Sh Milioni saba ‘zafichwa’ akaunti binafsi


Mratibu Elimu kata wilayani Nzega mkoa wa Tabora amekiri kuchukua pesa za ujenzi wa shule na kuweka kwenye akaunti yake.

Mratibu huyo, Richard Nkwabi wa Kata ya Puge wilayani Nzega alikiri kuweka fedha hizo baada ya malalamiko ya wananchi wa kata hiyo kumshutumu  yeye pamoja na diwani Alex Nyasani kujichukulia maamuzi ya kuweka pesa za maendeleo ya ujenzi wa majengo mawili ya shule ya kidato cha tano na sita ya shule ya sekondari Puge kwenye akaunti binafsi.

Shutuma nyingine zilizotolewa na wananchi hao kwa viongozi wao ni kutekeleza mradi wa madarasa hayo na kuuhamishia sehemu nyingine kwa lengo la kujitafutia njia ya ‘kutafuna’ pesa hizo za serikali.

Akizungumza na NIPASHE Jumapili kwa njia ya simu toka wilayani Nzega, Nkwabi alikiri na kusema kiasi cha Sh.milioni 7.4, zimewekwa katika akaunti yake Novemba 30, mwaka huu katika benki ya NMB tawi la Nzega kutokana na kutekeleza maamuzi ya Kamati ya Maendeleo ya Kata (OBC).

"Kweli kiasi hicho kimewekwa katika akaunti yangu ya NMB tawi la Nzega, lakini nimetekeleza maagizo ya OBC yaliyonitaka nifanye hivyo...hizo ni kati ya Sh.milioni 13 zilizotolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa shule," alisema Nkwabi.

Nkwabi alisema Sh.milioni sita kati ya 13, zilitumika kununulia vifaa vya ujenzi yakiwemo mabati, lakini kiasi kilichobaki kamati iliamua ziwekwe kwenye akaunti binafsi hadi hapo watakapofungua ya kamati ya ujenzi.

“Kweli pesa ziliingia tangu Juni mwaka huu, lakini kutokana na kuhofia kurejeshwa zilikotoka, ikaamuriwa nyingine zitumike kwa kununulia vifaa na nyingine ziwekwe kwenye akaunti yangu,” alisema.

 “Tunaamini lengo la viongozi hao na kamati yao, walikuwa na mpango wa kutafuta njia ya kuudhoofisha mradi huo ikiwa ni pamoja na kuhamisha ujenzi ambao tayari ulikuwa umeanza sehemu iliyopendekezwa na wananchi na kupeleka kwingine, lakini mbaya ni pesa za mradi kuwekwa akaunti binafsi,” alisema mmoja wa wananchi walalamikaji.

Aidha, walielekeza shutuma kwa Diwani wao, Alex Nyasani kwa kuruhusu ujenzi kufanyika wa shule kufanyika sehemu nyingine bila kuhusisha vikao vya wananchi wenye kutoa maamuzi.

Lakini wananchi hao wanasema, mvutano uliopo sasa na viongozi wao ni kushindwa kuwaeleza kuiendeleza shule hiyo ambayo ilipewa baraka na viongozi wa serikali na pesa zake kupewa halmashauri ili izigawe kwa ajili ya muendelezo wa shule hiyo ambayo mpaka sasa madarasa yake mawili yamesimama hatua ya madirishani.

Pia, wananchi hao walisema madarasa ya shule hiyo yamejengwa sehemu yenye nafasi na pia ni jirani na ilipo hosteli ya wanawake wa shule ya Puge, jengo la utawala na maabara, hivyo kuanzishwa kwa ujenzi mwingine kunaashiria ‘utafunaji’ wa pesa hizo.

Hata hivyo, diwani wa kata hiyo, Nyasani akizungumzia shutuma hizo za wananchi wa kata yake, alisema hayana msingi kutokana na kinachofanyika ndicho kinachotakiwa kwa ajili ya maendeleo ya kata ya Puge.

Wakati Nkwabi akikiri kuweka pesa za ujenzi wa shule katika akaunti yake, diwani Nyasani alimtetea na kusema hakuna kitu kama hicho, na kuirushia mpira kamati ya maendeleo ya kata.

No comments:

Post a Comment