JK kuzindua studio za Azam

 

Studio za Azam Tv 



Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete leo anazindua studio za kituo cha televisheni cha Azam zilizopo Tabata jijini hapa.

Naibu Ofisa Mtendaji wa Azam, Tido Mhando alisema jana kuwa mwitikio wa Rais kwa ajili ya shughuli hiyo ni faraja kubwa.

Mhando alisema viongozi mbalimbali wa dini na Serikali pia wanatahudhuria kwenye uzinduzi huo kuanzia saa tatu asubuhi.

Mhando ambaye aliwahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communication, alisema kuzinduliwa kwa studio hiyo ya kisasa kutaleta chachu ya mabadiliko katika tasnia ya habari.

“Hapo nyuma tulikuwa tukilega lega kwa kiasi fulani, lakini tunaamini uzinduzi huu utaamsha ari ya ushindani katika tasnia ya habari,” alisema huku akimwagia sifa studio hiyo kuwa inaweza kuwa bora kuliko zote Afrika Mashariki.

Alisema studio hiyo ambayo ujenzi wake umegharimu Dola 31 milioni za Marekani, (sawa na Sh55 bilioni), itapanua wigo wa kurusha matangazo na vipindi bora vitakavyohabarisha umma.

“Baada ya uzinduzi huu tunatarajia kuongeza studio nyingine mbili zitakazokuwa ndani ya hii kubwa,” alisema Mhando.

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa kampuni hiyo, Yahaya Mohamed alisema ubora wa studio hiyo utaendana na ubora waandishi wao.

Mohamed ambaye aliwahi kufanya kazi katika Kampuni ya Sahara Media Group alisema uwekezaji huo utafungua milango kwa waandishi.

“Tutakuwa tunapokea kazi za waandishi wengine, lakini jambo la kuzingatia ni ubora wa kazi yako,” alisema Mohamed.

No comments:

Post a Comment