Maafa juu ya maafa, Dar 36 Arusha 20


 

Kile kilichodhaniwa kuwa kilele cha sikukuu ya pasaka, kimegeuka msiba baada ya wachimba kokoto 20 kufukiwa katika kifusi Jijini Arusha.

Hiyo ilikuwa ni kama ndimu katika kidonda kibichi, kwani ni ijumaa iliyopita tu wakati watu wakijiandaa kwa sikukuu ya Pasaka jengo la ghorofa 16 lilidondoka Jijini Dar es Salaam na kuua watu 36.

Vifo hivi vilivyotokea katika msimu wa sikukuu vimeweka idadi ya watu waliopoteza maisha kufikia 56 hivi, ndani ya  siku nne tu.

Watu waliofukiwa na kifusi mkoani Arusha, walikuwa wakichimba kokoto katika eneo la Moshono.

 Imeelezwa kuwa ni maiti 14 tu ndizo zilizoopolewa na watu wengine bado wanahofiwa kuwa ndani ya kifusi hicho.

 Ilikuwa ni saa tano asubuhi, juzi, gema la kokoto liliporomoka kisha kuwafunika wote waliokuwamo ndani, sababu kubwa ikielezwa kuwa ni mvua kubwa zilizokuwa zikinyesha mjini Arusha.

 Vilevile magari mawili yaliyokuwa yamepaki pembeni kwa ajili ya kubeba mzigo huo yalizama ndani ya shimo hilo kubwa la kokoto.

Watu saba walikufa 1997

Inaelezwa kuwa hii ni mara ya pili kwa mgodi huu kuua watu kwani mwaka 1997 wachimbaji wa kokoto walifukiwa na saba kati yao walipoteza maisha.

Tukio la Dar

Mlinzi wa msikiti wa Shia, aliyeshuhudia kudondoka kwa ghorofa hilo amesema  alianza kuona mashine ya zege ikianguka kutoka ghorofa ya 17 ambapo ujenzi wa sakafu ya ghorofa hiyo ulikuwa ukiendelea.

Mlinzi huyo, Athuman Salum Mnere anasema alisikia sauti ya kukatika kwa kitu, ghafla sauti kubwa ya maporomoko, kisha mashine ya zege na baada ya sekunde kadhaa, jengo lote likawa chini.

Anasema walionusurika walianza kuwaokoa watoto waliokuwa wakicheza mpira katika uwanja wa ndani ya msikiti uliokaribu na jengo hilo.
Aliwakanya watoto waliopoteza maisha

Anasema aliwaambia watoto waliokuwa  wakicheza mpira katika uwanja huo waende nyumbani lakini hawakusikia.

Hata kabla ya dakika tano kwisha, jengo hilo liliporomoka na wale wanne waliokuwa wamekaa katika benchi walifunikwa na jengo.

“Wengine waliumia vibaya, ndiyo hao walioko hospitali. Wale waliokuwa kwenye benchi walikufa palepale”anasema.

 Shughuli za uokoaji zilimalizika juzi na eneo lilipokuwepo ghorofa hilo kubaki mithili ya shimo.

 

No comments:

Post a Comment