Usafiri wa reli wamchanganya Dk. Mwakyembe



Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amesma sekta ya usafiri wa reli nchini inakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo gharama kubwa za uendeshaji, kutoaminika, huduma duni, sheria, sera na mifumo ya udhibiti kutokana na kutokuwepo na uwekezaji wa kutosha usiokuwa na ushindani.

Dk. Mwakyembe alisema hayo wakati akifungua mkutano wa siku mbili wa watalaamu wa sekta ya usafiri wa reli uliokuwa ukijadili rasmu ya sera ya reli nchini ambao ulifanyika jana jijini Dar es Salaam.

Dk. Mwakyembe alisema ili kurejesha sekta ya reli kama ilivyokuwa miaka ya nyuma, serikali imeamua kuandaa sera ya reli itakayojitegemea badala ya hivi sasa ambapo ipo sera ya uchukuzi ambayo ni pana na inajumuisha mambo mengi.

Alisema miongoni mwa mambo ambayo yanatakiwa kuangaliwa na wataalam hao ni kuona kama Tanzania tuwe na reli ya upana upi, kwani iliyopo ina upana wa mita moja.

Aliongeza kuwa baadhi ya wadau wanaona kwamba upana wa mita moja ni kama umepitwa na wakati japo zipo nchi kama Japana na nchi nyingine barani Afrika zinazotumia reli yenye upana huo.

Dk. Mwakyembe alisema hata kwa nchi za Afrika Mashariki zinahitaji kuwa na mfumo wa reli zenye upana mmoja ambazo ni mita 1.435 ambayo inatumiwa na nchi nyingi duniani.

Alisema kwa nchi kubwa kama Tanzania yenye idadi ya takribani watu milioni 40 kunahitaji kuwa na usafiri wa reli wa uhakika ambao ni muhimu kwa maendeleo ya nchi.

Alisema katika kuhakikisha sekta ya usafiri wa reli inaboreshwa, serikali ipo katika mchakato wa kununua vichwa 13 vya treni na vingine 18 vya kukodishwa.

Hata hivyo, Dk. Mwakyembe alisema kukodisha vichwa vya treni imekuwa ghali sana hivyo serikali inalenga kufufua vichwa vibovu vilivyopo nchini kwa kuhakikisha mafundi wanafanya kazi hiyo usiku.

Mwenyekiti wa kamati iliyopewa jukumu la kutayarisha rasmu ya kutengeneza sera ya reli, Dk. Malima Bundara, alisema wakati wa kutembelea mikoa mbalimbali walibaini hali ya usafiri wa reli ni mbaya na miundombinu yake imechakaa sana.

Dk. Bundara alisema changamoto nyingine walizobaini ni kuvamiwa kwa njia za reli na uwekezaji hivyo kuna haja ya kuwa na miongozo kama serikali katika kuboresha usafiri huo.

No comments:

Post a Comment