KWA mara nyingine Jeshi la Polisi mkoni Kagera, limepata pigo
kutokana na askari wake wawili kuuawa kikatili na wananchi wilayani
Karagwe wakidhani kuwa ni majambazi na kisha gari lao kuteketezwa kwa
moto.
Tukio hilo linakuja zikiwa ni wiki chache tangu wananchi wenye hasira
kuua askari wengine wawili wilayani Ngara na kuteketeza kituo cha polisi
cha Mugoma mnamo Desemba 15, mwaka jana.
Akizungumza na Tanzania Daima, Kamanda wa Polisi Mkoa Kagera, Phillip
Kalangi, alisema tukio hilo lilitokea Januari 6, mwaka huu, saa 2:30
usiku katika kijiji cha Kasheshe, kata ya Rugu, upande wa wilaya ya
Karagwe wakati walipofika kijijini hapo kumfuatilia mtu mmoja aliyekuwa
na meno ya tembo.
Askari waliouawa ni SGT Thomas Migiro mwenye namba E1446 mwenyeji
wa mkoani Mara na Koplo Damas Kisheke mwenye namba E 8889 mkazi wa
Kamachumu Muleba mkoani hapa wote wakiwa watumishi wa jeshi hilo kituo
cha wilayani Ngara.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, askari walikuwa watatu ila
mmoja wao, Bryston aliyekuwa na bunduki alikimbia na kuwaacha wenzake
wakisulubishwa.
Habari zaidi zinasema kuwa katika tukio hilo gari la askari Damas aina ya IPSUM lilichomwa moto na wananchi hao.
Askari inasemekana walifika wilayani humo na kufanikiwa kumsaka hadi
kumkamata mtuhumiwa aliyekuwa na meno ya tembo saba na kuanza kuondoka
eneo la tukio.
Hata hivyo, taarifa zilizolifikia gazeti hili kutoka eneo la tukio
zinadai kuwa polisi hao walikuwa na biashara yao binafsi na mmoja wa
wananchi wa kijijini hapo, ambaye inasemekana kuwa walitaka kumdhulumu.
Chanzo hicho kiliongeza kuwa mwananchi huyo aliwapigia simu baadhi ya
wanakijiji kuwa akiwataarifu kuwa amevamiwa na majambazi ambao
wanaondoka kuelekea Ngara.
Kwamba wakati askari hao wakiwa safarini kurudi Ngara, walikuta mawe
na magogo yakiwa yamepangwa barabarani huku wananchi wakiwataka washuke
kutoka kwenye gari, amri ambayo waliikataa na hivyo mmoja wao kufyatua
risasi iliyomjeruhi mwananchi mmoja.
Majeruhi alitajwa kuwa ni Jovinary Gabanu (35), aliyepigwa risasi
katika sehemu ya kiganja cha mkono ambaye amelazwa katika Hospitali
Teule ya Wilaya ya Nyakahanga.
Hatua hiyo ilizua vurugu na hivyo wananchi kuanza kuwashambulia askari
hao hadi kuwaua ingawa muda mfupi baadaye askari wenzao walifika eneo
la tukio na kutuliza vurugu.
Baadaye Mkuu wa Wilaya hiyo, Dary Rwegasira, alifika eneo la tukio kuwataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi.
Kamanda Kalangi alisema kuwa askari Bryton aliyekimbia alipatikana
usiku huo saa tisa na miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali
Nyakahanga ikisubiri utaratibu wa kusafirishwa.
|
No comments:
Post a Comment