Mtoto mlemavu wa ngozi afariki baada ya kukatwa mkono

Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Antony Rutta

Mtoto Lugolola Bunzari (7) mlemavu wa ngozi (albino)  amepoteza maisha baada ya kukatwa mkono na kuvuja damu nyingi, kwenye tukio lililotokea  wiki hii mkoani  Tabora.

Kadhalika babu wa mtoto huyo aliuawa wakati akijaribu kumuokoa mjukuu wake baada ya kushambuliwa kwa  mapanga sehemu mbalimbali za mwili na kuvuja damu nyingi.

Kamanda wa Polisi mkoani Tabora,  Antony Rutta,  alisema mtoto huyo alikatwa mkono wa kushoto na mauaji hayo yalitokea juzi  saa 10 alfajiri katika kitongoji cha Kinondoni kilichoko kijiji cha Kanoge  wilayani  Kaliua mkoani humo.

Akizungumza na waadishi wa habari alisema watu nane  ambao hawajafahamika wakiwa na gobore,  mapanga na marungu walivamia nyumbani kwa Bunzari Shinga (33) baba wa mtoto huyo, kuishambulia familia yake  kabla ya kumkamata mtoto huyo na kumkata mkono walioondoka nao.

Alisema  pamoja na kumkata  mkono mtoto huyo  walimpiga mapanga Zengabuyaga Meli (95) babu wa mtoto huyo aliyejaribu kumsaadia mjukuu wake  asiuliwe.
Meli aliyekatwa mkono wa kulia ,  kichwani na begani alivuja  damu nyingi  na kufariki dunia muda mfupi baadaye.

Aidha Kamanda Rutta alisema licha ya watu hao kusababisha vifo vya watu hao  pia waliwajeruhi baba wa mtoto huyo Shinga kwa kumpiga risasi  mguu wa kulia  ambapo alikimbizwa katika hospitali ya Mkoa ya Kitete mjini hapa .

Pia Kamanda alisema walimjeruhi  Dama  Buyaga bibi wa albino huyo na sasa amelazwa Kitete na hali yake inaelezwa kuwa hairidhishi.

Alihusisha  mauji hayo na imani za kishirikina na kwamba uchuguzi unaendelea na kuongeza kuwa mauaji hayo ya albino ni ya kwanza mkoa humo.

Alisema familia ya Shinga  inaishi porini hivyo ilikuwa  vigumu kupata msaada kutoka kwa majirani. Kamada Rutta alitoa wito kwa wananchi na raia wema kushirikiana na polisi  kuwabaini na kuwakamata  waliohusika na mauaji  hayo.
 

No comments:

Post a Comment