Nyara za Serikali zakutwa nyumbani kwake

Polisi wa mkoa wa Arusha wakiangalia Nyara za Serikali zilizokamatwa katika eneo la Mateves Ngaramtoni jijni Arusha 

SHEHENA za nyara za serikali zinazokadiriwa kuwa za thamani ya mamilioni ya fedha zimekamatwa na polisi eneo Mateves, Ngaramtoni ya Chini mjini hapa.

Nyara hizo ni meno mawili ya Tembo, ngozi, vichwa na pembe za wanyamapori mbalimbali zikiwamo Tembo, Simba, Viboko, Nyati, Nyumbu, Ngiri, Mbwamwitu na wanyama wengine ambao thamani ya vitu hivyo haijajulikana.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema kukamatwa kwa mtuhumiwa ni kutokana na taarifa za raia wema kuhusu kuwapo mtu anayejihusisha na biashara ya uwindaji bila vibali vya mamlaka husika.

Sabas alisema baada ya kumhoji mtuhumiwa alidai nyara hizo zimekuwa zikikusanywa tangu mwaka 2007 na zimekuwa zikihamishwa kutoka eneo moja hadi jingine kwa nyakati tofauti.

Katika hatua nyingine, Sabas alikanusha taarifa zilizochapishwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari kuwa polisi inashirikiana na majangili kuwinda na kufanikisha mtandao wa ujangili nchini.

“Nataka niseme polisi haishirikiani na wahalifu kufanya uhalifu, hayo yanaweza kufanywa na polisi binafsi lakini siyo taasisi na wahusika wanachukuliwa hatua kama wahalifu wengine,” alisema.

Kwa upande wake, Ofisa wa Kikosi cha Kupambana na Ujangili Kanda ya Kaskazini, Deodanus Makene alisema thamani halisi ya nyara hizo haijajulikana na itatolewa baada ya wataalamu kufanya tathmini. Makene alisema nyara zilizokamatwa zinaruhusiwa katika uwindaji wa kitalii, ila mtuhumiwa hana vibali vinavyoonyesha mazingira alikozipata.

Tukio hilo lilivuta hisia za watu wa eneo hilo kutokana na wingi wa nyara hizo ambazo hazikuenea kwenye gari kubwa la polisi aina ya Scania ambalo hutumika kuwapelekwa watuhumiwa mahakamani.

No comments:

Post a Comment