Lema kuiteka Dodoma leo

MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbles Lema 


MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbles Lema wa Chadema, anatarajia kuhutubia mkutano mkubwa mjini Dodoma baada ya kupokewa kwa maandamano yanayotarajia kuanzia Ihumwa kilomita 14 kutoka Dodoma Mjini.

Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na kusainiwa na Katibu wa Chadema Wilaya ya Dodoma mjini, Jella Mambo, ilieleza kuwa msafara wa Lema utaanzia katika Kijiji cha Ihumwa ikiwa ni safari yake kuja bungeni.

Lema ataingia Dodoma na kutinga bungeni baada ya kushindwa kushiriki mikutano mitatu ya Bunge baada ya kuvuliwa ubunge wake na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha Aprili 5, mwaka jana.

Hata hivyo, Desemba 21 mwaka jana, mbunge huyo machachari alirudishiwa ubunge wake baada ya jopo la majaji kuridhika na sababu za rufaa yake na kumpa ushindi kuwa ni mbunge halali za Jimbo la Arusha Mjini.

Mambo alisema jana kuwa mapokezi ya Lema yatakuwa ni makubwa kuliko mapokezi yoyote ambayo yamewahi kufanyika katika Mji wa Dodoma na kuwa yataongozwa na msafara wa mapikipiki, magari pamoja na msururu mrefu wa watu.

Katibu huyo alisema kuwa mara baada ya kuingia mjini Dodoma, msafara wa Lema utakwenda moja kwa moja Ofisi za Chadema mkoa ambako mbunge huyo pamoja na msafara wake watakwenda kusaini kitabu cha wageni.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, mara baada ya kusaini kitabu msafara huo utakwenda katika Viwanja vya Shule ya Sekondari ya Central ambako hakutakuwa na jambo lolote litakalofanyika zaidi ya utambulisho na kisha mbunge huyo kupewa nafasi ya kuhutubia mkutano wa hadhara utakaoanza saa 10 jioni.

Kwa muda wa wiki sasa viongozi wa Chadema wa ngazi ya mkoa na wilaya wamekuwa wakihaha kwa kufanya maandalizi ya mkutano huo.

No comments:

Post a Comment