Mume amuunguza sehemu za siri mke wake
MWANAMKE mkazi wa Kijiji cha Matui, wilayani
Kiteto, mkoani Manyara ameponea chupuchupu kuuawa baada ya mume wake
kumchoma na chuma cha moto sehemu za siri kutokana na wivu wa mapenzi.
Mwanamke huyo alifanyiwa kitendo hicho juzi usiku
kwenye kijiji hicho, baada ya mume wake kumtuhumu kuwa ana uhusiano wa
mapenzi na msaidizi wao wa nyumbani.
Akizungumza kwenye Hospitali ya
Wilaya ya Kiteto juzi, wakati akipatiwa matibabu mwanamke huyo alisema
hivi sasa anasikia maumivu makali.
Alisema alipofanyiwa kitendo hicho alipoteza
fahamu kwa muda mrefu, kwani alitokwa na damu nyingi na alizinduka baada
ya kufikishwa hospitalini hapo iliyopo umbali wa kilomita 32 kutoka
nyumbani kwake.
Aliongeza kuwa kabla ya kufanyiwa kitendo hicho,
kila mara mume wake alikuwa anamweleza kuwa amesikia tetesi kuwa ana
uhusiano wa mapenzi na msaidizi wa kazi, hivyo atamfanyia kitu ambacho
hatakisahau.
“Siku ya tukio hilo alikoka moto akachukua nondo
ya kuweka alama kwenye ng’ombe, akaniambia ingia ndani mke mwenzako
anakuita, nilipoingia ndani naye akaingia na kufunga mlango akaniingiza
hiyo nondo ya moto,” alisema.
Daktari wa hospitali hiyo, Godfray Mbise alisema
mwanamke huyo amepata kilema cha maisha baada ya kufanyiwa kitendo hicho
cha kikatili, kwani ameachiwa majeraha sehemu za siri, mapajani na
mgongoni.
Hata hivyo, Diwani wa Kata ya Matui, Kidawa
Athuman alisikitishwa na kitendo cha Polisi wa Kituo cha Matui
kutochukua jambo hilo kwa uzito.
Athuman alisema askari hao wanashindwa kumchukulia
hatua mwanaume aliyefanya kitendo hicho, kutokana na nguvu kubwa ya
uchumi aliyonayo.
Pia, alisema kijana huyo msaidizi wa kazi ambaye
anahisiwa kuwa alikuwa na uhusiano na mwanamke huyo, naye alichomwa moto
sehemu ya taya na alitoroshwa katika maboma ya Kimasai akitibiwe ili
kuficha jambo hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Akili Mpwapwa
alisema hajapata taarifa za tukio hilo na kwamba, atazifuatilia
ikufahamu hatua zilizochukuliwa baada ya kutokea jambo hilo.
“Ndiyo
kwanza wewe unanipa habari hizi, ngoja nizifuatilie kisha nitakujulisha
kinachoendelea lakini hadi hivi sasa (jana) bado sijapewa taarifa yoyote
kuhusiana na kitendo hicho,” alisema KMpwapwa.
No comments:
Post a Comment