Mtoto wa ajabu azaliwa

Mtoto wa ajabu mwenye jinsia ya kike alizaliwa jana katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro huku viungo vyake vya ndani ya mwili vikiwamo utumbo, figo, maini na bandama vikiwa nje.

Muuguzi katika wadi ya kina mama wajazito, Mercy Matogo, alisema walimpokea mama wa mtoto huyo, Hadija Issa, majira ya asubuhi akiwa ana maumivu ya uchungu wa kujifungua, hadi majira ya saa sita mchana alipojifungua mtoto huyo.

Alisema wakati mama huyo akijifungua, walishangaa mtoto kutanguliza vitu vya ndani ya tumbo tofauti na hali ya kawaida kwa watoto wengine ambao hutanguliza kichwa wakati wa kutoka.

Matongo alisema baada ya kumtoa mtoto huyo, walibaini viungo vyake vyote vya ndani ya tumbo viikiaemo maini, utumbo, figo na bandama vikiwa nje.

Aidha, mwili huo haukuwa na kitovu wala sehemu ya haja kubwa wala ndogo, ingawa kitaalamu walibaini kuwa alikuwa ni mtoto mwenye jinsia ya kike.

Waandishi wa habari walishuhudia mtoto huyo aliyedaiwa kufariki muda mchache baada ya kuzaliwa, aliwa  na mguu mfupi ulioonekana kama kukatika kuanzia upande wa goti huku mguu mwingine ukiwa umelegea kama uliovunjika.

Afisa Muuguzi Mkuu wa wadi hiyo, Santieli Kinyingo, alisema tukio hilo ni geni katika wadi hiyo.

Alisema huenda sababu mbalimbali zinaweza kuchangia tatizo hilo kama mjamzito kutumia  dawa za kienyeji au ya kisasa bila ushauri wa kidaktari wakati wa ujauzito.

Mama wa mtoto huyo, Hadija Issa, mkazi wa Msamvu mjini Morogoro, alisema kuwa hiyo ilikuwa ni mimba yake ya kwanza na kwamba hakuwa na dalili zozote mbaya wakati wa ujauzito.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment