Mamia wamzika Semdoe Handeni

Mjane wa marehemu Hussein Semdoe akiwa amempakata mtoto wake wamiezi mitatu 

Kilindi. Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda ameongoza mamia ya watu katika kumzika mwandishi wa habari wa gazeti hili, Hussein Semdoe aliyefariki dunia Alhamisi iliyopita kutokana na ajali ya gari iliyotokea wilayani Handeni na kusababisha vifo vya watu watatu.

Dk Kigoda ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Handeni alisema alilazimika kuacha kikao cha baraza la mawaziri na kuruhusiwa na Rais Jakaya Kikwete kuhudhuria mazishi hayo.

Alisema Rais Kikwete amestushwa na vifo hivyo vilivyosababisha vya waandishi wa habari wawili na Ofisa Uhamiaji.

Semdoe alizikwa katika shamba la baba yake Kijiji cha Mafureta wilayani hapa katika mazishi yaliyohudhuriwa na umati wa watu kutoka mikoa mbalimbali wakiwamo wawakilishi wa klabu za waandishi wa habari za mikoa ya Pwani na Morogoro na Tanga.

Mwakilishi wa Kampuni ya Mwananchi Mkoa wa Tanga, Burhani Yakub aliwasilisha kwenye mazishi hayo salamu za Mkurugenzi na wafanyakazi wa MCL.

Alisema: “Mkurugenzi, wahariri, waandishi wa habari pamoja na wafanyakazi wa Mwananchi Communications Ltd kwa ujumla wamestushwa na kifo cha Semdoe na kwamba ameacha pengo kubwa ambalo halitaweza kuzibika kirahisi.”

Alisema wakati wa uhai wake alikuwa tegemeo la kampuni katika kuandika habari za wilaya za Kilindi na Handeni.

Burhan aliwasilisha kwa familia ya marehemu ubani wa Sh 621,000.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Gallawa alifika kwenye mazishi hayo akiwa ameambatana na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa kuwafariji wafiwa.

Akizungumza katika msiba huo, Gallawa alisema, Semdoe na wenzake wamekufa wakati wakilitumikia taifa kwa sababu walikuwa wakienda kupanda miti.

Hata hivyo, Gallawa alilazimika kwenda pia kwenye mazishi ya mwandishi wa habari wa gazeti la Uhuru na Mzalendo, Hamis Bwanga aliyezikwa Muheza. Baadaye pia alienda kuhudhuria mazishi ya Ofisa Uhamiaji Wilaya ya Handeni, mjini Handeni. Wote walikumbwa na mauti katika ajali hiyo.

Marehemu Semdoe ameacha mjane, Mariam Semdoe pamoja na watoto watano; Najma, Hussein, Saadam, Saada na Shakira ambaye ana umri wa miezi mitatu.

No comments:

Post a Comment