Sumaye kunyang’anywa shamba

Frederick Sumaye 


SHAMBA la Frederick Sumaye lililoko Kisarawe mkoani Pwani, liko hatarini kuchukuliwa na halmashauri ya wilaya hiyo na kuligawa upya, kutokana na Waziri Mkuu huyo mstaafu kushindwa kuliendeleza.

Habari zilizothibitishwa na viongozi kadhaa wa Wilaya ya Kisarawe, zimeeleza kuwa shamba la Sumaye lililoko eneo la Vikurunge Kata ya Kiluvya, ni miongoni mwa mashamba yaliyoko kwenye orodha ya kunyang’anywa na kugawiwa upya.

Hata hivyo mwenyewe amesema kuwa hana taarifa ya mpango huo wa halmashauri kuwanyang’anya watu mashamba.

“Sijui chochote na nipo kanisani, Sijui hata hiyo notisi ya halmashauri kutaka kunyang’anya mashamba,” alisema na kukata simu.

Chanzo cha habari kilisema “Huu ni mpango wa halmashauri na tayari imeshatoa tangazo tangu mwaka jana. Ilitoa siku 60 tangu Desemba 30 mwaka jana kwa wamiliki wake kuyaendeleza mashamba hayo, baada ya hapo yatanyang’anywa,” chanzo cha habari kilieleza na kuendelea;

“Mheshimiwa Sumaye ni miongoni mwa wamiliki hao, yeye shamba lake lina zaidi ya ekari 40 na lipo eneo la Vikurunge Kata ya Kuluvya. Ameshindwa kuliendeleza kwa kipindi cha miaka mitano sasa.”

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Makurunge, Jocline Mfuru alikiri Sumaye kumiliki eneo kubwa eneo hilo, lakini alisema taarifa zaidi zipo halmashauri ndio ambao wanajua zaidi kwani hata yeye mwenyewe ni mgeni katika nafasi hiyo ana mwezi mmoja tu tangu awepo hapo baada ya mtendaji wa awali kuondolewa.

“Sina muda mrefu katika nafasi yangu na ninatambua notisi ya siku 60 ya wale ambao hawajaendeleza mashamba lakini siwezi kuzungumzia zaidi kwani sina taarifa za kutosha,” alisema Mfuru.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kisarawe, Yona Maki alithibitisha kutekelezwa kwa operesheni hiyo na kusema kuwa sasa wapo katika hatua ya kufanya tathamini.
Akiwa amekwepa kuthibitisha kama shamba la Sumaye nalo litanyang’anywa, Maki alisema, “Ni kweli Sumaye anamiliki eneo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe na amejenga nyumba ya kuishi.”

Aliendelea “Lakini, kujenga nyumba hakutoshi kueleza kuwa shamba hilo limeendelezwa. Tunapitia nyaraka zinazohusu umiliki wake na kuona kama lipo kwenye mpango huo au la.”
Maki alisema uchunguzi unaofanyika dhidi ya Sumaye ni pamoja na kujua aliomba kumilikisha eneo hilo kwa ajili ya shughuli gani na kuangalia iwapo kile alichoombea ndicho anachokitekeleza.

“Nipe muda niweze kujua alimilikishwa kwa ajili ya utekelezaji wa jambo gani na kama hicho alichoombea ndicho anachokifanya,” alisema Maki.

Maki alifafanua kuwa hatua ya kupitia upya umiliki wa mashamba wilayani humo na uendelezwaji wake, inafanyika kwa mujibu wa sheria ya vijiji na miji namba 4 na 5 ya mwaka 1999.

 “Sheria hiyo inaeleza kuwa mtu ambaye amemilikishwa shamba au kiwanja na kushindwa kukiendeleza katika kipindi cha miaka mitano, umiliki wake utafutwa na kurudishwa halmashauri,” alisema Maki.

Mkurugenzi huyo wa halmashauri alisema kuwa eneo hilo kuna watu ambao wamemilikishwa maeneo makubwa ambao wameshindwa kuyaendeleza hali na kulingana na utekelezaji wa sheria hiyo notisi hiyo haitawahusu wale ambao wameanza uendelezaji hata kama watakuwa hawajafanya hivyo kwa asilimia mia moja.

“Kuna wawekezaji kama wale wa mradi wa kilimo cha miti aina ya mbono ambao wamepewa hekta 9,000 na tayari wameanza uendelezaji hivyo hao hawataguswa” alisema na kuwa hakutakuwa na mjadala kwa wale ambao watashindwa kufanya hivyo ndani ya muda ambao umetolewa.

No comments:

Post a Comment