Mkapa akoleza mjadala wa gesi

Rais Mstaafu Benjamin Mkapa 


WITO wa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa kutaka suluhu ya mgogoro wa gesi unaoendelea baina ya Serikali na wakazi wa mikoa ya kusini, umepokewa kwa hisia tofauti. Baadhi ya wasomi wamempongeza huku wakazi kadhaa wa Mtwara wakimpinga.


Juzi, baada ya mgogoro huo kuendelea kwa takriban mwezi mmoja sasa, Mkapa alizitaka pande hizo mbili kutafuta mwafaka akieleza kuwa linalowezekana leo, lisingoje kesho.


“Mtafaruku huu haufai kuachwa na kutishia usalama, mipango ya maendeleo siyo siri, mikakati na mbinu za utekelezaji wake siyo siri. Maelezo yake mazuri yanaweza kutolewa yakadhihirisha namna na kasi ambayo rasilimali zinawanufaisha wananchi wa eneo zilimo na taifa zima,” alisema Mkapa katika taarifa yake.


Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana alisema jana kuwa kauli ya Mkapa ni nzuri, huku akisisitiza kuwa katika suala hilo, lazima utaifa uwekwe mbele.
“Hata wakati wa ujenzi wa Barabara ya Mtwara, wapo waliosema kuwa mikoa ya kusini inatengwa, kauli hizi zilikuwapo tangu zamani, kikubwa ni suala hili kuchukuliwa kitaifa zaidi,” alisema Dk Bana.


Wazee watafuta suluhu Dar
Wazee wa Mtwara Mikindani wako Dar es Salaam kusaka suluhu ya mgogoro huo, baada ya kusema kwamba wamebaini kuwa kutakuwa na uvunjifu wa amani kama suala hilo litaachwa liendelee.


Wakizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, wazee hao walisema suala hilo linaleta hofu kubwa kwa taifa hivyo linapaswa kupatiwa ufumbuzi wa haraka.
Katibu wa wazee hao, Selemani Mademu alisema wananchi wa Mtwara wako tayari kufa kuliko kuona wakidharauliwa katika suala hilo.


Mademu alisema: “Wananchi wa Mtwara wanaamini kuwa kituo cha kuchakata gesi asilia kama kitajengwa Mtwara kitatoa fursa kubwa ya kushawishi wawekezaji ambao watajenga viwanda vitakavyotumia malighafi ya gesi asilia na hivyo kuchochea maendeleo ya Mtwara kwa jumla,” alisema na kuongeza kuwa kama Serikali inaamini kwamba wazo lake la kuisafirisha hadi Dar es Salaam ni jema na lenye manufaa kwa wananchi wa Mtwara, ingejikita katika kutoa elimu badala ya kukaa kimya na kuendelea na kile inachoamini.


“Wanamtwara hatupendi kuendelea kuelezwa kwamba tutanufaika na gesi iliyogunduliwa kwa kuahidiwa viwanda kama ambavyo imekuwa desturi ya Serikali yetu. Tunahitaji vitendo vitawale badala ya ahadi ambazo hazitekelezeki. Kwa mfano barabara, umeme, kuimarishwa kwa bandari, mikopo kwa ajili ya ujasiriamali, viwanda vidogo vya kubangua korosho n.k.” alisema.


Wengine wapinga
Mwenyekiti wa Umoja wa Maendeleo Mikoa ya Kusini (UMMK), Said Mannoro (72) alimshutumu Mkapa akidai kuwa ndiye chanzo cha gesi ya Songosongo kupelekwa Dar es Salaam.


Mzee Mannoro ambaye alifika katika ofisi za gazeti hili, Tabata Relini, Dar es Salaam jana alisema Mkapa anatakiwa kueleza faida walizopata wananchi wa Lindi baada ya gesi ya Songosongo inayozalishwa mkoani humo, kupelekwa Dar es Salaam.


Mbali na mzee huyo, baadhi ya viongozi wa dini na vyama vya siasa nao wamempinga Mkapa wakisema kuwa ushauri wake umeegemea upande mmoja na kwamba alipaswa kumshauri Rais Jakaya Kikwete.


Askofu Mteule wa Kanisa la KKKT Dayosisi Mpya ya Kusini Mashariki, Mchungaji Lucas Mbedule alisema Mkapa, amechelewa kutoa ushauri wake na kwamba kwa hali ya sasa alipaswa kumshauri Rais Kikwete akubaliane na matakwa ya wananchi.

 


“Namheshimu sana Mkapa, lakini amechelewa kutoa kauli yake, yeye alipaswa kumshauri Rais mwenzie. Kutoa tamko lake saa hizi kunatufanya tuwe na shaka naye. Nasikitika kuwa kauli aliyoitoa haitakuwa na msukumo kwa wakati huu,” alisema Mchungaji Mbedule ambaye alishawahi kutoa msimamo wake wa akipinga mradi huo na kuongeza:


“Usiwalaumu kwa kuandamana na kuitisha mikutano, jiulize ungejuaje kama wananchi hawataki mpango wa Serikali wa kusafirisha gesi, kama siyo kupitia maandamano, mikutano na mihadhara? Atambue kuwa suala hili lilianza kabla ya maandamano nani alijua kuwa Mtwara hawataki gesi itoke? Nilidhani amshauri Rais Kikwete asitishe mradi huo.”


Msemaji wa Shura ya Maimamu mkoani Mtwara, Sheikh Abubakari Mbuki alisema: “Tunamheshimu sana Mkapa lakini nachelea kusema amekosea… siku nyingi alikuwapo Mtwara, suala la gesi alilifahamu kwa nini asiliseme mapema? Anaotaka kuzungumza nao wapo Mtwara kwa nini akazungumzie Dar es Salaam?” alisema Sheikh Mbuki na kuongeza:


“Tutaendelea na makongamano, kwa nini afedheheshwe na harakati zetu na asifedheheshwe na kauli za Mkuu wa Mkoa (wa Mtwara, Joseph Simbakalia), Waziri wa Nishati na Madini (Profesa Sospeter Muhongo) na Rais Kikwete, anadhani wao wapo sahihi?... Kubeza maandamano na mikutano ni kuwakosea Wanamtwara.”


Askofu wa Kanisa la Angalikana Dayosisi ya Newala, Oscar Mnung’a akizungumzia tamko la Mkapa alisema: “Nadhani amechelewa… awaite viongozi aliowaachia madaraka awaambie wasipuuzie jambo hili … naunga mkono hoja ya Serikali kukaa pamoja na wananchi wa Mtwara… maandamano ni haki ya msingi ya Kikatiba wasipuuzwe unafikiri wangefanya nini kama hawasikilizwi?”


Aliongeza: “Tanzania tumekuwa mafundi wa kutatua migogoro ya wenzetu, kinawashinda nini katika hili? Hapa ni suala la kuweka wazi mikataba, kama kweli Serikali ina mipango mizuri na wananchi wa Mtwara si iweke wazi. Wanashindwaje kujieleza, kuna nini hapa? Wajibu hoja wasitafute mchawi, mjusi ukimfukuza sana mwisho anakuwa nyoka… wananchi hawa wamesema basi.”


“Lazima sisi (viongozi wa dini) tuseme kwa sababu kwenye waumini wetu wapo maskini… sasa tunaposema, mtu mwingine asianze kumtafuta aliyesema, sioni kama ni busara badala ya kutatua tatizo, anawalaumu watu kuwa ndiyo chanzo cha tatizo… kigugumizi cha nini kama mradi una maslahi na watu wa Mtwara?


No comments:

Post a Comment