Baba wa binti aliyebakwa ataka mwanawe atajwe

Kikundi cha Jumuiya ya wanafunzi nchini India wakiwa wameshika mabango wakati wa maandamano ya kupinga vitendo vya ukatili likiwamo kitendo cha ubakaji kilichofanywa kwa mwanamke aliyefariki. Picha na AFP 

NEW DELHI, India
BABA wa binti aliyefariki dunia baada ya kubakwa na kuteswa amesema kuwa anataka jina la binti yake litajwe hadharani ili afahamike na kuwa mfano kwa waathirika wengine wa vitendo vya ubakaji.

Mzazi huyo amesema hayo katika mahojiano yaliyochapishwa leo na gazeti moja la Uingereza, ambapo alisema anaona kwamba ni sahihi kwa dunia kujua jina halisi ya binti huyo.
Baba huyo aliliambia gazeti hilo la Sunday People kuwa binti yake hakuwa na kosa na alikufa wakati akijaribu kujihami na yeye kama mzazi anajivunia mwanaye huyo kwa ushujaa wake.

“Binti yangu hakufanya jambo lolote baya, alikufa wakati alipokuwa akijaribu kujitetea. Ninajivunia ujasiri wake. Kulitaja wazi jina lake kutawapa ujasiri wanawake wengine ambao wamewahi kukumbwa na matukio kama haya. Watapata ujasiri mpya kupitia kwa binti yangu,” alisema baba huyo.
Anasema kutajwa jina la mwanawe kutawapa moyo wanawake wengine waliobakwa na kufanikiwa kubaki hai na kuwapa nguvu ya kusonga mbele na maisha. Sheria za India zinazuia kujulikana hadharani kwa waathirika wa visa vya ubakaji.
Kauli ya baba huyo inakwenda sambamba na ombi la mmoja wa mawaziri nchini humo, Shashi Tharoor ambaye alisema kwamba ni vyema jina la binti huyo likitajwa hadharani ili litumike kaka chanzo katika kutunga sheria mpya dhidi ya wabakaji.
Wiki iliyopita, Tharoor ambaye ni Waziri mdogo wa Elimu alizitaka mamlaka zinazohusika kuliweka wazi jina la binti huyo ili kutoa fursa kwa sheria mpya kumtumia kama mfano wa waathirika wa ubakaji unaofanywa kwa makundi nchini humo.
“Labda tu kama wazazi wake watazuia, lakini atapewa heshima na kutumiwa kama chanzo cha sheria mpya dhidi ya wabakaji. Huyu alikuwa binadamu mwenye jina, hakuwa alama ya ishara,” alisema.
Binti huyo aliyekuwa na umri wa miaka 23 alifariki dunia akipatiwa matibabu nchini Singapore baada ya kuvamiwa, kubakwa na kuumizwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake akiwa mjini New Delhi, India.
Sheria hizo zina lengo la kumsitiri mwathirika na kumuwepusha na usumbufu wa vyombo vya habari hasa ndani ya taifa hilo ambapo unyanyapaa dhidi ya watu waliobakwa ni mkubwa sana.
Baba mzazi wa binti huyo aliliambia pia shirika la habari la Reuters kuwa hana pingamizi lolote kwa vyombo vya habari kulitaja na kulitumia jina la mwanawe katika mikasa ya ubakaji.

No comments:

Post a Comment