Mbunge Kigwangalla mbaroni

Mbunge wa Nzega, Dk. Khamis Kingwangalla (CCM).

Mbunge  wa Nzega, Dk. Khamis Kingwangalla (CCM), ametiwa mbaroni na Jeshi la Polisi katika tukio la vurugu kwenye machimbo ya dhahabu.

Vurugu hizo ziliibuka jana katika machimbo ya dhahabu ya Mwashina yaliyopo wilayani Nzega, Tabora na Jeshi la Polisi kulazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya wachimbaji wadogo waliokuwa wakiandamana wakiongozwa na mbunge huyo.

Wananchi hao walikuwa wakiandamana jana kuanzia eneo la Isunga Ngwanda kuelekea katika machimbo hayo kupinga kitendo cha serikali kufunga machimbo hayo ambayo wamekuwa wakichimba dhahabu kwa muda mrefu na kuwasaidia kupata riziki.

Vurugu hizo ambazo zilianza majira ya mchana, zilisababisha watu wengine kadhaa kutiwa mbaroni sambamba na Dk. Kigwangalla.

Dk. Kigwangalla akizungumza na NIPASHE kwa simu muda mfupi baada ya kutiwa mbaroni, alisema wakiwa katika maandamano hayo polisi walianza kuwatawanya waandamanaji kwa mabomu ya machozi na yeye alifanikiwa kutoroka.

Hata hivyo, baadaye polisi walifanikiwa kumkamata na kumuweka ndani na hadi jana saa 10:45 jioni, mbunge huyo alikuwa bado chini ya ulinzi wa polisi huku waandamanaji wakiwa wametawanyika.

“Soma facebook yangu, nimenusurika kufa na sasa nimekamatwa na polisi na kuwekwa ndani…baada ya askari kuwatawanya wananchi kwa risasi za moto. Nitatoka kwenye mawasiliano sasa hivi,” alisema Dk. Kigwangala wakati akizungumza na NIPASHE.

Dk. Kigwangalla katika mtando wake wa facebook alisema katika vurugu hizo kijana mmoja aliyekuwa karibu naye alipigwa risasi baada ya riasi hiyo kumkosa yeye.

“Nimenusurika kuuawa muda si mrefu. Mungu mkubwa. Askari kwenye gari ananiambia na bahati yako nimekukosa, nililengwa kichwa....kijana mmoja aliyekaa mbele yangu amepigwa risasi kwenye paji la uso, sijui kama amenusurika,” alisema na kuongeza:

 “Vijana wamenilinda kwa ujasiri bila hofu. Leo askari wamenikamata kwa staha. Siwezi kukubali kamwe dhuluma ya mabepari dhidi ya wanyonge. Niliwaahidi na niliapa kuwatetea.”

Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Bituni Msangi, alisema alijulishwa kuwapo kwa vurugu hizo na Mkuu wa Polisi wa wilaya (OCD).

“Nipo nje ya wilaya, lakini nimepata taarifa kutoka kwa OCD kwamba kumetokea vurugu ila sijafahamu vurugu hizo zimesababishwa na nini,” alisema Msangi.

Hata hivyo, taarifa ambazo zililifikia gazeti hili jana  jioni, zilieleza kuwa wachimbaji  watano akiwamo mbunge huyo waliokamatwa sambamba na mbunge huyo wamewekwa katika kituo kikuu cha polisi wilayani humo.
 

No comments:

Post a Comment