Mgomo kila kona kuzipinga EFDs


Mikoani. Sakata la matumizi ya Mashine za Elektroniki za Kutolea Risiti (EFD), limechukua sura mpya baada ya wafanyabiashara mikoa mbalimbali kuja juu wakisema matumizi yake yanalenga kuwaangamiza katika biashara.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wafanyabiashara hao wameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kufikiria upya mfumo wa kuzitumia, vinginenyo watajikuta wanaingia kwenye mgogoro mkubwa baina yao.

Tayari, wafanyabiashara miji ya Iringa, Songea na Mara wametoa msimamo wa kugomea matumizi ya mashine hizo na kuazimia kufunga biashara zao kama njia ya kupinga matumizi yake.

Wafanyabiashara wa Manispaa ya Iringa, jana walitangaza mgomo usio na kikomo kwa sababu mashine hizo zinawasababishia hasara. Wanadai mashine hizo licha ya kununuliwa kwa bei kubwa, inawabidi kuajiri wafanyakazi wenye ujuzi na kodi nyingine wanajikuta wakitumia sehemu za mitaji yao.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma aliwataka wafanyabiashara kuacha migomo isiokuwa na tija wala sababu, badala yake wafikishe malalamiko yao kwa uongozi husika kupitia viongozi wao.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani Mara, Baltazar Gibogo alisema mgomo huo ni halali yao, kwani Serikali inawanyanyasa wananchi wake.

Gibogo alikanusha kuwa Serikali imeshindwa kukusanya kodi hadi kubuni kutumia mashine, bali chanzo kikubwa ni kukithiri kwa rushwa baina ya wafanyabiashara wakubwa na wafanyakazi wa TRA.

Mjini Mbeya, wafanyabiashara walishauri Serikali kuzitoa bure mashine za EFD ili kuwasaidia wafanyabiashara kujijenga kibiashara badala ya kufilisika.

“Pamoja na kwamba Mamlaka ya Mapato tanzania (TRA) inasema mfanyabiashara akinunua anaweza kurudisha fedha zake kwa kupunguza zile za kodi, ukweli unabaki palepale kwamba wafanyabiashara hawana fedha taslimu kununua kitu ambacho siyo cha kuuza na kupata fedha kwa wakati huo,’’ alisema Anania Kasisi.

Imeandikwa na Florence Focas , Musoma; Geofrey Nyang’oro na Zainab Maeda, Iringa na Lauden Mwambona, Mbeya

No comments:

Post a Comment