Katiba ituruhusu kuhoji matokeo ya urais’

Baadhi ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wamependekeza muundo wa Katiba utoe mamlaka kwa Mahakama kutangaza matokeo ya uchaguzi na kuwapa nguvu wananchi kuhoji matokeo hayo ikiwa imebainika kuwapo na matatizo, badala  ya kuiachia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).


Wakazi hao walisema hayo wakati wakitoa maoni yao kwa tume ya mabadiliko ya katiba jana jijini Dar es Salaam, katika mchakato unaoendelea ikiwa ni awamu ya nne tangu uanze.

Walisema katiba iliyopo haitoi fursa kwa wananchi kuhoji matokeo ya uchaguzi hata kama kunaonekana kuwapo na matatizo hususani upande wa Rais.

“Nafasi ya Rais imepewa kinga kubwa sana katika uchaguzi, hata pale matokeo yanaponekana kuwa na utata, wananchi wanashindwa kuhoji kwa kuwa Katiba haijaruhuru kufanya hivyo,” alisema Jackson Makala.

Kwa mujibu wa katiba ya sasa, baada ya Nec kutangaza matokeo ya uchaguzi wa Rais, hakuna chombo chochote kinachoweza kuhoji, ikiwemo Mahakama.

Kwa upande wake Ntogwa Manamba, aliomba katiba mpya imuondolee Rais nafasi 10 za kuteua wabunge, badala yake nafasi hizo waongezewe wanawake wa viti maalum.

Aliongeza kwamba nafasi za wakuu wa mikoa na wilaya wasiteuliwe na Rais, bali zitangazwe nafasi za ajira  kama zinavyotangazwa nafasi nyingine za kawaida.

Kuhusiana na suala la Muungano, wananchi hao wameiomba tume ya mabadiliko ya katiba kuwaunganisha Watanzania kutoka Zanzibar na Bara ili wapige kura ya maoni  juu ya muungano huo.

“Katika suala la Muungano ni lazima maamuzi magumu yafanyike, Watanzania wa pande zote mbili wapige kura waamue kuuvunja au kuendelea nao,” Julius Agensi.

Aliongeza: “Hakuna haja ya kuendelea kulumbana la suala moja la muungano, tunaomba maamuzi yafanyike suluhu ipatikane kwa kura.”

Suala jingine lilionekana kutolewa maoni sana na wananchi hao, ni kutaka katiba mpya iainishe nafasi ya vyombo vya habari kuwa mhimili wa nne.

No comments:

Post a Comment