Majambazi yamvamia Mchina yakitaka kumpora

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela

Watuhumiwa wa  ujambazi  waliokusudia kupora fedha kutoka kwa mkurugenzi wa kampuni moja wamezua taharuki kwenye kituo cha mabasi Mwenge  jijini Dar es Salaam baada ya kurusha risasi za moto zilizosababisha watu kukimbia ovyo kunusuru maisha yao.
Wezi hao waliokuwa na  pikipiki  juzi saa 3:00 usiku  walivamia  gari  la Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Hunting International, raia wa China Jung  Won Jyo (44) kwa lengo la kumwibia fedha.

Baadhi ya abiria walikuwa na wakati mgumu kwa vile baadhi walikoswa koswa na magari wakati huo wakikimbia kujiokoa huko magari nayo yakikimbia kuondoka eneo la tukio.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela, alithibitisha kutokea kwa mkasa huo aliosema ulihusisha watuhumiwa watatu  waliokuwa kwenye pikipiki hadi jana walikuwa hawajakamatwa.

Alieleza kuwa walipofika  kituoni  hapo walilifuata moja kwa moja gari namba T 198 BRE aina ya Toyota Hiace lililokuwa limembeba Mkurugenzi Jyo likiendeshwa na Mohamed Seleman.

Alisema ndani ya gari hilo kulikuwa na mizigo ambayo majambazi hao walidhani ni fedha.
Kamanda alisema baada ya mkurugenzi huyo kufikishwa kituoni akitokea kazini kwake Sinza Makaburini,  watuhumiwa hao walianza kufyatua risasi zilizosababisha tafrani kwa watu waliokuwa kituoni hapo.

Alisema  pia walitumia jiwe  kuvunja kioo cha mbele cha gari hilo kwa lengo la kuiba mali zilizokuwamo. "Licha ya kutumia silaha za moto lakini watuhumiwa hawa waliambulia  simu mbili aina ya Samsung… hatukupata namba ya pikipiki, ila polisi wangu walifika eneo la tukio" alisema na kuongeza:

"Eneo la tukio tumeokota  risasi na ganda  la risasi iliyotumika ninachosema ni kwamba wananchi watambue kuwa wizi wa kutumia pikipiki  upo hivyo wachukue tahadhari kwa kutoa taarifa mapema …," alisema na kuongeza kuwa  hakuna aliyejeruhiwa

No comments:

Post a Comment