Malleko: Tanzania inaweza kupata Rais Mwanamke 2015

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), Wilaya ya Arumeru, Ester Malleko. 

 TANZANIA inatarajia kufanya uchaguzi mkuu wa Rais wa awamu ya tano mwaka 2015. Uchaguzi huo pia utahusisha nafasi za ubunge na udiwani ukitanguliwa na ule wa serikali za mitaa mwakani.

Mengi yanazungumzwa kuhusu chaguzi hizo, ikiwemo uwezekano kuwa na Rais, Makamu wake au Waziri Mkuu mwanamke kutokana na uwezo wa kiuongozi unaoonyeshwa na wanawake waliopata fursa za uongozi.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), wilaya ya Arumeru, Ester Malleko anazungumzia nafasi na uwezekano huo  kama alivyozungumza na Mwandishi Wetu, Peter Saramba.

Swali: Nini kilikusukuma kuingia kwenye siasa na nini malengo yako ya baadaye?
Jibu: Nimeingia kwenye siasa kuwatumikia wananchi na kuthibitisha kuwa wanawake tunaweza. Nimekuwa mwenyekiti wa UVCCM wilaya na sasa ninaongoza wanawake.
Nafasi ya mwanamke kwenye jamii siyo kuzaa na kutunza familia pekee. Tunapaswa na hakika tuna haki ya kushiriki katika ujenzi wa taifa sawasawa na wanaume kwa kila mmoja kutekeleza na kutimiza wajibu wake pale alipo.

Swali: Wewe ni mwanachama na kiongozi wa CCM. Kuna madai kwamba chama chako kimepoteza haiba mbele ya umma kutokana na ninyi viongozi kuacha misingi iliyoasisi chama hicho. Nini maoni yako?
Jibu: CCM kama taasisi haina tatizo na haijapoteza haiba. Bado ipo na itaendelea kudumu katika misingi yake ile ile iliyoasisiwa na waasisi wa Taifa hili ambayo ni amani, upendo, udugu na mshikamano bila kujali tofauti zetu za kikabila, kidini wala maeneo mtu anakotoka.

Chama hiki bado kinaaminiwa na umma. Hilo linathibitishwa na matokeo ya uchaguzi mkuu ambapo CCM ilipewa ridhaa ya kuunda Serikali baada ya kushinda kiti cha urais na kupata wabunge na madiwani wengi.


Hata hivyo, ni kweli kuna kosoro ndogo ndogo zinajitokeza kutokana na makosa ya watu binafsi ambazo zinashughulikiwa  kupitia vikao, katiba, kanuni na taratibu za chama.

Swali: Mwaka 2015 tunaingia kwenye uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na madiwani,  kuna maneno kuwa wanawake waliopata fursa wameonyesha uwezo mkubwa kiuongozi. Unadhani muda umefika wa kuwa na Rais, Makamu au Waziri Mkuu mwanamke?

Jibu: Muda umefika, tena unapita. Ninaamini Taifa hili linaweza

kuongozwa na mwanamke kwa sababu viongozi wanawake waliopata fursa za kuongoza wameonyesha kuwa wanaweza.


Wanawake wana uwezo mkubwa wa kufanya kazi nyingi kwa wakati mmoja na kutoa uamuzi wa haraka wenye faida na maslahi kwa umma.

Wanawake viongozi wamethibitisha kuwa hawapigi dili kama ambavyo mama nyumbani asivyoweza kuisaliti familia.

Swali: Unaweza kutaja kwa uchache majina ya wanawake unaodhani wana uwezo wa kuwa Rais wa taifa hili?

Jibu: Wapo wanawake wengi wanaonivutia katika uongozi wao. Baadhi wapo kwenye nafasi zao uongizi hadi sasa katika medani mbalimbali ikiwemo uongozi wa kisiasa, kijamii na harakati mbalimbali.

Ingawa wako wengi ambao siwezi kuwataja wote, lakini kwa uchache wapo Dk Asha Rose Migiro, Dk Hellen Kijo-Bisimba, Profesa Anna Tibaijuka, Ananilea Nkya, Mama Anna Abdalah, Mama Gertrude Mongella na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Anne Makinda.

Swali: Kuna msemo kwamba mwanamke anaweza akiwezeshwa. tupe maoni yako?


Jibu: Binafsi sikubaliani na msemo huo, kwani unafifisha uwezo wa

kijiamini kwa wanawake ambao hukaa kutegemea kuwezeshwa ndipo wafanye jambo.

Siyo kweli kwamba ili mwanamke afanikiwe au kuweza jambo lazima awezeshwe. Nadhani kauli hii iliyotumika huko nyuma kuwahamasisha na kuwatia moyo wanawake kujitokeza kuwania nafasi za uongozi sasa imepitwa na wakati.


Mimi naamini uwezo wa mwanamke upo dhahiri ndiyo maana nyuma ya kila mwanaume shupavu na mwenye mafanikio, yupo mwanamke shupavu na jasiri. Na huu unathibitishwa na usemi kuwa “Kila mwanaume aliyefanikiwa,nyuma yake kuna mwanamke”

Kifamilia, mshauri mkuu wa baba ni mama. Sasa tutakubali vipi kwamba ili mwanamke afanikiwe lazima awezeshwe? Awezeshwe na nani? Huyo huyo mwanaume ambaye yeye anamshauri?

Hata hivyo, pamoja na ukweli huo, lazima tukubali kwamba adui wa mwanamke ni mwanamke mwenyewe. Wanawake hatujiamini. Lakini hata anapotokea mwenzetu kujiamini na kujitokeza, hatumuungi mkono, pengine kwa ile

ile dhana kuwa hatuwezi au wivu tu wa kike.

Swali: Jiji la Arusha ni miongoni mwa halmashauri zenye chaguzi ndogo za madiwani kujaza nafasi zilizo wazi. Unatarajia chama chako kitamudu kurejesha kata hizo nne zilizonyakuliwa na upinzani uchaguzi uliopita?

Jibu: Yeyote anayeingia kwenye mashindano, lengo lake ni kushinda. CCM tuna matumaini makubwa ya kushinda baada ya kugundua na kurekebisha makosa madogo madogo yaliyosababisha tupoteze kata hizo.

Tumesimamisha wagombea wanaokubalika na tumejiandaa kuwanadi kukamilifu kupitia sera za chama. Hatutatukana wala kuzungumzia watu binafsi kama wenzetu wanavyofanya. Tutanadi sera ili kutoa fursa kwa wananchi kuzilinganisha na za wenzetu.

Napenda kuchukua fursa hii kuwaasa watu wa  Arusha tusikubali

kutenganishwa wala kufarakanishwa kutokana na chaguzi hizi. Ni kweli kila mtu ana haki ya kufuata na kuamini itikadi aipendayo kisiasa, tufanye hivyo bila kubezana, kufarakana wala kusababisha ufa kwenye uhusiano wetu.

Baada ya uchaguzi huu na zingine zijazo, Arusha inapaswa kuendelea kuwa sehemu salama kwa maisha na mali zetu. Wananchi tunataka ufumbuzi wa matatizo yanayotukabili kwa pamoja bila kujali tofauti zetu kisiasa, kidini wala kibabila.

No comments:

Post a Comment