Marekani yakerwa na ziara ya Assad Moscow

Assad na Putin


Marekani imeshutumu Urusi kwa kumpa mapokezi ya taadhima Rais wa Syria Bashar al-Assad mjini Moscow.

"Tunatazama mapokezi ya zulia jekundu aliyopewa Assad, aliyetumia silaha za kemikali dhidi ya watu wake, kuwa kinyume na lengo lililoelezwa wazi na Urusi la kutaka kuwepo na shughuli wa mpito kisiasa Syria,” msemaji wa ikulu ya White House Eric Schultz amewaambia wanahabari.

Afisa wa wizara ya masuala ya ndani ya Marekani alisema taifa hilo halijashangazwa na ziara hiyo, lakini wasiwasi mkubwa kwa Marekani ni Urusi kuendelea kumsaidia kivita Assad.

Alisema hilo litaipa nguvu zaidi serikali ya Assad na hivyo kuendeleza mapigano ya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.

Ziara hiyo ya kiongozi huyo wa Syria Jumanne ilifanyika wiki tatu baada ya Urusi kuanza kushambulia kwa ndege ngome za wapiganaji wa Islamic State na makundi mengine yanayopinga utawala wa Assad.

Ilikuwa ziara ya kwanza kabisa kwa Assad nje ya nchi baada ya mapigano kuzuka Syria 2011. Mapigano hayo ya wenyewe kwa wenyewe yameua watu 250,000.

Akiwa jijini Moscow, Assad alitoa shukrani zake kwa Urusi kuingilia kati kijeshi nchini mwake.

Alisema operesheni hiyo ya Urusi ilikuwa imezuia ugadi kueneza zaidi na kuwa madhara makubwa Syria.

Kwa upande wake, Bw Putin alisema matumaini ya Moscow ni kwamba suluhu ya muda mrefu itapatikana kupitia mchakato wa kisiasa na kwa kushirikisha makundi yote ya kisiasa, kikabila na kidini.

Mwandishi wa BBC aliyeko Moscow Steve Rosenberg anasema kuwa kwa kumkaribisha kiongozi huyo wa Syria mjini Moscow, Putin alikuwa akituma ujumbe mkali kwa mataifa ya Magharibi kwamba Moscow ni mhusika mkuu katika mzozo huo Mashariki ya Kati na kwamba suluhu haiwezi kupatikana bila kuhusisha Urusi.

No comments:

Post a Comment