata taarifa za dunia.
“Waheshimiwa majaji mimi ni msikilizaji mzuri wa redio na kituo nilichokuwa nikikifanyia kazi Kass FM kinasikika kimataifa, hata hapa Netherland mimi nasikiliza redio hii, hivyo nina ufahamu wa kutosha wa kazi hii.
Napenda tu niseme haya mashtaka hayana ukweli wowote kabisa,”alisema.
Kuhusu vipindi alivyokuwa akiviendesha ambavyo vinadaiwa kupendelea kambi ya ODM, Sang alipuuza hoja hiyo kwa kueleza kuwa, wakati wa kampeni vyama vya siasa ndivyo vinavyolipia matangazo kwa ajili ya kutangaza sera zao.
“Pale Kass FM mimi ni mtu mdogo kabisa, sina uwezo wa kuamua jambo lolote lile mbali ya kufuata utaratibu uliowekwa na mmiliki wa kituo, lakini pia kusema mimi nilipendelea kambi ya ODM kwa kuwapa vipindi vingi hili siyo kweli kabisa, lazima tujue kwamba wakati wa kampeni vituo vingi huuza muda kwa wanasiasa ili watangaze sera zao ndivyo ilivyokuwa kwetu,” alieleza.
Sang pia alikanusha tuhuma za kuendesha vipindi vya redio vinavyodaiwa kurushwa kwa kipindi cha siku tatu kuanzia mwanzoni mwa Januari, 2008 vilivyokuwa vikiwahimiza wananchi wa kabila la Kilinjini kuanzisha machafuko.
Wanusurika kufa kwa pombe
Iringa. Zaidi ya watu 19 katika Kijiji cha Imega, katika Wilaya ya Kilolo, wamenusurika kufa baada ya kunywa pombe ya kienyeji inayodhaniwa kuwa na sumu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi alisema tukio hilo lilitokea juzi wakati watu hao walipokwenda kuhudhuria sherehe iliyoandaliwa na mzee mmoja. Kwa mujibu wa kamanda huyo, sherehe hizo zilikuwa ni za kumuaga binti yake aliyekuwa akiolewa.
Alisema baada ya kazi hiyo, watu hao walianza kunywa pombe ya kienyeji na ilipofika jioni watu 19 walipatwa na ugonjwa wa tumbo. Kamanda huyo alisema baadaye watu hao walipelekwa katika Zahanati ya kijiji hicho kwa matibabu.
Alisema wakati wakiendelea kupata matibabu ,mmoja wa watu hao, alizidiwa na kukimbizwa katika Hosptali ya Itunda kwa matibabu zaidi. Alisema uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa huenda pombe walioitumia ilikuwa na sumu.
“Pombe hiyo inatokana na mahindi na inasemakana mahindi hayo yalikuwa na dawa. Tunafanya uchunguzi,” alisema Mungi.
WAHAMIAJI HARAMU 133 MBALONI JIJINI DAR ES SALAAM
Jijini Dar es Salaam hekaheka za wahamiaji
haramu zimeendelea, baada ya watu 133 kutoka mataifa mbalimbali kutiwa mbaroni.
Hatua hiyo, inatokana na msako mkali uliopewa
jina la ‘Endelevu’ unaoendelea katika maeneo mbalimbali.
Akizungumza na MTANZANIA ofisini kwake mwishoni
mwa wiki iliyopita, Naibu Kamishna wa Idara ya Uhamiaji na Msemaji Mkuu, Abbas
Irovya, alisema msako ambao ulianza mwanzoni mwa mwezi huu umekuwa na
mafanikio.
Alizitaja nchi wanazotoka na idadi yao kwenye
mabano kuwa ni Burundi (41), Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (30), Kenya (11),
Uganda (6), Pakistan (3), Somalia (7), Nigeria (4) na Cameroon (1).
Nchi nyingine ni Afrika Kusini (1), Malawi (11),
Rwanda (44) na Msumbuji (7).
Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA mjini Dar es
Salaam katika maeneo ya Mwananyamala, Mikocheni, Tegeta, Msasani, Sinza na
Temeke umebaini kuwapo na idadi kubwa ya wahamiaji haramu.
Juzi katika eneo la Mikocheni B, MTANZANIA
ilishuhudia raia kadhaa wa Malawi wakiwa wamekusanyika kwa ajili ya kufanya
kikao cha dharura, kwa ajili ya kuchangishana fedha waondoke nchini.
Mmoja wa raia hao (jina tunalo), alisema hivi
sasa hawaishi kwa amani hata kidogo kutokana na jamaa zao wengi kukimbia makazi
na kutelekeza familia zao.
“Tunaishi maisha ya shaka mno, naona ni bora
nitafute mtu nimuuzie vyombo vyangu ili nirudi nyumbani haraka, maisha Malawi
ni magumu mno tofauti na Tanzania,” alisema
Chanzo: Mtanzania
Tanzania kuwa ya viwanda
Dar es Salaam. Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda, amesema Tanzania itakuwa nchi ya viwanda vya kati ifikapo mwaka 2025 ikiwa wawekezaji watajengewa mazingira mazuri ya kuwekeza.
Akizungumza katika uzinduzi wa kiwanda cha kuzalisha wa ‘gypsum’ cha Kampuni ya Sunshine ya China kilichopo katika Kata ya Visiga, Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani juzi, Dk Kigoda alisema kuwa sekta ya viwanda inakuwa kwa kasi nchini.
“Kiwanda hiki ni muhimu kwa uchumi wa kata ya Visiga na taifa kwa jumla. Uchumi wetu hauwezi kutegemea kilimo peke yake, tunataka nchi yetu iwe ya viwanda vya kati ifikapo mwaka 2025,” alisema Dk Kigoda.
Dk Kigoda alisema kwa sasa sekta ya viwanda inachangia pato la Taifa kwa asilimia 30, hivyo ukuaji wa viwanda utakuza pato hilo ikiwa wawekezaji watajengewa mazingira mazuri.
“Nimeambiwa kuwa tangu uamuzi wa kulifanya eneo hilo la Visiga kuwa la viwanda tayari kuna viwanda vitano vya chuma, kusafisha mafuta, kutengeneza nondo na hiki cha gypsum. Sekta ya viwanda inachangia pato la Taifa kwa asilimia 30 na asilimia 40 ya ajira,’’ alisema.
hia Sunshine kuwa soko la bidhaa zao lipo kubwa,” alisema Dk Kigoda.
Alisema uwekezaji wa kampuni hiyo ambayo pia ina kiwanda cha baruti kilichopo wilayani Kibaha na madini wilayani Chunya Mkoa wa Mbeya, utazingatia wajibu kwa jamii (corporate social responsibility)
Licha ya kuipongeza kampuni hiyo, Dk Kigoda aliwataka wawekezaji hao katika sekta ya viwanda kuzingatia ubora wa bidhaa wanazozalisha ili kukuza uchumi wa nchi.
Naye Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hun Xue Hui, alisema kampuni hiyo ambayo ni tanzu ya kampuni za Sunshine ya China itatoa ajira rasmi kwa watu 60 na ajira nyingine zisizo rasmi na itakuwa ikizalisha gypsum tani 700,000 kwa mwaka.
Aliongeza kuwa, wananchi wanaozunguka kiwanda hicho watafaidika kwa kupewa kipaumbele cha ajira na huduma za jamii.
Kwa upande wake mwakilishi wa Ubalozi wa China nchini anayeshughulikia masuala ya siasa, Li Xuhang, alisema uwekezaji wa viwanda unaendeleza uhusiano kati ya Tanzania na China uliodumu tangu wakati wa uhuru.
“Mmefanya vizuri kuwekeza katika eneo hili kwani wananchi nao watafaidika. Tanzania na China zimekuwa marafiki kwa zaidi ya miaka 50, hivyo kwa niaba ya Balozi wa China nchini tunawaunga mkono,” alisema Xuhang.
Subscribe to:
Posts (Atom)