Ukumbi bunge la Katiba sasa wakamilika





Spika wa Bunge, Anne Makinda (aliyekaa) akiwa na Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge wakati wakikagua Ukumbi wa Bunge, ambao utatumika kwa ajili ya Bunge la Katiba, mjini Dodoma jana. Picha na Ofisi ya Bunge 


Dodoma. Matengenezo yaliyotarajiwa ndani ya ukumbi wa bunge la Muungano ambao ndio utakaotumika kwa bunge la Katiba, yamekamilika na sasa ukumbi huo uko tayari kwa kazi inayotarajia kuanza Februari 18 mwaka huu.

Kukamilika kwa ukumbi huo kunaondoa hofu iliyoanza kutanda kuwa huenda bunge hilo lingesogezwa mbele kwa siku tatu kwani kulikuwa na mashaka kwa kazi hiyo.

Jana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alitembelea ukumbi huo kwa mara ya mwisho na kujiridhisha katika maeneo muhimu yaliyokuwa yakifanyiwa marekebisho .

Akizungumza na waandishi wa habari ndani ya ukumbi huo, Lukuvi alisema tayari viti 676 vimeshafungwa pamoja vipaza sauti vyake ambavyo Rais Jakaya Kikwete alionyesha mashaka kama vingekamilika kwa wakati.

Februari Mosi, Rais Kikwete alipita kukagua ukumbi huo wakati akielekea mkoani Mbeya ambapo alionyesha kutokuridhika hasa akatilia mashaka katika eneo la vipaza sauti ambako alisema kuwa bado kulikuwa na kazi kubwa ya kufanya.

Hata hivyo, jana Lukuvi licha ya kushuhudia kuwa vimefungwa katika viti vyote, lakini alipotakiwa na waandishi kuwasha kwa majaribio, wajenzi wa ukumbi walizuia na kusema kitaalamu hakutakiwa kuwasha jana kwani kazi ilikuwa bado inaendelea.

Alisema kuwa Ofisi ya Bunge imeshatafuta kumbi nyingine nje ya bunge kwa ajili ya kufanyika mikutano ambayo itahitaji wajumbe zaidi ya 60.

No comments:

Post a Comment