Lowassa: Siwezi kuzuia mafuriko kwa mikono


 

Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa amesema kuwazuia wananchi kwenda nyumbani kwake kumshawishi agombee urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu ni sawa na kuzuia mafuriko kwa mkono.

Lowassa alitoa kauli hiyo nyumbani kwake mjini Dodoma jana wakati alipotembelewa na kundi jipya kutoka Mbarali mkoani Mbeya waliokwenda kumshawishi atangaze nia kugombea urais.

Lowassa ametoa kauli hiyo siku moja baada ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye kusema kuwa kwa kuandaa makundi ya kumshawishi, mbunge huyo wa Monduli anajua adhabu yake na anaweza kupoteza sifa za kuwa mgombea urais kupitia CCM.

“Sasa mmekuja siku mbaya kwa sababu jana kuna watu wamesema maneno mengi mabaya ambayo kwa malezi yangu mimi mambo ya chama humalizwa kwenye vikao vya chama na siyo kwenye vyombo vya habari. Mnazungumza, mnaelewana mnatoka pale,” alisema.

“Na utaratibu huu ulioanzishwa na watu, mimi ni vigumu kuuzuia, utazuiaje mafuriko kwa mikono? Mafuriko yanakuja halafu nazuia kwa mikono nitaweza kweli? Hawa watu sina hoja nao, sina cha kuwaambia,” alisema.

Mambo ya chama

Lowassa ambaye hivi karibuni aliweka bayana kuwa ameshawishika kuwania nafasi hiyo, alisema, “Lakini mambo ya chama hayawezi kuwa kwenye ma-TV, magazeti na maredio, mara huyu hivi, mara huyu vipi. Mkiona chama kinakwenda kwa utaratibu huo, ni hatari sana, CCM ninayoijua mimi ni ya vikao.”

Alisema hakusudii kujibu hizo hoja (za Nape) bali rafiki yake Hussein Bashe amezielezea vizuri.

“Niseme mawili tu yanayonisikitisha wanasema eti nawaiteni, nakupeni fedha, mimi hela natoa wapi? Lakini kibaya zaidi nikiweka maturubai hapa ni kosa, mkiwa na viti hapa ni makosa? Na wanasema nawapeni chakula mambo ya ajabu sana na yanasemwa na watu wazima wenye heshima

zao,” alisema Lowassa na kuongeza:

“Juzi walikuwapo vijana 300 hapa, nitawapikia chakula nitawaweza? Nyie kwa wingi huu mtaenea hapa? Lakini ni vibaya unamdhalilisha binadamu mwenzako kuwa maisha yake yote ni kufikiria tumbo. Hamna cha kufikiri isipokuwa tumbo, kwa hiyo mnakuja hapa kwa sababu mnataka Lowassa awapeni chakula, ni kudhalilisha watu.”

Alisema watu wanaofika nyumbani kwake wanafanya hivyo kwa utashi, hiari na gharama zao wenyewe na wengine yeye hawafahamu kabisa.

Lowassa alisema hajawahi kuwaona, wala kuwatuma kufanya hivyo au kuwaomba kufika nyumbani kwake watu ambao wanamshawishi kutangaza nia ya kugombea urais.

Ushauri wa Kikwete

Aliwashauri wengine ambao hawajafika wasubiri chama kiseme nini kifanyike kwa watu wanaotaka kuja kunishawishi.

“Kwa sababu Rais (Jakaya Kikwete), alivyokuwa Songea kule na mimi nilikuwapo kule akasema mkiona hawa hawatoshi muda upo bado washawishini wengine waingie, sasa mkifanya hivi ni kosa, ni kampeni.

Ipi si kampeni sasa? “alihoji Lowassa na kuongeza:

“Nawashauri tusiingize mgogoro kwenye chama tungoje tupate maelekezo, mimi nina uhakika kuwa tutapata nafasi. Hakika ipo siku Watanzania watapata uhuru wa kusema juu ya mtu mimi. Watapiga kura zao kusema naam ama hapana. Kwa hiyo tungojee siku. Nami nina hakika wako Watanzania wengi wanaonipenda.”

Lowassa alisema, “Kwa hiyo huyo anayepiga kelele nyingi sijui tutoke chama, sijui tufanye nini? Angojee wanachama wa CCM na wananchi waamue. Mimi ni mwanademokrasia, ninaamini kwenye demokrasia lakini pia kwenye utendaji bora.”

Lowassa, ambaye bado anatumikia kifungo cha mwaka mmoja kutoka chama chake aliwataka watu hao kujiandikisha kwa wingi na kupiga kura kwa mtu ambaye wanaamini ataweza kuwaongoza kwa kutoa maamuzi magumu na makubwa kwa faida ya nchi.

Juzi, Nape alisema kitendo cha makundi ya watu kwenda kumshawishi Lowassa atangaze nia ya kuwania urais ni kinyume cha Katiba ya CCM.

Alisema kitendo hicho ni kampeni ya wazi ya urais anazoendelea nazo kabla ya muda kufika na kuonya kama ataendelea atapoteza sifa za

kugombea nafasi ya urais.

Katika kipindi cha wiki mbili sasa kwenye makazi yake Monduli mkoani Arusha na Area C mjini Dodoma makundi ya watu mbalimbali yamekuwa yakifika kumshawishi agombee urais baadaye mwaka huu.

No comments:

Post a Comment