Rais Mahama alipokuwa anaapishwa mbele ya maelfu ya wananchi wa Ghana
Chama rasmi cha upinzani nchini
Ghana, kimesusia sherehe za kuapishwa kwa rais mpya John Mahama kufuatia
uchaguzi wa mwezi jana uliokumbwa na utata.
Chama cha New Patriotic Party (NPP) kilisema kuwa bwana Mahama hakushinda uchaguzi huo kihalali.
Matokeo rasmi ya uchaguzi huo,
yalionyesha bwana Mahama akiwa na aslimia 50.7 idadi ambayo inatosha
kuweza kuzuia duru ya pili ya uchaguzi dhidi ya mpinzani wake Nana
Akufo-Addo, aliyepata asilimia 47.7 ya kura.
Kabla ya kuapishwa kwake, bwana Mahama alitoa
wito wa amani na umoja nchini Ghana, nchi ambayo inaonekana kama mfano
mzuri wa demokrasia barani Afrika.
Bwana Mahama alikuwa makamu wa rais wa Ghana hadi pale kifo cha ghafla cha aliyekuwa rais,John Atta Mills kutokea mwezi Julai.
Tangu hapo alihudumu kama rais wa mpito.
Rais John Mahama
Katika hotuba yake, rais Mahama aliwaambia wananchi wa Ghana kuwa hatawaangusha .
Akiwa amevalia gauni nyeupe iliyorembeshwa kwa
rangi za bendera ya nchi hiyo,rais John Mahama alitoa kauli ya
upatanishi mbele ya umati mkubwa wa watu waliofika kumshangilia.
Madai ya ulaghai na wizi wa kura, bila shaka yataathiri sifa yake kwa muda.
Lakini kuwepo kwa baadhi ya marais wa Afrika katika sherehe ya kuapishwa kwake, kunaonyesha kuwa bwana Mahama anaungwa mkono na jamii ya kimataifa.
Na sasa huenda mzozo huu ukatatuliwa kwa njia ya amani.
No comments:
Post a Comment