Serikali ‘yaipiga stop’ Tanesco kupandisha bei ya umeme

Shirika la Umeme Nchini (Tanesco)

Wizara ya Nishati na Madini imelizuia Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) kupandisha bei ya umeme kama lilivyokuwa limepanga kufanya hivyo Januari, mwakani.

Waziri wa Wizara hiyo, Profesa Sospeter Muhongo, alisema hayo juzi wakati akihojiwa kwenye kipindi cha dakika 45 kinachorushwa na Kituo cha Televisheni ya ITV.

“Kumekuwa na madai kwamba, Tanesco watapandisha bei ya umeme ifikapo Januari 2013. Lakini nimewaelekeza Tanesco na Ewura (Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji) wasipandishe bei ya umeme,” alisema Profesa Muhongo.

Alisema ameielekeza Tanesco isipandishe bei kwa sababu katika deni la dola za Marekeni milioni 250 inazodaiwa, serikali imekuwa ikilisaidia kulipa.

Profesa Muhongo alisema hadi sasa serikali imekwishatoa dola za marekani milioni 50 kupunguza deni hilo, ambalo limebaki dola za Marekani milioni 200.

Alisema serikali imepunguza bei ya kuunganisha umeme wananchi ili ifikapo mwaka 2015 asilimia 30 ya Watanzania wawe wanapata nishati hiyo tofauti na sasa, ambapo wanaopata ni asilimia 18.4 tu.

Profesa Muhongo alisema wizara yake imejipanga kuongeza kiwango cha uzalishaji wa umeme kifikie megawati 2,780 kutoka megawati 1,438 zinazozalishwa hivi sasa ifikapo mwaka 2015.

Alisema uzalishaji huo utaongezeka kutokana na mkakati uliopo wa kuongeza vyanzo vya uzalishaji umeme na kwamba, hivi sasa matumizi ya umeme kwa nchi nzima ni megawati 830.

“Mgawo wa umeme haupo na wala hautakuwapo, wengine wanaufurahia uwapo  kwa sababu zao binafsi za kibiashara na kisiasa. Lakini nawahakikishia wananchi hakutakuwa na mgawo wa umeme,” alisema Profesa Muhongo.

Akizungumzia suala la gesi, alisema wizara yake imewasilisha sera ya gesi katika Baraza la Mawaziri na rasimu ya sera hiyo imepelekwa kwa wakuu wa mikoa ili wananchi waweze kutoa maoni yao kabla ya kupelekwa bungeni Februari, mwakani.

Profesa Muhongo alisema rasimu ya sera hiyo imepelekwa katika mikoa, ambayo gesi na mafuta inapatikana na, ambayo inatumia gesi hiyo kwa wingi ni Lindi, Mtwara, Tanga, Pwani, Rukwa (Sumbawanga), Katavi, Mbeya na Arus
ha.

No comments:

Post a Comment