J.K kukabidhi Vitambulisho vya Taifa

 

Rais Jakaya Kikwete, leo anatarajia kuzindua mfumo wa Taifa wa Usajili na Utambuzi wa Watu na kutoa vitambulisho vya Taifa katika Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na gazeti hili jana, , Ofisa Habari wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), Rose Mdami alisema maandalizi ya uzinduzi huo yamekamilika na kwamba utahudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa na kimataifa wakiwamo mabalozi na mawaziri wakuu wastaafu.

Alisema katika uzinduzi huo, Rais Kikwete na baadhi ya viongozi wakuu wa kitaifa watapatiwa vitambulisho vyao vya taifa na baadaye vitambulisho hivyo vitatolewa kwa watu wote waliosajiliwa na kuchukuliwa alama za vidole.

Aliongeza kuwa picha na saini za kielektroniki zimechukuliwa na kwamba zoezi hilo litaanzia kwa wabunge, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na watumishi wa umma ambao taarifa zao zimekwishachukuliwa. “Maandalizi yote ya sherehe yamekamilika na kwamba baada ya uzinduzi huu kinachofuata ni kuwapatia vitambulisho watumishi wa umma na wengine ambao taarifa zao zimeshachukiliwa,” alisema Mdami.

Aliongeza kuwa baada ya makundi hayo maalumu watafuatia wananchi wa kawaida kwa awamu ambao watachukuliwa alama za vidole, picha na saini za kielektroniki na hatimaye kuwapatia vitambulisho hivyo.

Kwa mujibu wa Mdami, uzinduzi huo unafanyika baada ya kukamilika kwa hatua mbalimbali ikiwamo ununuzi na upokeaji wa baadhi ya vifaa vya usajili ambavyo ni muhimu na msingi wa ujenzi wa mfumo wa usajili na utambuzi wa watu.

No comments:

Post a Comment