Simba,Yanga viwanjani leo


Timu ya Simba

Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara ambayo imefika kwenye raundi ya 11 ya mzunguko wa kwanza itaendelea leo kwenye viwanja vitano tofauti ambapo timu 10 zitashuka dimbani kuwania pointi tatu muhimu, zikiwamo za Simba na Yanga zilizo kileleni mwa ligi hiyo.

Mechi nyingine ya ligi iliyotarajiwa kufanyika leo kati ya Ruvu Shooting dhidi ya Prisons ya Mbeya imeahirishwa hadi itakapotangazwa baadaye kufuatia ajali ya gari waliyoipata wachezaji wa Prisons wiki iliyopita wakati walipokuwa njiani kuelekea jijini Tanga.

Vinara wa ligi hiyo, Simba, ambao waliwasili Morogoro jana saa 7:00 mchana, watakuwa wageni wa Polisi Morogoro katika mechi itakayofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri wakati watani zao wa jadi, Yanga, wanaoshika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi  watawakaribisha JKT Mgambo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Kocha wa Simba, Mserbia Milovan Cirkovic, aliliambia gazeti hili kwamba wachezaji wake wako tayari kwa mechi hiyo ya ligi na jana jioni walitarajiwa kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Jamhuri ili kuuzoea kabla ya kushuka dimbani leo jioni.

Mserbia huyo alisema kwamba licha ya ushindani mkali wanaokabiliana nao katika mechi zao za mikoani, Simba inataka kuendeleza kasi yake ya kufanya vizuri na hatimaye kuendelea kubaki kileleni mwa msimamo na kutowapa nafasi mahasimu wao, Yanga kuwashusha.

Alisema kwamba amewataka nyota wake kutoidharau Polisi Morogoro licha ya kuonekana kuwa hawakufanya vizuri katika mechi zao zilizopita kwani timu ya aina hiyo huwa ni hatari zaidi.

"Tunatarajia kushinda na nimewaeleza kuwa wasiidharau kwa sababu haijashinda mechi yoyote tangu ligi ilipoanza," alisema kocha huyo.

Kocha Mkuu wa Yanga, Ernest Brandts, alisema kwamba kikosi hicho sasa kimeiva na kinataka kusonga mbele tu.

Brandts alisema kwamba kila siku amekuwa akiwakumbusha wachezaji wake kupambana katika dakika zote 90 za mechi na kutoruhusu wapinzani kukaribia lango lao.

Daktari wa timu hiyo, Juma Sufiani, alisema kuwa wachezaji, Kevin Yondani, Said Bahanunzi na Didier Kavumbagu ambaye jana alirejea mazoezini kuungana na wenzake, wako vizuri na maamuzi ya kucheza au kutocheza yako kwa kocha Brandts.

Daktari huyo alimtaja beki Salum Telela ambaye aliteguka kifundo cha mguu ndiye anayeendelea na matibabu kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na hana nafasi ya kucheza mechi ya leo na ya Jumapili dhidi ya Azam.

Mechi nyingine zitakazochezwa leo ni kati ya Toto Africans dhidi ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa CCM, Kirumba jijini Mwanza huku JKT Ruvu wakiikaribisha African Lyon kwenye Uwanja wa Chamazi, Mbagala na jijini Arusha, wenyeji JKT Oljoro nao wataikaribisha Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.

Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Arusha, kocha wa Mtibwa Sugar, Mecky Maxime, alisema kwamba timu yake haijapata matokeo mazuri hivi karibuni lakini hali hiyo ni ya kimchezo kwa sababu wachezaji wamekuwa wakipambana kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mchezo.

Maxime alisema kwamba wanaamini watazinduka na kurejesha kasi yao kuanzia leo na watatumia vyema uwanja wa nyumbani katika mechi zote zinazofuata.

Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwenye Uwanja wa Chamazi kwa kuzikutanisha Azam inayoshika nafasi ya nne kwenye msimamo dhidi ya Coastal Union iliyo kwenye nafasi ya pili.

No comments:

Post a Comment