Wabunge walalamikia jengo lao kuvuja

Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai 


BAADHI ya wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wanaoendelea na kikao cha 10, wameulalamikia uongozi wa Bunge kwa kutojali kufanya marekebisho ya jengo la Bunge wakidai kuwa linavuja kwa muda mrefu sasa.

Malalamiko ya wabunge hao yalifikishwa kwa Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai jana, ambapo walisema kwamba wana wasiwasi na usalama wa jengo hilo.

Ubovu huo ulibainika juzi Ijumaa baada ya mvua kuanza kunyesha usiku saa saba na kuendelea hadi mchana katika maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma.
Mbali na eneo linalokaliwa na wabunge kuvuja, maeneo mbalimbali ya jengo la bunge yalikuwa yanavuja.

“Taarifa mheshimiwa Naibu Spika, hili jengo linavuja, kwa kweli hata hapa nilipokaa ndiyo hasa maji yanapita... sasa tuhakikishiwe usalama wetu Naibu Spika,” alisema Mchungaji Peter Msigwa.
Akijibu hoja hiyo, Ndugai alisema, “Taarifa zimefika kwa sasa wataalamu wetu wa maeneo mbalimbali ya jengo wanafanya kazi kuhakikisha wanarekebisha hali hiyo.”

Jengo la Bunge mjini Dodoma lililojengwa kisasa zaidi kwa ushirikiano kati ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa gharama ya zaidi ya Sh29.8 bilioni kwa sasa lina uwezo wa kubeba wabunge 350 kwa pamoja, wageni maalumu zaidi ya 100 na wananchi wasikilizaji 200.

Ukumbi huo wa kisasa umekuwa mfano wa kuigwa ambapo wawakilishi wa mabunge kadhaa kutoka nchi mbalimbali za Afrika ambao wamekuwa wakifika mjini Dodoma wamekuwa wakiuchukulia kama mfano.

No comments:

Post a Comment