Mwanza kwachafuka tena

 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Valentino Mlowola.

Na Aidan Mhando, Mwananchi

Mwanza. Shughuli za wakazi na wafanyabiashara wa Soko Kuu na Mtaa wa Makoroboi jijini Mwanza jana zilisimama kwa zaidi ya saa nne baada ya kuibuka vurugu kati ya Wamachinga na polisi na kusababisha maduka katika maeneo hayo kufungwa.

Vurugu hizo ziliibuka saa sita mchana na kusababisha polisi waliokuwa kwenye magari manne aina ya Land Rover Defender na Toyota Land Cruiser kurusha mabomu ya machozi kuwatawanya wafanyabiashara waliokuwa wakijibu mapigo kwa kuwarushia mawe.

Hali hiyo ilisababisha magari yaliyokuwa yameegeshwa pembeni mwa Barabara ya Nyerere kuvunjwa vioo pia madirisha ya Msikiti wa Singasinga na ya nyumba kadhaa za Mtaa wa Makoroboi pia yalivunjwa vioo. Zaidi ya Wamachinga 50 walikamatwa na polisi ingawa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Valentino Mlowola alisema ni mapema kutaja idadi.

Kwa mujibu wa polisi, chanzo cha vurugu hizo ni baadhi ya wafanyabiashara walioondolewa Mtaa wa Makoroboi karibu na Msikiti wa Singasinga, kurejea hivyo kuondolewa kwa nguvu.

Mwandishi wa habari hii alishuhudia mamia ya wakazi wa Jiji la Mwanza katika barabara za Pamba, Nyerere na Kituo cha Sokoni wakiwa wakikimbia huku na kule kutokana na mabomu ya machozi yaliyokuwa yakirushwa. Moja ya mabomu hayo yaliangukia katika jengo la Benki ya Access na kusababisha wafanyakazi wake kutoka nje.

Kamanda Mlowola alisema operesheni hiyo ni ya kawaida na kwamba wamefanya hivyo kuondoa wafanyabiashara waliorejea maeneo wasiyotakiwa.

No comments:

Post a Comment