Mramba amsukumia zigo Balali

Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba

Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba (74), amedai mahakamani kuwa alimwelekeza aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Marehemu Daudi Balali, asisaini mkataba wa kuipa kazi kampuni tanzu ya Alex Stewart ( ASSAYERS) Government Business Corporation hadi atapofanya mazungumzo na Rais (wakati huo Benjamin Mkapa).

Mramba alitoa madai hayo jana wakati akihojiwa na wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro, mbele ya jopo la mahakimu watatu wakiongozwa na Mwenyekiti  John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela wanaosikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.

Mshitakiwa huyo na wenzake wawili wanakabiliwa na mashtaka ya matumizi mabaya ya madaraka,  kutoa msamaha wa kodi kwa Kampuni ya Alex Stewart (ASSAYERS) ya Uingereza kupitia kampuni tanzu ya Alex Stewart (ASSAYERS) Government Business Corporation. 

“Nilimweleza Balali aanishe kwa sababu bado nilikuwa sijamaliza kazi kwa kumshauri Rais hatua za kukubali mkataba na kujua jinsi ya kupata fedha za mkataba huo kwa kuwa bajeti ya mwaka wa fedha ilikuwa imeshapitishwa (wakati huo),” alidai Mramba na kuongeza:

“Mkataba ule ulikuwa wa Serikali na ulilipwa kwa fedha za serikali, kwa sababu nilikuwa nimefunga bajeti ya mwaka huo, nilitaka kukutana na Rais kumshauri na kumuelekeza jinsi ya kupata fedha.”  Alidai kuwa maagizo yake kwa Gavana ya kufanya ainisho yalikuwa kujenga imani kwa mkandarasi kwa serikali kwamba ina nia ya kujenga na hatimaye itasaini mkataba huo.  Hata hivyo, kuhusu maelezo aliyohojiwa na kuyatoa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuinisha mkataba, alidai kuwa alikuwa na maana ya kuinisho ni kuingia mkataba. 

Alidai kuwa, hajawahi kusomea mambo ya kodi bali alikuwa na mamlaka ya kusamehe kodi, kwamba alikuwa anapata ushauri kutoka kwa wataalamu wa masuala ya kodi kutoka Wizara ya Fedha na washauri wa jopo la wataalamu wa uchumi ambalo liliundwa kwa ajili ya kumshauri Waziri wa Fedha.

 Alidai, alikuwa anatumia vigezo vya kusamehe kodi kutokana na faida ya umma inayoweza kupata kama vile makampuni ya kutengeneza barabara na kwamba kukiwa na kodi kubwa makampuni yanaweza kukataa kutengeneza.  Mbali na Mramba washtakiwa wengine ni aliyekuwa Waziri wa Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu wa Hazina, Gray Mgonja

Katika kesi ya msingi, washitakiwa wanadaiwa kuwa, kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14 mwaka 2004 jijini Dar es Salaam, wakiwa watumishi wa umma kama mawaziri na katibu mkuu walitumia vibaya madaraka.

 

No comments:

Post a Comment