Nahodha, mmiliki boti iliyoua Ziwa Tanganyika mbaroni

Mkurugenzi wa SUMATRA, Ahmad Kilima

Jeshi la Polisi mkoani Kigoma linawashikilia nahodha wa boti ya MV Yarabi Tunashukuru yenye namba za usajili KST 0029, Akilimali Seif (34) na mmiliki wake, Musiwa Omary (37), kwa tuhuma ya kubeba abiria zaidi na mizigo kupita kiasi na kusababisha boti kupasuka na watu 13  kufariki dunia na 67 kuokolewa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Frasser Kashai, alisema tukio hilo lilitokea Januari 3, mwaka huu saa 4:30 usiku katika eneo la mwambao wa Ziwa Tanganyika katika Kjiji cha Herembe Kata ya Sigunga Wilaya ya Uvinza.


Kashai alisema kuwa boti hiyo ilikuwa inatokea Namansi, wilayani Nkasi, Mkoa wa Rukwa ikielekea Burundi ilikuwa imebeba abiria zaidi ya 85 na mizigo na kusababisha boti hiyo kupasuka  na kuzama katika Ziwa Tanganyika.


Miili ya watu 13 wamepatikana wakiwa wamekufa wanaume wanne na wanawake tisa huku  67 waliokolewa wakiwa hai.

Kamanda huyo alisema wanaohofiwa kufa maji juhudi za kuwatafuta bado zinaendelea na kwamba nahodha na mmiliki wa boti hiyo wanatarajiwa kufikishwa mahakamani upelelezi utakapokuwa umekamilika.

Kamanda Kashai aliwataka wamiliki wa vyombo vya majini kuzingatia sheria za usalama majini zilizowekwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra).

No comments:

Post a Comment