Bagamoyo na maeneo ya kihistoria yasiyojulikana

Sehemu ya lango la Mji wa Bagamoyo, wakati wa ukoloni.


Siku chache zilizopita nilitembelea Kitongoji cha Magomeni, mjini Bagamoyo, katika kitongoji hicho nilipiga picha vipande vya nguzo ambayo ni mabaki ya lango la mji huo.

Dereva wa bodaboda aliyenipeleka hapo nilimuuliza kama anaelewa chochote kuhusu kuta hizo mbili, lakini cha ajabu alisema hajui licha ya kuishi  Bagamoyo miaka mingi.

Baada ya hapo nilikutana na dada ambaye anasema amezaliwa na kuishi eneo la Magomeni, lakini hajui maana ya kuta hizo. Nilimwambia kijana kwamba enzi hizo, Bagamoyo ilipokuwa chini ya Wakoloni wa Kiarabu, eneo hilo palikuwa na lango likionyesha mtu anaingia mjini na kwa wenye nchi.

Misafara ya watumwa, wamisionari na wavumbuzi, wafanyabiashara, walipita katika lango hilo. Kuta  nyingine zilizokuwa upande mwingine wa barabara, zimepotea. Kuta nilizopiga picha ziko kwenye uwanja wa mtu. Zinaweza kupotea kwa kuharibiwa wakati wowote.

Pia kulikuwa na nguzo nyingine pale ‘top life bar’ lakini sasa imebaki moja, nyingine imepotea. Nilielezwa na wahifadhi kwamba eneo linalozunguka Caravan Serai, katika soko, na kule kituo cha mabasi kipya lilitumika kujenga kambi za watumwa. Lakini hakuna anayefahamu hilo.

Katika Idara ya Mambo ya Kale, inayoshughulikia masuala ya historia, hakuna maelezo yanayoonyesha eneo hilo kulikuwa na lango hilo. Hakuna kumbukumbu yoyote.

Nimekwenda Bagamoyo mara kadhaa, kila unapotembelea moja ya kivutio cha historia utapata habari tofauti, aidha itatofautiana na ya zamani, au itapotoshwa kidogo. Inafika mahali unashindwa kuelewa ukweli ni upi.

Baada ya kusoma kitabu cha Henry Morton Stanley anaeleza walipoanza safari walipumzika kwenye shamba la mama mmoja, Gonera wa Kihindi, nje ya Bagamoyo. Lakini safari hii niliambiwa Gonera alikuwa ni askari mlinzi aliyejengewa nguzo pale eneo la Mji Mkongwe na von Wisman mwaka 1898.

Inaonekana Bagamoyo ina maeneo mengi ya kihistoria ambayo hayajawekwa katika historia kuu. Na hili ni kosa la idara husika.

No comments:

Post a Comment