Wabunge na Madiwani wa Wilaya ya Nzega wamemchongea
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo kwa Rais Jakaya Kikwete
wakimtaka kuondoka naye kwa kile walichodai kuwanywesha wananchi maji
machafu kwa kipindi cha miaka mitano.
Wabunge hao ni wa Nzega (CCM), Dk. Hamis Kigwangalla na Sellemani Zedi
wa Bukene (CCM), ambao walimtaka Rais Kikwete kuondoka na mkurugenzi
huyo, Kyuza Kitundu, kwa kuwa alikwishakataliwa na Baraza la madiwani.
Dk. Kigwangalla alisema Mkurugenzi huyo hatakiwi katika halmashauri hiyo
kutokana na kutumia miaka mitano kuwanywesha maji machafu wananchi huku
uwezekano wa kupata maji safi na salama ukiwepo.
Alisema Baraza la madiwani lilikwishapitisha azimio la kumkataa katika
vikao vyake lakini utekelezaji haujafanyika hali ambayo inaendelea
kuwaumiza wananchi.
“Mheshimiwa Rais hapa tuna kero kubwa ya maji, wananchi wanakunywa maji
machafu, yananuka na yana wadudu; yote haya ni kwa sababu ya mkurugenzi
kushindwa kufanya kazi yake baraza la madiwani limekwisha mkataa naomba
mkuu mkurugenzi uondoke naye kwani ni kero kwa wananchi,” mbunge huyo
alimweleza Rais.
Kwa upande wake, Zedi alipopewa fursa ya kuwasalimia wananchi alimuunga
mkono mbunge mwenzake na kumwomba Rais Kikwete aondoke na mkurugenzi
huyo pamoja na mhandisi wa maji ili wananchi waweze kupata maji safi na
salama.
Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe aliposikia suala hilo
aliwaahidi wananchi hao kuwa mhandisi wa maji wilayani Nzega, Mariam
Majara ataondoka naye katika ziara hiyo ili kuleta ufanisi katika
utendaji kazi na wananchi hao waweze kupata fursa ya kupata maji safi na
salama.
Kwa upande wake, Waziri wa Fedha Dk. William Mgimwa, alisema Wilaya hiyo
imetengewa fedha za kutosha katika sekta ya maji hivyo ni kosa
kushindwa kutoa huduma hiyo kwa wananchi.
Akijibu maombi ya wabunge hao ya kuondoka na mkurugenzi mtendaji pamoja
na mhandisi wa maji Rais Kikwete alisema kuwa suala hilo litatatuliwa.
Alisema inasikitisha kwamba serikali inatenga fedha za kutosha kwenye
halmashauri kwa ajili ya kurahisisha wananchi kupata huduma bora lakini
baadhi ya watumishi wanakwamisha jitihada hizo.
No comments:
Post a Comment