Mbatia, Kafulila kumaliza tofauti zao za kisiasa

James Mbatia 


MWENYEKITI wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia amesema chama hicho bado kinatafuta njia bora ya kumaliza tofauti zake na mbunge wake, David Kafulila (Kigoma Kusini).

Kafulila alifukuzwa uanachama Desemba, 2011 pamoja na  wajumbe wengine sita akiwamo aliyekuwa mgombea urais wa chama hicho katika Uchaguzi  Mkuu wa 2010, Hashim Rungwe.

Uamuzi huo ulitolewa kwenye kikao cha dharura cha Halmashauri Kuu (Nec) ya chama hicho kilichoketi Dar es Salaam na kutawaliwa na vurugu mpaka polisi wakaitwa ili kuongeza ulinzi.
Licha ya kuomba msamaha wajumbe wa mkutano huo hawakubadili uamuzi wao, licha ya  Kafulila kupinga uamuzi wa kikao hicho kumvua uanachama kwa madai ya utovu wa nidhamu kwa  kufungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Baada ya siku kadhaa Mahakama hiyo ilitoa amri ya muda ya kusitisha utekelezwaji wa azimio la kikao cha Nec  kilichomvua uanachama Kafulila, kumfanya apoteze sifa ya kuwa mbunge.
Katika vipindi tofauti aliwahi kufanya mikutano ya hadhara katika jimbo lake, na kumfanya Katibu Mkuu wa NCCR, Samwel Ruhuza kuibuka na kumtaka aache kufanya mikutano hiyo kwa tiketi ya chama hicho.

Akizungumza na gazeti hili jana, Mbatia alisema bado chama kinatafuta njia nzuri ya kumaliza tofauti hiyo, kwamba kauli alizowahi kuzitoa mbunge huyo ziliwaudhi baadhi ya watu ndani ya chama hicho.
“NCCR ni taasisi ambayo sio mali ya Mbatia wala mtu yoyote na itaendelea kuwepo hivyo ni lazima masuala ya chama tukayajadili kama chama,”alisema Mbatia.

Alifafanua kuwa suala la mbunge huyo bado linatafutiwa njia nzuri ya kumalizwa.
Mbatia alisema siyo muda mwafaka kulizungumzia suala hilo kwa kuwa NCCR ni chama kinachofanya mambo yake kwa njia za kidemokrasia.

Hata hivyo, alipoulizwa kama suala hilo litajadiliwa nje ya Mahakama alisema kuwa hawezi kueleza kiundani. “Hayo ni mambo ya chama, nisingependa kulizungumzia suala hili, tuacheni tutamaliza mambo yetu ndani  ya chama” alisema Mbatia.

Kwa upande wake, Kafulila aliwahi kulieleza gazeti hili kuwa kama chama hicho kitakuwa tayari kufanya naye mazungumzo yupo tayari kuondoa kesi hiyo mahakamani.

No comments:

Post a Comment