Warioba: Tunahitaji rais mzalendo


Jaji Joseph Warioba 


Aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, Jaji Joseph Warioba, ametaja sifa za rais ajaye kuwa ni uzalendo, uadilifu na dira katika kuliongoza taifa.

Jaji Warioba alisema hayo juzi, katika Kipindi cha Dakika 45 kilichorushwa hewani na ITV.

“Rais anapaswa pia kujua matatizo ya Watanzania, awe mzalendo, mwadilifu na aone mbali. Anapaswa pia kujua  atafanya nini kuboresha maisha ya wananchi kupitia sekta za afya na uchumi,” alisema.

Kwa kauli hiyo, Jaji Warioba anaungana na viongozi wengine kadhaa waliowahi kuzungumzia sifa za rais ajaye, akiwamo aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa, Dk Hassy Kitine; Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye; Mwanasiasa mkongwe, Cleopa Msuya; Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba;  na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Dk Emmanuel Nchimbi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, viongozi hao walitaja sifa hizo za rais ajaye kuwa ni uadilifu, busara, uzalendo, uwezo wa kufanya uamuzi na kuyasimamia, weledi wa masuala ya maendeleo, kutokuwa na makundi, kuwa na nguvu ya mwili na akili na uwezo wa kusimamia Katiba na sheria za nchi.

Walisema yeyote asiyekuwa na sifa hizo, hafai kuwa rais na kuwaongoza Watanzania.

Dk Kitine: Urais siyo lelemama

“Mtu anayetangaza (mwenyewe) kuwa anataka kuwa rais anakuwa hajui anachokisema..., anakuwa hajui matatizo ya urais. Mtu asiyejua matatizo ya urais anaweza kujisemea tu kwa sababu haelewi urais maana yake ni nini,” alisema aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa na Waziri wa kwanza wa Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Dk Hassy Kitine.

Kitine alisema hayo Septemba 9 mwaka jana. Alisisitiza, “Mtu anayejua maana na changamoto za urais hawezi kutangaza anautaka urais. Ataogopa kwa sababu ya changamoto (nyingi) za urais…, kwa hiyo hawezi kujitangazia ovyo kuutaka.”

 Kwa mujibu wa Dk Kitine anayetaka kuwa rais lazima awe mwadilifu wa asili na siyo wa kujifanya. Awe pia mzalendo na mwenye uwezo wa kufanya uamuzi.

“Rais awe amesoma na asiwe na kundi, pia ajue misingi ya utawala bora, utawala wa sheria na aonekane kuwa anachukia rushwa kwa vitendo. 

Kauli ya Msuya

 Mwezi huohuo wa Septemba mwaka jana, mwanasiasa mkongwe nchini, Cleopa Msuya, alitaja sifa 16 za rais ambazo ni pamoja na uadilifu, uzalendo, mpambanaji dhidi ya rushwa na ufisadi na mwelewa na msimamizi wa uchumi.

Sifa nyingine kuwa na shauku ya ustawishaji wa uchumi na uelewa wa kujua umuhimu wa kujenga na kusambaza huduma za miundombinu ya kiuchumi na kijamii. Pia rais anapaswa awe ni mtu mwenye kujua umuhimu wa watu kufanya kazi, uwezo wa kuwatetea na kukomesha unyanyasaji wa wananchi ndani ya nchi yao, uwezo wa kuelewa misingi ya uchumi wa taifa na uwezo wa kufumua maovu yanayofanyika.

Awe pia mnyenyekevu na mapenzi kwa taifa na wananchi,  awe na uwezo kuongoza na kuona mbele, awe na uwezo wa kutofautisha mambo ya nchi na binafsi, aweze kutofautisha mambo ya biashara na mali za umma, kutofautisha mambo ya ofisi na nyumbani na pia awe na uwezo wa kusimamia na kuwezesha wananchi katika uchumi.

No comments:

Post a Comment